Kwa nini ndoa nyingi za leo hazina furaha na amani?
Mungu
alipanga kwamba mtu anapoingia katika ndoa awe anaonja uzuri wa mbinguni na sio
uchungu. Lakini kinyume chake, ndoa nyingi zimekuwa ni jehanamu ndogo. Wanandoa
wana majuto, maumivu, simanzi, majeraha na hofu. Pamoja na ugumu huu, liko
tumaini kwa Mungu aliyeanzisha taasisi hii ya ndoa.
Kwa
utafiti wangu mdogo na kwa ufunuo wa Roho Mtakatifu napenda kukushirikisha
sababu kadhaa za kukosekana kwa furaha na amani katika ndoa nyingi za leo:
1. Makosa katika uchaguzi wa mwenzi wa maisha.
Matatizo
ya ndoa nyingi yanatokana na uchaguzi mbaya. Mungu anasema kwamba uzima na
mauti vyote viko mbele yetu. Ni wajibu wetu kuchagua uzima kwa faida yetu na
vizazi vijavyo. Kum 30:19 ‘nimekuwekea mbele yako uzima na mauti, baraka na
laana; basi chagua uzima, ili uwe hai, wewe na uzao wako’ . Kama mtu
alifumba macho asiangalie matatizo yanayojulikana wazi ya mchumba wake, lazima
avune alichopanda. Tunatakiwa kuwa waangalifu sana kuruhusu moyo kummeza mtu
ambaye hajulikani vizuri. Ukimpenda sana mtu macho yanapofuka hivyo huwezi
kuona wala kukubali kwamba ana matatizo yanayoweza kukugharimu baadaye. Gal 6:7
‘Msidanganyike, Mungu hadhihakiwi; kwa kuwa chochote apandacho mtu, ndicho
atakachovuna’. Pengine ulijua wazi tabia mbaya za mchumba wako lakini
ukazipuuzia kwa vile tu ni tajiri au ni msomi au ni maarufu au umechoka
kusubiri.
Kama
Adamu hangekuwa na subira, angeoa sokwemtu kwa vile wanyama walishaumbwa. Sokwemtu
ndiye alikuwa na sura inayokaribiana na mwanadamu. Isije ikawa umeoa au kuolewa
na sokwemtu kutokana na kukosa subira au kushinikizwa na watu uoe au uolewe na
mtu ambaye si chaguo lako la moyo na wala si mpango wa Mungu.
2. Msingi mbovu katika kuanza maisha ya ndoa.
Kama
mlianza kukutana kimwili kabla ya ndoa kufungwa, lazima msingi utakuwa na nyufa
ambazo baadaye zitaonekana hata kwenye kuta za ndoa yenu. Msingi wa ndoa yenu
ni dhambi na kukosa subira ndiyo maana mnaishi kwa hatia na kutoaminiana. Tendo
hilo linathibitisha kwamba mlikuwa na uwezo mdogo katika kusubiri na kutawala
tamaa za miili yenu. Pia inadhihirisha mlikosa hofu ya Mungu.
Lakini
pia inawezekana mlijiheshimu katika uchumba hadi ndoa lakini hamkuandaliwa
vizuri kuwa mume na mke. Ndoa ni kiwanda cha kuzalisha watu kinachohitaji
meneja mzuri. Lazima wanandoa wakae chini mapema na kupanga wanataka nyumba yao iwe ya aina
gani. Mjenzi hawezi kuamua baadae kuibadilisha nyumba iwe ya gorofa wakati
msingi aliouweka awali ni wa nyumba ya miti. Kwa kuthamini hili mimi niliweka
bajeti ya kukaa na mke wangu siku tano kwenye hoteli baada tu ya arusi yetu ili
tuweke msingi wa nyumba yetu badala ya kulisha watu kifahari siku ya arusi.
Lazima ndoa iwe na kanuni na dira ya kuiongoza.
Wengine
walifichana uhalisi wa maisha yao. Pengine mume hakutaka mwenzake ajue kiwango
chake cha maisha wakati wakiwa wachumba. Jambo hili linasababisha kujikwaa
wakati wa kuishi pamoja. Inashindikana kumpa mke zawadi nyingi kama wakati
wa uchumba kwa vile sasa hakuna wa
kukukopesha. Hivyo mke anakosa hata
mafuta ya kupaka. Ingekuwa bora zaidi kama mwanaume angekuwa muwazi ili
mwanamke apige gharama kama ataishi naye au la badala ya kushtukizwa maisha
ambayo hakuyategemea wala hakujiandaa kuwa nayo. Hata mwanamke pia anapaswa
kuwa muwazi kwa mwenzake tangu mapema.
3. Kutegemea ndugu na kushindwa kuambatana.
Kuna
wana ndoa ambao hawana maamuzi binafsi katika masuala ya nyumba zao. Kwa nje
wanaonekana kama mume na mke lakini katika uhalisia ni ‘remote control’ ya
ndugu zao. Wanaongozwa kwa mbali kama mtu anayewasha TV kwa rimoti. Kwa maneno
mengine, ni bendera fuata upepo. Hawajaweza kutekeleza maagizo makuu matatu ya
Mungu ya kuacha, kuambatana na kuwa
mwili mmoja. Mwa 2:24 ‘Kwa hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake
naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja’. Haiwezekani kuwa mwili mmoja
(kuunganishwa kimwili, kiroho na kimawazo) kabla ya kuwaacha wazazi na
kuambatana. Kuacha wazazi sio kuwasahau bali ni kujitegemea katika kuiongoza
nyumba yako. Si lazima mfumo wako wa kuongoza ufafanane na wa wazazi wako.
Kuambatana ni kuwa marafiki wa karibu kuliko yeyote mwingine. Kuna msemo
unaosema, ‘Out of sight, out of mind’, yaani, ukiwa humuoni mtu kwa karibu,
anatoka kwenye mawazo yako. Kadiri wanandoa wanavyokuwa mbali, ndivyo kila
mmoja anavyomsahau mwenzake na wakati huohuo mwingine aliye karibu anaingia
moyoni kuziba pengo lililopo. Hatimaye, mlango wa zinaa unakuwa wazi. Lazima
jitihada zifanyike za kuhakikisha hakuna mwanya au ufa unaotokea kwa watu
waliounganishwa kuwa mwili mmoja.
4. Kumsahau aliyeanzisha ndoa.
Watu wengine hawakumshirikisha
Mungu katika kupata mwenzi wa maisha isipokuwa wanataka tu Mungu aibariki ndoa
yao. Mungu alianzisha ndoa kwa malengo ya kusaidiana katika kumtumikia. Mungu
hakuwaumba Adamu na Hawa kwa faida zao wenyewe bali watawale, wamiliki na
kuitiisha nchi. Mwa 1:28 “Mungu akawabarikia, Mungu akawaambia, Zaeni,
mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na
ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.” Kinyume
chake wengi wanadhani ndoa ni kwa ajili ya kujifurahisha tu wao wenyewe. Na hii
ndiyo sababu watu wengi wakioa au kuolewa wanaacha kufanya kazi ya Mungu na
matokeo yake wanaishi katika laana. Kum 28:30a, 47 ‘Utaoa mke na mtu
mwingine atalala naye...kwa kuwa hukumtumikia BWANA, Mungu wako, kwa furaha na
moyo wa kushukuru, kwa ajili ya ule wingi wa vitu vyote’. Yeyote anayetaka
Mungu aiponye na kuisimamia ndoa yake ajiulize kwanza swali hili: ‘Mungu
ananufaika nini na ndoa yangu?’
5. Kuthamini pesa kuliko utu (ubinadamu).
Kuna
wanandoa ambao wamejenga upendo wao katika mafanikio ya kimwili. Kwa hiyo,
mwenzi ana thamani kama tu ana pesa. Msingi huu unasababisha ndoa iyumbe hali
ya uchumi inapobadilika. Ndoa inatakiwa ithamini mpango wa Mungu na utu kuliko
kitu kingine chochote. Vinginevyo, mtu atatafuta zaidi pesa kuliko kuwa na
faragha na mwenzi wake. Matokeo yake ukaribu (intimacy) unapungua, upweke alioukimbia
unajitokeza tena na maana halisi ya ndoa inatoweka. Kumbuka Mungu
anawaunganisha mume na mke ili kudhibiti upweke (Mwa 2:18). Kuna watu wengi
siku hizi ni ‘married singles’ badala ya kuwa ‘married couples’. Yaani, mtu
anaonekana kwa nje kwamba ameoa au kuolewa lakini kwa ndani yuko peke yake. Mtu
yuko tayari atafute pesa na kusahau umuhimu wa mahusiano. Lazima pesa tunazozipata
ZITUTUMIKIE NA SIO SISI KUZITUMIKIA. Pesa zisaidie kuijenga familia na sio
kuibomoa. Mama mmoja alikuwa mkweli kwa mumewe aliyekuwa anajali tu kutuma pesa
lakini harudi nyumbani. Alimwambia, “Nashukuru kwa pesa unazotuma lakini naomba
usisahau kwamba sikuolewa na pesa zako!”
6. Kuingia katika ndoa kabla ya kujua kwamba ndoa ni
majukumu.
Wapo wanaoingia katika ndoa
kichwakichwa bila maandalizi ya msingi ya maisha. Mungu hakumpa Adamu mke hadi
pale alipohakikisha amempa bustani ya kulima na kuitunza (Mwa 2:15-17). Ni
kweli kwamba Mungu hapendi mtu awe peke yake lakini alishughulikia upweke wa
Adamu baada ya kumpa kwanza bustani na majukumu. Hawa naye aliumbwa ili
kumkamilisha Adamu. Ndiyo maana Mungu alitoa ubavu wa Adamu akautumia kumuumba
Hawa. Mungu alitaka kila mmoja amuhitaji mwenzake.
Lazima
kila mmoja ajue majukumu yake katika ndoa. Pamoja na ukweli kwamba wanandoa
wanapaswa kusaidiana lazima kila mmoja
ajue majukumu yake. Wapo watu wanaosema kazi zote ni za mume ikiwa ni pamoja na
kupika na kudeki na mke ni msaidizi anayesaidia tu pale inapobidi. Tatizo hili
linatokana na kutafsiri neno msaidizi kwa lugha ya kiswahili au kingereza badala
ya lugha ya kiebrania iliyotumika katika kuandika Agano la Kale. Neno msaidizi
ni EZER KENEGDO – mwanamke ni mtu mwenye nguvu wa kumuokoa mwanaume. Kumbuka
hata Roho Mtakatifu anaitwa pia msaidizi lakini haina maana kwamba ni mdogo
kwetu wala haina maana kwamba anatusaidia tu pale tukishindwa. Roho Mtakatifu
ni msaidizi kwa maana ya ‘kuwa karibu kututia nguvu ya kutenda’. Mke anayejua
vizuri wito wake anatakiwa awe mfariji au muwezeshaji. Mwanamke ana hadhi sawa
na mwanaume isipokuwa tu majukumu yao yako tofauti. Kama kuumbwa kabla
kunasababisha mume awe wa maana zaidi kuliko mke (kwa wanaoamini waliumbwa kwa
nyakati tofauti), basi itabidi sokwe mtu naye awe wa maana zaidi kuliko mume
kwa vile aliumbwa kabla ya Adamu. Hata hivyo tusisahau kwamba mfumo dume
ulianzishwa na Mungu mwenyewe ingawa hauna maana ya kumnyanyasa mwanamke. Ndiyo
maana Mungu alichagua kuitwa baba na sio mama. Huu sio udhalilishaji bali ni
ugawaji wa majukumu kwa utukufu wake mwenyewe. Maumbile yenyewe yanaonyesha
kwamba Mungu alikusudia tofauti ziwepo kwa ajili ya mume na mke kuhitajiana. Ingawa
wote wana haki sawa, lazima pawe na kiongozi. Hakuna ‘authority sharing’ yaani,
kugawana madaraka. Ndiyo maana mke akaitwa msaidizi na sio msimamizi. Mungu
aliweka tofauti kati ya mke na mume kwa vile mtu anavutiwa zaidi na kitu asicho
nacho ili akamilike (opposites attract). Tofauti hizi za kimaumbile ni kwa
ajili ya kukamilishana na sio kushindana. Hivyo tuufurahie na kuulinda uumbaji
wa Mungu wetu bila kuukosoa. Kuna vitu mwanaume anaweza zaidi kuliko na
mwanamke na kuna vitu mwanamke anaweza zaidi kuliko mwanaume. Sina haja ya
kusema uwezo wa mwanaume maana unajulikana. Lakini mwanamke ana uwezo wa ajabu
aliopewa na Mungu ili kumuokoa (kumlinda mwanaume). Na shetani kwa kulijua hilo
anawatumia baadhi yao vibaya. Mfano, mwanamke ana uwezo wa kuhisi kitu kwa
haraka bila kufikiri kwanza (intuition). Mke anaweza kukuambia huyu mtu
unayetaka kufanya naye biashara atakudhulumu. Ukipuuzia halafu ukadhulumiwa,
unaanza kumlaumu mkeo kwamba amekulaani. Tuutumie huu uwezo wao kwa faida ya
familia zetu.
7. Kutotambua kwamba shetani aliyevuruga
ndoa ya kwanza hajafa
Shetani
anabuni mbinu mpya usiku na mchana kwa ajili ya kuharibu ndoa na familia. Siku
moja ndugu mmoja aliyeokoka alikuwa safarini kwenye ndege. Alipoona jirani
waliyeketi naye anaomba kwa bidii alimuomba washirikiane maombi. Yule ndugu
akamwambia, “Mimi ni muabudu shetani (satanist) na siku ya leo tunaomba ndoa za
watu wa Mungu zivunjike.” Ndoa yenu inayumba kwa vile shetani amefanyia kazi
maombi ya watu wake (waabudu shetani). Watu wengi wanaoanguka kwenye ndoa
hawafanyi makusudi bali wanalishwa limbwata. Wanakamatwa mioyo yao kwa uchawi
mpaka wanajikuta wanamfuatilia mtu ambaye hakuwa na mvuto wowote kwake na
hatimaye kutelekeza familia zao. Unashangaa mtu anang’ang’ana na mtu na
kumkabidhi pesa zote huku familia inateseka. Lazima maombezi yenye nguvu na mamlaka
yafanyike ili kuwatoa watu katika mashimo walikowekwa ndipo watakumbuka familia
zao na kujutia dhambi zao.
Hata
kama kuna makosa yalifanyika huko nyuma, Mungu anaweza kuponya na kuhuisha ndoa
za watu wake wanaomkimbilia kwa imani bila kukata tamaa.
Naomba
kwamba:
1.
Mungu akusaidie ukubali makosa uliyofanya na kuuendea msalaba bila kuficha
dhambi zako ili ndoa yako iponywe na kurejezwa.
2.
Mungu akusaidie kuwa karibu na mwenzi wako kuliko mtu mwingine yeyote hata kama
umelazimika kuwa mbali naye kikazi au kimasomo.
3.
Mungu akupe macho ya kuwatambua majini-watu ambao unadhani wanavutia kumbe ni
mawakala wa kukuingiza katika ufalme wa giza.
4.
Mungu ahuishe tena ndoa yako iliyochoka ili usiishi mazingira hatarishi na
ambayo hayampi Mungu utukufu.
Pokea
majibu ya maombi haya katika Jina la Yesu Kristo!
Dr. Lawi Mshana, +255712924234, Tanzania