Ticker

6/recent/ticker-posts

Tuwasaidie watoto, vijana na walimu washinde uhatarishi mashuleni


 Tuwasaidie watoto, vijana na walimu washinde uhatarishi mashuleni

Tumeanza mpango wetu wa kutambua uhatarishi na majanga na kusaidia katika kutafuta ufumbuzi kwa kutumia mbinu shirikishi. Leo tumekutana na watoto na vijana (adolescents and youth) wa umri wa miaka 10-24 kupitia programu yetu ya Kijana Nitatoboa. Napenda kukushirikisha kama mdau ili uhusike katika kufanya sehemu yako. Huu sio wakati wa kulalamika au kulaumu bali ni wa kufanya unaloweza ili kupunguza madhara na kumlinda mtoto na kijana. Tuunge mkono juhudi za serikali kwa kufanyia kazi yale tunayoyaweza kama jamii, wazazi, walimu, viongozi na wanafunzi pia.

 

Washiriki wa mdahalo wa leo wametaja uhatarishi ulioko kwenye mashule kama ifuatavyo:

 

Tunachapwa kupitiliza mpaka mwanafunzi anajisaidia muda huohuo wa adhabu, mwalimu anatunyima ruhusu ya kwenda kujisaidia mpaka mwanafunzi anajikuta amejisaidia darasani, chumba cha darasa kina ufa ambao ni hatarishi, monita anasingizia kwamba mwanafunzi amepiga kelele kama hatampa rushwa ya sh 200, monita akiomba kalamu ukimnyima anakuandika kwamba umepiga kelele hivyo unaadhibiwa bila kosa, unaporipoti ofisini kwamba kuna mwanafunzi amekupiga unaambiwa, ‘Na wewe kampige!’, tunalazimishwa kununua bidhaa ili tusiadhibiwe, mwanafunzi anapewa simu ili kuwasiliana kwa siri na kuhakikishiwa kwamba hatafeli somo lake.

 

Kuna matumizi mabaya ya vyoo (wanafunzi hawamwagi maji kuflashi vyoo hata kama yapo), ukosefu wa maji vyooni unasababisha matumizi ya vitu vinavyoziba mfumo wa maji taka kwenye vyoo, wanafunzi wanaandika matusi kwenye kuta za vyoo, taulo za kike zinatupwa kwenye vyoo vya kuflashi na kusababisha vyoo kuziba kwa vile hakuna mahali maalum pa kuzitupa na pa kuzichoma.

 

Tunapigwa na wanafunzi wakubwa na kuonywa tusithubutu kusema na kama utamwambia mwalimu, mwanafunzi huyo anakusubiri ukitoka shule ili akupige vizuri, baadhi ya wanafunzi wanaandikiana barua na kukabidhiana kwa siri muda wa darasani. Mmojawapo anasema aliandikiwa barua lakini hakujua hatua za kuchukua.

 

Nilipowauliza kama wanajua simu za dharura wanapokutana na uhatarishi au majanga, niligundua kwamba wanajua chache sana. Lakini pia inaonyesha kwamba hakuna sehemu maalum za kupatiwa huduma ya kwanza wanapopata matatizo ingawa kinadharia wanajua kutaja vifaa vyote muhimu kuwepo kwenye sanduku la huduma ya kwanza.

 

Mwisho

Tutumie tathmini hii ndogo kuwalinda watoto, vijana na walimu dhidi ya uhatarishi ulioko shuleni. Naamini tukipata nafasi ya kuwahoji walimu pia tutagundua kwamba wanakutana na uhatarishi mwingi unaotakiwa pia kufanyiwa kazi. Msongo wa mawazo unaweza kumfanya mtu afanye mambo mengi ambayo hayakutarajiwa katika jamii iliyostaarabika.

 

Beyond Four Walls, Korogwe, Tanga