Ticker

6/recent/ticker-posts

Hesabu gharama kabla ya utekelezaji wa mpango wako

Hesabu gharama kabla ya utekelezaji wa mpango wako

Maono: Nimeona mtu akisema afadhali kwa sasa apange nyumba kwenye eneo ambalo ni salama kwake na mali zake na barabara zinapitika kuliko kujenga nyumba mbali ambapo hakuna usalama na barabara haipitiki kwa gari lake.

Maono haya hayana maana ya kukatisha tamaa watu kujenga. Ila yanatufundisha tu umuhimu wa kuhesabu gharama kulingana na wakati na kazi anayoifanya mtu. Mtu anaweza kulipa gharama kubwa ya pango lakini anaingizia kipato kikubwa kuliko akikaa nyumba ya bure aliyoijenga mwenyewe mahali penye gharama kubwa za ziada kv usafiri, usalama nk.

Kuna watu wengi wanapenda kusingizia ‘imani’ mahali ambapo panahitaji ‘mipango’ na ‘mikakati’. Wanasahau kwamba ingawa Bwana Yesu anatutaka tuishi kwa imani kuna mahali ametufundisha kwamba tuhesabu gharama ili tusije tukaaibika na kuchekwa.

Lk 14:28-31 “Maana ni nani katika ninyi, kama akitaka kujenga mnara, asiyeketi kwanza na kuhesabu gharama, kwamba anavyo vya kuumalizia? Asije akashindwa kuumaliza baada ya kuupiga msingi, watu wote waonao wakaanza kumdhihaki, wakisema, Mtu huyu alianza kujenga, akawa hana nguvu za kumaliza. Au kuna mfalme gani, akitaka kwenda kupigana na mfalme mwingine, asiyeketi kwanza na kufanya shauri, kwamba yeye pamoja na watu elfu kumi ataweza kukutana na yule anayekuja juu yake na watu elfu ishirini?”

Ili kukazia ujumbe wake, Bwana Yesu aliamua atoe mifano ya aina mbili tofauti yenye maana moja ya kututahadharisha kwamba TUSIKURUPUKE bali TUJITATHMINI KWANZA NA KUJIRIDHISHA KWAMBA TUNAWEZA. Alitumia mfano wa UJENZI na mfano wa VITA. Tuache tabia ya ‘kukopa na kuahidi kwamba tutalipa kwa imani.’ Lazima tuwe na mkakati wa ulipaji unaoeleweka. Tusijiingize kwenye miradi au vita ambazo iko wazi kwamba adui ana nguvu au silaha za kisasa kuliko sisi. Tunashauriwa tutumie njia ya kidiplomasia zaidi kuliko kujipanga kwa vita tusizoziweza.

Mfano hai: Katika semina ya vijana niliwaomba tupige mahesabu ya kulinganisha kipato cha mfanyakazi wa nyumbani (house girl/boy) na waajiriwa kwenye steshenari, ofisi nk. Tukagundua kwamba wanalipwa kati ya sh 80,000 mpaka 150,000 kwa mwezi lakini wanajitegemea malazi, umeme, maji, chakula, matibabu na pango. Na sio rahisi baada ya matumizi hayo abaki na sh 50,000 kama faida. Tulipoondoa gharama za ziada kwa msichana wa kazi tuligundua mtu anayejitegemea anaweza kumfikia kama atalipwa mshahara usiopungua 250,000 kwa mwezi. Hata hivyo inategemea mfanyakazi wa nyumbani anafanya kazi kwa nani. Maana kuna watu hawashindwi kumkata msichana wa kazi posho yake anapohitaji Panadol. Hawana huruma kiasi kwamba wanathubutu kumnyanyasa mtu anayewapikia. Hawaogopi kulishwa vitu vichafu. Lakini pia wazazi wa wasichana wa kazi wengine wanawanyanyasa kwa kuchukua mshahara wote bila huruma. Lakini huu unyanyasaji haupo kwao tu. Hata walioajiriwa pia wanakutana na unyanyasaji katika sehemu za kazi.

Mambo kadhaa ya kujifunza kuhusu utendaji wa Mungu tunayemuabudu

1. Alipopanga kumuumba mwanadamu alishirikisha (kikao kilifanyika)

Mwanzo 1:26 “Mungu akasema, Na tumfanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu; wakatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na wanyama, na nchi yote pia, na kila chenye kutambaa kitambaacho juu ya nchi.”

Hapa tunaona Mungu ambaye angeweza kuumba tu mwenyewe anasema, “Na tumfanye mtu.” Lakini pia akashirikisha huyo mtu awe na sifa zipi. 1. Awe na sura ya Mungu kv utashi. Malaika hawana uwezo huo. Wao wanatumwa tu kutekeleza maagizo. 2. Awe mtawala wa viumbe vingine na mazingira yake.

Mungu hakumtengenezea Adamu barabara wala kumjengea nyumba bali alimpa akili na ubunifu wa kubadilisha mazingira yake.

2. Aliumba kwa utaratibu maalum

Mwa 1:12,13 “Nchi ikatoa majani, mche utoao mbegu kwa jinsi yake, na mti uzaao matunda, ambao mbegu zake zimo ndani yake, kwa jinsi yake; Mungu akaona ya kuwa ni vyema. Ikawa jioni ikawa asubuhi, siku ya tatu.”

Mungu hakushindwa kuumba vitu vyote kwa sekunde moja. Lakini aliamua kutufundisha kuwa na ratiba na utaratibu kwa kuzingatia nini kianze na kipi kifuate. Lakini pia alitathmini kwanza kazi aliyoifanya ndipo akaumba nyingine – Mungu akaona kuwa ni vyema.

Watu wengi leo wamelemewa na matatizo kwa sababu tu hawana VIPAUMBELE. Mfano, mtu hana nyumba ya kukaa ananunua gari na kulipaki polisi. Mwingine badala ya kusoma kwanza anaamua aoe na kujikuta masomo yanamshinda. Mwingine ananunua sofa ili ajionyeshe wenzake sebuleni wakati hana kitanda chumbani. Mwingine anatumia pesa zote kwenye kusomesha kwa gharama kubwa bila kuwekeza katika maisha yake binafsi. Matokeo yake anataka kuwaalani watoto wakishindwa kumsaidia wanapopata kazi nk.

3. Mungu hakumuumba mwanadamu mpaka alipomtengenezea mazingira

Mwa 1:27,28 “Mungu akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimwumba, mwanamume na mwanamke aliwaumba. Mungu akawabarikia, Mungu akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.”

Kwa vile Mungu alijua mwanadamu atahitaji hewa, mwanga, maji, chakula nk alihakikisha anatanguliza vitu hivyo. Mara ngapi umenunua vitu ambavyo kwa sasa havina faida kwako. Mfano, mtu anakushawishi ununue kifaa kinachotumia umeme mwingi na unakinunua wakati nyumba yako sio tu kwamba haina umeme bali hukuwa na mpango wa kuweka miundombinu ya umeme mkubwa.

Lazima tujifunze kufanya upembuzi yakinifu (feasibility study) ili kujiridhisha kama kuna uwezekano wa kufanikiwa katika mipango tunayoifanya. Unaweza kudhani ukihamia mji fulani utafanikiwa kwa vile utalipwa mshahara mkubwa na kumbe gharama za maisha za mahali hapo ziko juu sana.

Ndiyo sababu kila tunapotaka kufanya kazi zetu za kiroho na kijamii tunaingia gharama kufanya tathmini. Hii inatuepusha na maumivu mengi yasiyo na sababu.   

4. Mungu anatenda miujiza anapoona hakuna uwezekano kibinadamu

Yoshua 5:12 “Ndipo ile mana ikakoma siku ya pili yake, baada ya wao kuyala hayo mazao ya nchi; na hao wana wa Israeli hawakuwa na mana tena; lakini wakala katika viliwa vya nchi ya Kanaani mwaka huo.”

Mungu hatendi miujiza kama mazingaumbwe. Anakuwa na sababu. Kwa mfano, wana wa Israeli walipewa mana jangwani kwa vile hapakuwa na uwezekano wa kulima mazao wakiwa safarini. Lakini Mungu alipoona wanaweza kujilimia na kuvuna, hakuwapa tena mana. Jifunze kufanya yote unayoweza kufanya kwa nguvu zako na kumuachia Mungu kwa lile tu ambalo liko juu ya uwezo wako aliokujalia.

Marko 6:47,48 “Na kulipokuwa jioni mashua ilikuwa katikati ya bahari, na yeye yu peke yake katika nchi kavu. Akawaona wakitaabika kwa kuvuta makasia, kwa maana upepo ulikuwa wa mbisho; hata ilipopata kama zamu ya nne ya usiku akawaendea, akitembea juu ya bahari; akataka kuwapita.” Bwana Yesu alitembea juu ya maji kwa vile wakati wanafunzi wakipambana na dhoruba baharini Yeye alikuwa nchi kavu. Haikuwepo mashua nyingine ya kumfikisha pale walipo. Hapo ndipo akatumia uwezo wake wa Kiungu ambao hauhitaji mashua za kibinadamu.

Kuna watu wanaaibika kwa vile wanasubiri miujiza hata kwa mambo ambayo Mungu amewapa uwezo wa kuyafanya.

Maombi ya wiki hii:

1. Ee Mungu naomba unifundishe jinsi ya kushirikisha maono yangu kwa watu sahihi ili nisikwame.

2. Ee Mungu naomba unifundishe kuwa na mpangilio wa shughuli zangu nijue naanza na lipi na kumaliza na lipi ili nisijilaumu wala kukulaumu ninaposhindwa.

3. Ee Mungu naomba uniwezeshe kutambua wakati muafaka wa kufanya kila jambo ili nisipate hasara zinazoepukika.

4. Ee Mungu naomba unisaidie nijitambue ili nisikungoje kwa mambo ambayo ulishanipa uwezo wa kuyafanya.

Kumbuka ku-follow kurasa zetu na kujiunga na makundi yetu ili uendelee kupata mafundisho ya kukua katika neema ya Mungu na kushinda changamoto za maisha.

Lawi Mshana, 0712-924234