Ticker

6/recent/ticker-posts

UNATESWA NA SONONA NA HUJUI UFANYEJE? (sehemu ya pili)

JE UNATESWA NA SONONA (DEPRESSION) NA HUJUI UFANYEJE? (Sehemu ya pili) 

Katika sehemu ya kwanza tulipata utangulizi, mifano ya viongozi mashuhuri waliokuwa na sonona na vyanzo vya sonona.

Nitajuaje kwamba nina sonona?

 

Tafsiri ya sonona inabadilika mara kwa mara, lakini kwa ujumla lazima mtu awe na angalau moja ya dalili zifuatazo muda mwingi kwa siku, takriban kila siku, kwa wiki mbili au zaidi ndipo ahesabike kitabibu kwamba “ana sonona”.

 

·       Kujisikia huzuni, kusononeka au kuwa mtupu (empty)

·       Kupoteza shauku au furaha katika takriban shughuli zote.

 

Zaidi ya hayo, lazima mtu huyo awe na mambo zaidi ya matatu au manne katika haya yafuatayo takriban kila siku kwa wiki mbili au zaidi:

·       Kuongezeka sana au kupungua sana kwa hamu ya kula

·       Kulala sana au kidogo sana

·       Kufadhaika au kuwa goigoi

·       Kuchoka au kukosa nguvu

·       Kujihisi huna thamani au hatia

·       Kupungua uwezo wa kufikiri au kuamua

·       Kuwa na mawazo ya kufa au kujiua

 

Dalili hizi lazima zikufikishe kwenye kudhoofika kwa utendaji wako wa kila siku. Hata kama hujawa na sonona mafunzo haya yanaweza kukusaidia.

 

Nifanye nini kama nina sonona?

 

Wapo washauri wa afya wanaoweza kusaidia ingawa hawapatikani maeneo mengi na unaweza kulazimika kulipia huduma hii. Lakini kama unajisikia kuwa na mawazo ya kujiua, inaonyesha kwamba unahitaji msaada wa haraka kutoka kwa mtu mwingine zaidi ya wewe mwenyewe. 

 

Zifuatazo ni “Kanuni za Jumla za Uwakili wa Nafsi” ambazo mojawapo inaweza kukusaidia katika kuanza kujihudumia.  

 

1.    Soma vifungu vya Maandiko vinavyofaa katika kuelezea hisia na mawazo ya watu wanapokuwa na sonona. Kwa mfano, omba Zaburi 13 pamoja Mfalme Daudi, kiongozi wa watu wa Mungu. Pia soma vifungu vya Maandiko vilivyojaa matumaini, kama vile Zab 40, 42 au 2 Kor 1:3-11. 

2.    Tafuta mafunzo kuhusu sonona kwenye Internet kama ilivyo kwenye huu ukurasa wangu wa Facebook. Kumbuka tovuti zenye .gov na .edu zina taarifa za kuaminika zaidi.

3.    Soma vitabu na majarida mazuri kuhusu sonona.  

4.    Tunza orodha ya dalili za sonona ili ugundue matukio yanayotokea kabla ya hali kuwa nzuri au mbaya. Kisha epuka matukio yanayotangulia sonona na ongeza ushiriki wako katika matukio au mawazo yanayozuia au kupunguza sonona.

5.    Tafuta njia za kujizawadia kwa kufikiri au kutenda katika namna inayopunguza sonona unapogundua kinachosaidia. Kwa mfano, kama kwa kusema, “Hili pia litapita” kunasaidia, jipige kikofi cha upendo (pat) mgongoni kwa kusema, “Naamua kusema na nafsi yangu namna hii katika maombi yangu.”

6.    Fanya shughuli ambazo ziliwahi kukufurahisha, hata kama hudhani kama zitakupa furaha sasa. Kama hukumbuki chochote, fanya mambo ambayo wengi wanayafurahia kama vile, kusikiliza nyimbo, kufurahia uumbaji au kusoma kitabu kizuri.

7.    Tenga muda wa kufanya matembezi katika mwanga wa jua kwa vile mwanga wa jua mara nyingi unasaidia kupunguza sonona.

8.    Ungama kosa au dhambi kwa mtu uliyemkosea ili kukabili hatia.

9.    Kabili kwa namna inayoonyesha kujali kama unataka kumkabili mtu kuhusu mambo anayofanya ambayo yanakuumiza wewe au wengine.

10.Omba msaada kwa marafiki wanaoaminika, familia, matabibu au wanasihi (washauri nasaha).  

11.Fanya uchaguzi kuchukua hatua ya kwanza katika kuweka miguu kwenye maombi yako kwa ajili ya kushinda sonona kwa kuamua kufanya jambo unaloweza kulifanya mwenyewe leo.

12.Mwambie mtu fulani kuhusu uamuzi wako wa kuchukua hatua uliyoamua katika kufanya jambo fulani. Mwombe mtu huyo kukuwajibisha kwa kuchukua hatua hiyo.

13.Dhihirisha huzuni, simanzi na maumivu ya kupoteza. Isaya mara nyingi anatafsiriwa kwamba anamzungumzia Yesu kama “Mtu wa Huzuni” (53:3-4). Yohana pia aliandika kwamba “Yesu alilia” (11:35). Usizuie kulia ili mradi usiwe kama watu waliopoteza tumaini.

14.Weka shabaha katika kutafakari mambo yo yote yaliyo ya kweli, yo yote yaliyo ya staha, yo yote yaliyo ya haki, yo yote yaliyo safi, yo yote yenye kupendeza, yo yote yenye sifa njema, yaliyo mema (Fil 4:8).  Haya ni mambo yanayotupa tumaini. Vua “miwani ya giza” na tazama mema yanayotoka kwenye hali yako ngumu.

15.Unaweza pia kutumia tibalishe inayofaa kushughulikia sonona.

16.Baada ya kuonana na daktari, kama yupo, taratibu anza mazoezi kwa muda usiopungua dakika 20 kama mara tatu hivi kwa wiki. Haya mazoezi yamethibitisha kusaidia kupunguza sonona.

17.Jilazimishe kuwa na watu hata pale unapokuwa hujisikii kufanya hivyo. Ukiwa na sonona unajisikia kujitenga na wengine, lakini kuwa na watu sahihi kunasaidia sana kupunguza sonona.

18.Kama huwezi kujichanganya na watu kijamii, muombe mtu akupe msukumo wa kuwa na watu wengine hata unapokuwa hujisikii kufanya hivyo.

19.Tafuta mtu au kikundi ambacho unaweza kushirikisha mapito yako. Kama ambavyo umelia nao waliao, waruhusu wengine nao walie na wewe. Ukiwa katika upweke, wapo watu wanaoweza kukutegemeza hata kwa kupitia mtandao.  

20.Dhibiti mawazo yako unayojisemea ambayo yanapoteza tumaini lako. Kisha jiambie, “Acha!” Usiendelee kufikiri namna hiyo lakini chagua kurudia mawazo ya kweli na yenye matumaini.

21.Soma au imba au sikiliza nyimbo au pambio au muziki mwingine wa Kikristo ambao unaleta tumaini.  

22.Tafakari mambo yaliyosaidia zamani wakati ulipokuwa umesononeka. Kisha yafanye mambo hayo tena.  

23.Uliza watu wengine walifanya nini waliposononeka. Kilichofanya kazi kwa wengine kinaweweza kufanya kazi kwako pia.

24.Andika mawazo yako na hisia zako kwenye karatasi. Tunga shairi. Tunga wimbo unaoelezea maumivu ya sonona yako na tumaini la uponyaji.  

25.Fanya kitu kusaidia mwingine bila matarajio ya kurudishiwa chochote. Hii itakusaidia kuondoa hali ya kujiwazia zaidi na kuanza kuwasaidia wengine. 

26.Usiogope kuwainamisha wengine kwako. Unaweza kuwapa fursa ya kukuhudumia – na unaweza kuwa mfano mzuri kwamba na wewe unaweza kupata madhara usiposaidiwa.

27.Kipekee omba mwongozo wa Roho Mtakatifu kuhusu kinachosababisha sonona na jinsi ya kukishughulikia. Kumbuka kwamba Roho Mtakatifu ni Tabibu mkuu.

28.Waombe wengine wakuombee kipekee kuhusu sonona na athari zake.

29.Tumia vizuri huduma za uponyaji zinazopatikana kanisani kwako.

30.Kama kila unachofanya hakisaidii, jaribu kupambanua jinsi Mungu anavyoweza kutumia sonona yako katika muktadha mpana wa ufalme wake.

 

·        Inaweza kukuandaa vizuri kwa wengine kwa kukupa ushirikeli (empathy)  (2 Kor 1:3-7).

·        Inaweza kukufanya uzidi kuwa mnyenyekevu na kumtegemea Mungu (2 Kor 12:7).

·        Inaweza kuzaa baraka za kiroho (Yk 1:12) au kudhihirisha nguvu ya Mungu (Yn 9:1-7).

·        Inaweza kuwa ishara kwamba u mali ya Kristo (1 Pet 4:12-19).

·        Mungu anaweza kuitumia kupima uaminifu wako (Kitabu cha Ayubu).

 

Inawezekana usiweze kufanya mambo haya yote, na si lazima yote yafanye kazi kwa kila mtu. Hata hivyo, unaweza kuhitaji mojawapo au baadhi katika kushughulikia sonona yako.

 

Mungu akusaidie ili utoke katika kifungo hicho na kujiona kwamba una thamani kubwa na unapendwa na Mungu.


Dr. Lawi Mshana, +255712924234, Tanzania