Ticker

6/recent/ticker-posts

Kipindi cha Maswali na Majibu kuhusu Utoaji kinaendelea (swali la 5 hadi 7)


Kipindi cha Maswali na Majibu kuhusu Utoaji kinaendelea (nimejibu swali namba 1 hadi 4 katika Makala zilizopita. Sasa ni swali namba 5 hadi 7.

Swali la 5. Kuna mtu amekuwa akiniombea na kunishauri kwa njia ya mtandao. Sasa ameniambia nimtumie sadaka ya shukrani. Je, nimtumie?

Kama mtu huyo angekuwa ni mtaalamu wa ushauri nasaha ambaye anahitaji kulipwa ada ya ushauri, hapo hakuna shida. Ni sawa na kumuona wakili kwa ajili ya kesi yako ambaye unamlipa kwa huduma yake ya kitaalamu.

Huyu mtu anayekuombea na kukushauri kiroho kwa njia ya mtandao, alipaswa kukujulisha tangu mwanzo kwamba anataka huduma yake ilipiwe. Kimsingi anapokuambia umpe sadaka ya shukrani ana maana hii:

1. Anataka umlipe kwa huduma anayokupatia ingawa hapendi kukutajia kiasi maalum cha kutoa kwa vile anaogopa kwamba ataonekana sio mtumishi wa Mungu.

2. Anataka kuchukua nafasi ya Mungu katika maisha yako. Mtu anapotoa sadaka ya shukrani, hampi mchungaji au kiongozi wa dini bali anampa Mungu. Hata kama sadaka hiyo itatumiwa na kuhani, haina maana mtoaji amempa kuhani. Matumizi ya sadaka yanasimamiwa kwa kanuni maalum za Neno la Mungu kwa watumishi wake.

3. Hatambui kwamba wewe una kanisa na pia una kiongozi wa kiroho anayekulea. Ingawa ukipata changamoto za maisha hataweza kukusaidia kwa vile yuko mbali, hatambui taabu ya viongozi wako wanaukulea kiroho.

Nashauri viongozi tutafute njia za kuingiza kipato zinazokubalika kwa vile hatujakatazwa kufanya kazi baada ya muda wa huduma zetu za kiroho. Lakini tusitoze watu kwa huduma ambazo tumepewa bure na kukatazwa kulipisha watu. Mathayo 10:8 “Pozeni wagonjwa, fufueni wafu, takaseni wenye ukoma, toeni pepo; mmepata bure, toeni bure.”

Swali la 6. Ni lazima nitoe malimbuko ya kila mazao ya shamba langu au naweza kutoa ya shamba moja tu?

Kila shamba linahitaji baraka zake kwa vile changamoto zake ni tofauti na pengine mazao yake pia ni tofauti. 2 Mambo ya Nyakati 31:5 “Mara ilipotangaa amri, wana wa Israeli wakatoa kwa wingi malimbuko ya nafaka, na divai, na mafuta, na asali, na mazao yote ya mashamba; na zaka za vitu vyote wakazileta nyingi.” Nehemia 10:35 “tena kuleta malimbuko ya ardhi yetu, na malimbuko ya matunda yote ya miti ya namna zote, mwaka kwa mwaka, nyumbani kwa Bwana.”

Kusudi la malimbuko ni KUKALISHA BARAKA KATIKA NYUMBA YAKO. Ezekieli 44:30 “Na kitu cha kwanza cha malimbuko yote ya vitu vyote, na kila toleo la kila kitu cha matoleo yenu, litakuwa la makuhani. Tena mtampa kuhani sehemu ya kwanza ya unga mbichi, ili kukalisha baraka juu ya nyumba yako.” Kumbuka unaweza kupata baraka na zisikae (zisidumu) bali ziwe kama zinazopita tu. Unashika pesa nyingi mkononi lakini hazikufanyii kitu cha maana katika maisha yako. Unatakiwa kutoa malimbuko ili baraka zako zidumu. 

Swali la 7. Ni sawa kutoa sadaka kama mbegu katika madhabahu ya Mungu kwa mahitaji maalum?

Wengi wetu tumezoea kutoa sadaka siku za ibada peke yake. Hatujui kwamba sadaka ni njia ya kujiunganisha na madhabahu ya Mungu kila unapoiendea kwa suala nyeti. Waabudu shetani wanajua sana kanuni hii kwa mungu wao.

Lazima tujue kwamba madhabahu haina maana kama hakuna SADAKA na KUHANI WA MADHABAHU HIYO. Kwa hiyo unapotoa sadaka kwenye kanisa ambalo hujajiridhisha kwamba kuhani wake ni wa kweli, unahatarisha maisha yako. Akiitumia sadaka yako vibaya lazima utapata madhara.

Kumbuka kuna wakati Mungu anatupa ‘mbegu’ na wakati mwingine anatupa ‘mkate’. 2 Wakorintho 9:10 “Na yeye ampaye mbegu mwenye kupanda, na mkate uwe chakula, atawapa mbegu za kupanda na kuzizidisha, naye atayaongeza mazao ya haki yenu.” Mungu anapokupa mbegu anataka upande ili usife njaa msimu ujao. Anapokupa mkate anakutia moyo ule vizuri kwa vile ulipanda msimu uliopita. Maana yake ni kwamba sio wakati wote tunatakiwa kupanda mbegu. Wakati mwingine tunafurahia mavuno ya upandaji wetu.

Kwa hiyo ni sawa kutoa sadaka kama mbegu kwa ajili ya hitaji maalum. Unaweza kufanya hivi kwa mtumishi ambaye ana funguo za baraka zako. Usiwe mwepesi kutoa sadaka kwa mtumishi ambaye hujui madhabahu yake ni ya aina gani. Kum 12:13,14 “Ujihadhari usitoe sadaka zako za kuteketezwa katika kila mahali upaonapo; bali katika mahali atakapopachagua Bwana katika kabila zako mojawapo, ndipo utakapotoa sadaka zako za kuteketezwa, ndipo utakapotenda yote nikuamuruyo.”

Dr. Lawi Mshana, 0712-924234, Korogwe, Tanga