Ticker

6/recent/ticker-posts

Tahadhari kwa wanawake wanaoenda kuombewa kwa faragha (go to TRANSLATE and select your language for translation).


Tahadhari kwa wanawake wanaoenda kuombewa kwa faragha 
(Safety tips for a woman attending private prayer sessions 
alone with a man)

Kama unaombewa na mtumishi wa jinsi tofauti na wewe, zingatia mambo yafuatayo:

1. Fahamu historia ya mtumishi anayekuombea. Hakikisha huyo mtumishi amepona katika maeneo ambayo anakuombea. Usimuendee mtumishi ambaye ndoa yake mwenyewe imemshinda au yuko karibu na wanawake wengine kuliko mwenzi wake wa maisha. Usimuamini mtumishi kwa kumtazama tu akiwa anahubiri madhabahuni.  Siku moja nikiwa nafanya semina mahali fulani, mama mmoja aliniambia kuhusu mabaya yaliyomkuta. Hitaji lake lilikuwa kubwa kwa mchungaji hivyo mchungaji huyo akampa rufaa aende kwa askofu kuombewa. Huyo mama aliniambia kwa machozi kwamba alijikuta akianguka kwenye uzinzi na askofu huyo badala ya kupata ufumbuzi wa tatizo lake. Kipofu akimwongoza kipofu mwenzake, watatumbukia shimoni wote wawili (Mt 15:14).

2. Ombewa mahali sahihi. Si vizuri kufanyiwa maombi mkiwa peke yenu kwenye chumba na mlango umefungwa. Ni vizuri kuwa katika eneo ambalo madirisha na milango iko wazi kama vile kanisani wakati wa mchana. Hii inasaidia msijaribiwe na muweze kulinda ushuhuda. Hata hivyo kuna wakati shetani anapenda kuharibu ushuhuda kwa kulifanya pepo lililolipuka limkimbize nje na kusema ananibaka. Ndiyo maana katika huduma ya kukemea mapepo haifai mtu awe peke yake. Wakati nafanya semina Dar, mapepo yalilipuka kwa dada mmoja wakati wa maombezi. Wahudumu walipokuwa wamembeba wanamleta madhabahuni bila watu kutegemea akavua sketi na hakuwa amevaa underskirt. Hivi ndivyo shetani anavyofanya ili kuaibisha watu na kuvuvia wengine roho ya uzinzi. Unadhani hili lingetokea ofisini wakiwa wawili tu nini kingetokea? Hata kama hawangezini kimwili, wangezini moyoni!

3. Usipangiwe muda wa kuombewa mara kwa mara bila sababu. Mnapozoeana kupita kiasi na mtumishi, adui anaweza kupata nafasi. Sio rahisi watu ambao hawajazoeana kupanga mipango ya kufanya dhambi. Labda kwa waliobobea sana katika dhambi ya zinaa. Mara nyingi watu wanaanguka wanapofikia hatua ya kuzoeana sana na kuanza kutaniana kiasi kwamba hawaheshimiani tena. Jifunze kuweka mipaka katika mahusiano yoyote hasa na watu wa jinsi tofauti na wewe. Mfano, hakuna sababu ya kuitwa mara kwa mara ili uombewa labda kama katika vipindi hivyo huendi peke yako. Maombi hayana mipaka hivyo mtu anaweza kuendelea kuombewa hata akiwa mbali bila kukutana mara kwa mara.

4. Msiwe na siri kati yenu bila sababu. Mfano msiwe na siri ambazo huwezi kumwambia mumeo au mtu mwingine wa karibu na wewe. Labda tu kama ni siri ambazo ukimjulisha mwenzi wako zitaleta madhara ya kiusalama. Mfano, kama umegundua kwamba amehusika katika jambo fulani la kishirikina kuhusu wewe kv kutaka kukutoa kafara. Lakini siri za masuala ya ndani ya ndoa mkiwa wawili tu zinaweza kumsisimua mmoja wenu na kuanza kuvutiwa kimapenzi. Ni vizuri zaidi kuombewa na mtumishi akiwa pamoja na mkewe au na wahudumu wengine wa jinsi mchanganyiko (wanaume na wanawake). 

5. Kuwa macho na namna unavyoombewa. Mfano usiruhusu kuombewa kwa kushikwa shikwa kila sehemu katika mwili wako. Pia omba kimoyomoyo ukivunja roho zote zilizo kinyume na Mungu kabla hujawekewa mikono. Kuna mtu alibakwa baada ya kuwekewa mikono. Alipowekewa tu mikono alilala usingizi na alipoamka akahisi hali ambayo sio ya kawaida. Alihisi kama kuna mtu amemuingilia kimapenzi. Alipouliza akaambiwa ni uponyaji unaendelea katika mwili wake. Mara nyingi watu wa aina hii wana viapo ambavyo kama mteja atasema alichotendewa anaweza kufa. Labda tu kama mteja huyo ataombewa na mtu mwenye mamlaka ya kuvunja maagano ya kimapepo ndipo aseme alichofanyiwa.   

6. Vaa nguo za heshima unapoenda kuombewa ili uwe salama na usiwatie majaribuni watumishi wa Mungu. Vaa gauni la heshima, refu ambalo halijakubana badala ya sketi fupi na blauzi fupi kwa vile ni rahisi kufunuka hasa mapepo yakilipuka. Hata hivyo ndani unaweza kuvaa nguo zilizokubana vizuri ili isiwe rahisi ukikumbana na mtu anayetaka kukubaka. Sio tu katika kuombewa bali hata safarini katika mazingira hatarishi. Kumbuka mtumishi anayeombea anaweza kuwa dhaifu kiroho au anaweza kuwa amebobea katika kuzini na watu anaowaombea. Ukiwa hujavaa nguo za heshima unaweza kumfanya ajaribiwe hata kama hakuwa amekusudia kwa vile na yeye ni mwanadamu. Neno la Mungu limetuonya kwamba tusimpe Ibilisi nafasi. (Efe 4:27)

Lawi Mshana, Freelance Facilitator & Public Speaker, +255712924234, Tanzania