
Kwa kipindi sasa nimekuwa nikiombea watumishi wa Mungu
waijue kweli na kuisimamia katika makanisa yao na Mungu afungue milango ya
kufanya semina ambazo hazina ubaguzi wa kimadhehebu kwa ajili yao.
Maono: Usiku wa kuamkia jana niliona yakitajwa matatizo
matatu ya wachungaji. La kwanza, hawajui majukumu yao ya msingi. La pili,
hawajui kugawa madaraka na la tatu, wameacha kazi zao na kufanya kazi za
wengine. Niliona wengine wakifanya kazi za mashemasi.
Maono haya hayana maana kwamba wachungaji wote wana
mapungufu hayo. Ila Mungu anatuonyesha maeneo ambayo yanahitaji msaada ili watumishi
wafanye kazi waliyoitiwa itakayowafanya wapate thawabu na kuwa na matokeo
chanya katika huduma zao.
Napenda kuzungumzia mapungufu hayo matatu. Mwongozo huu
unaweza kuwasaidia hata wale ambao ni viongozi wanaosimamia familia na taasisi
mbalimbali.
1.
Hawajui majukumu yao ya msingi
Kuna watumishi ambao hawajui majukumu
wala mipaka ya kazi zao. Anatumika kwa dharura kulingana na mahitaji
yanayojitokeza. Hana ratiba kwamba leo atafanya kazi gani na kesho ataanza na
kazi ipi. Anapohubiri au kutumika hana lengo wala shabaha. Anahubiri kwa
kufurahia na kusisimka lakini hana lengo maalum. Haijulikani kama anahamasisha,
anafurahisha, anatafuta mabadiliko fulani yatokee au anataka watu wafikie hatua
fulani. Biblia imeonyesha kusudi na lengo la Mungu kuita watumishi wake.
Makusudi hayo ni kukamilisha watakatifu, kazi ya huduma itendeke na mwili wa Kristo ujengwe. Kiwango cha juu tunachotakiwa kulifikisha kanisa ni KUMFAHAMU SANA MWANA WA MUNGU NA KUFIKIA CHEO CHA KIMO CHA UTIMILIFU WA KRISTO. Efe 4:11-13 “Naye alitoa wengine kuwa mitume, na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa wachungaji na waalimu; kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa Kristo ujengwe; hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa imani na kumfahamu sana Mwana wa Mungu, hata kuwa mtu mkamilifu, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo.”
Mungu alipoita watumishi wake aliwapa maelezo ya kazi (Job
Description) na namna ya kujitathmini (self-evaluation). Mfano, mtume Paulo
alijui vizuri ameitiwa nini na anatarajiwa kuleta matokeo gani. Mdo 26:18 “uwafumbue macho yao, na kuwageuza waiache
giza na kuielekea nuru, waziache na nguvu za Shetani
na kumwelekea Mungu; kisha wapate msamaha wa dhambi zao, na urithi miongoni
mwao waliotakaswa kwa imani iliyo kwangu mimi.” Mungu alichotaka kwake sio kupewa jina au wadhifa fulani
bali aone watu wakifunguliwa na kumuacha shetani, wamgeukie Mungu na kupokea
msamaha na urithi wao kutoka kwa Mungu. Mara ngapi tumejitathmini kwamba ni
wangapi wamefanyiwa mambo hayo kupitia huduma zetu? Tunaendelea kuhubiri na
kuimba lakini wengi tunaowahudumia bado wamechoka na kukata tamaa na hatujali
wala kujihoji.
2.
Hawajui kugawa madaraka
Kuna watumishi wanafanya kila kazi wenyewe. Wamehodhi
madaraka. Ingawa mtumishi ameteua au ana viongozi wasaidizi chini yake, wapo
kama mapambo au vivuli tu lakini hawaamini na kuwaachia majukumu. Bado watu
wanamuendea kwa kila aina ya tatizo. Tena kiongozi mwingine anapoona watu
wamepunguza kumuona kutokana na kazi nzuri ya wasaidizi wake, anakasirika na
kuwasema vibaya hadharani. Kutokana na hofu hii anashindwa hata kusafiri na
kuwaacha wasaidizi wakiendeleza huduma. Watumishi wa aina hii sio wa kwanza
kutokea duniani. Kipindi cha Biblia Musa alipoitwa alikuwa pia na mtazamo huu
ambao ungemdhoofisha na kukwamisha huduma yake nzuri. Kwa vile Mungu anatumia
watu, Musa alishauriwa na mkwe wake achague watu wenye sifa ili washughulikie
mambo madogo na yale makubwa ndiyo wamletee. Kutoka 18:17-22 “Mkwewe Musa akamwambia, Jambo hili
ufanyalo si jema.Huna budi utadhoofika wewe, na hawa watu walio pamoja nawe
pia; maana jambo hili ni zito mno kwako; huwezi wewe
kulitenda peke yako….Zaidi ya hayo utajipatia katika watu hawa watu walio na
uwezo, wenye kumcha Mungu, watu wa kweli, wenye kuchukia mapato ya udhalimu;
ukawaweka juu yao, wawe wakuu wa maelfu, na wakuu wa mia, na wakuu wa hamsini,
na wakuu wa kumi; nao wawaamue watu hawa sikuzote; kisha, kila neno lililo
kubwa watakuletea wewe, lakini kila neno dogo wataliamua wenyewe; basi kwako
wewe mwenyewe utapata nafasi zaidi, nao watauchukua huo mzigo pamoja nawe.”
3.
Wameacha majukumu yao na kufanya ya wengine
Mtumishi wa Mungu anaweza kuitwa Mchungaji au
Kasisi lakini kazi anazofanya ni za mashemasi. Jambo hili linaleta mgongano na
manung’uniko mengi. Mitume walikutana na changamoto hii wakaanzisha
ushemasi mara moja ili wasitoke kwenye lengo kuu la kitume ambalo ni MAOMBI na
NENO. Mdo 6:3,4 “Basi ndugu, chagueni
watu saba miongoni mwenu, walioshuhudiwa kuwa wema, wenye kujawa na Roho, na
hekima, ili tuwaweke juu ya jambo hili; na sisi
tutadumu katika kuomba na kulihudumia lile Neno.” Watumishi wengine hawana nafasi hata ya kusifu na kuabudu
ibadani wala hawawezi kushiriki vipindi vya maombi. Wanazurura tu muda wa ibada
wakati wengine wakiendelea kumsifu Mungu. Tukifika hatua ya kutingwa na kazi za
ofisini na kuacha NENO na MAOMBI tumeshatoka kwenye wito tulioitiwa. Tunatakiwa
kuwaandaa watu wafanye kazi za ofisi ili tuendelee na wito wetu wa msingi.
Sijui kazi zako ni zilezile za wito ulioitiwa au umeziacha na kufanya za watu
wengine?
HITIMISHO
Katika mwili wa Kristo (Kanisa) mifupa
(skeleton) ni uongozi na nyama (flesh) ni waumini. Ukuaji wa mwili wenye afya
unahitaji maeneo yote (mifupa na nyama) yakue kwa uwiano sawa. Wengi
tunasisitiza sana kanisa likue kiidadi na kusahau ukuaji wa uongozi. Matokeo
yake tunakuwa na watu wengi makanisani lakini hawamjui Mungu, hawajui kuomba,
hawafanyi huduma yoyote, wamechoka kiroho na wametawaliwa na dhambi. Kazi yao
kubwa ni kutoa tu sadaka na zaka na kutarajia kuombewa na kutabiriwa. Watu wa
aina hii hata kama ni wengi wanaitwa washirika/washarika na sio wanafunzi kama
tulivyopewa Agizo Kuu. Washirika/washarika WANAJIUNGA NA KANISA lakini
wanafunzi WANAFANYWA/WANATENGENEZWA. Sijui kama kwa vigezo hivi tuna
wanafunzi wangapi mpaka sasa makanisani. Mathayo 28:19 “Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza
kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu.”
Kiongozi pia anatakiwa kukua kama anataka kuwa
na wanafunzi badala ya washirika/washarika. Kiongozi anapitia hatua kama za
kwenye timu ya mpira (Mchezaji, nahodha, kocha, meneja). Huduma inapoanza
mchungaji anafanya kazi zote pamoja na waumini kama MCHEZAJI. Baada ya muda
anatakiwa kubadilika na kuwa NAHODHA WA TIMU. Hapa anaendelea kucheza lakini
pia ni kiongozi. Ni kama monita anavyoongoza wenzake darasani wakati yeye pia
ni mwanafunzi. Hatua inayofuata ya
kiongozi anakuwa KOCHA. Hachezi uwanjani lakini lazima awaandane wachezaji kwenye
mazoezi na na kuwafuatilia uwanjani. Hatua ya juu kama kiongozi ni kuwa MENEJA
WA TIMU. Anaweza kutokuwepo uwanjani kama alivyo kocha lakini mambo yanaenda
kwa vile amewaandaa wengine. Kwa hiyo sasa anapanga mipango ya kuboresha timu,
maslahi ya wacheza nk. Nimekutana na wachungaji wenye makanisa makubwa lakini
kiuongozi hawajakua kabisa matokeo yake kazi wanazofanya haziendani na idadi ya
watu wanaowasimamia. Mchungaji asipojua kuwaandaa vizuri waumini kwa ajili ya
huduma atashangaa wakichangia tu sherehe na burdani zao na kusahau kabisa kazi
ya Mungu. Mchungaji anaweza kulalamika lakini ukweli ni kwamba amepungukiwa
ujuzi wa uongozi. Mfano, kanisa lina waumini wengi lakini mchungaji ndiye
anaenda kuchukua barua za kanisa posta, kupanga viongozi wa sifa, kushauri
baada ya ibada kwa masaa mengi na tena watu wanamuona kwa matatizo ambayo
yangeshughulikiwa na wasaidizi wake nk
Maombi:
1. Ee Mungu naomba uwasaidie wachungaji
watumike katika viwango vyako ili wafikie kusudi na malengo yako.
2. Ee Mungu naomba unisaidie nisimame
katika nafasi yangu kama mwanafunzi wa Yesu na sio mshirika/msharika tu wa
kanisa.
3. Ee Mungu naomba ufungue milango ili
watumishi wako wapatiwe mafunzo ya mara kwa mara ya uongozi ili amani yako
itawale katika huduma ulizowapa.
Lawi Mshana