Ticker

6/recent/ticker-posts

Huwezi kujitakasa bila kujua kwanza uchafu ni nini na usafi ni nini

HUWEZI KUJITAKASA BILA KUJUA KWANZA UCHAFU NI NINI NA USAFI NI NINI

Ufufuo wa Yesu ni tukio muhimu sana katika maisha yetu. Kama Bwana Yesu hangefufuka, Ukristo wetu haungekuwa na maana. Na kama tunaitwa Wakristo kwa ajili ya maisha ya hapa duniani peke yake kuna mambo mawili ya kutafakari:

(1). Sisi ni maskini kuliko watu wote. 1 Kor 15:19 “Kama katika maisha haya tu tumemtumaini Kristo, sisi tu maskini kuliko watu wote.”

(2). Maana ya kuabudu na kujitakasa itakuwa haipo. 1 Kor 15:32 “…..Wasipofufuliwa wafu, na tule, na tunywe, maana kesho tutakufa.”

Sasa basi, kama tunaamini kuna maisha mengine tena halisi kuliko haya, tunahitaji kutakaswa na damu ya Yesu. 1 Yohana 1:9 “Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote.” Kuungama ni kukiri au kukubali kwamba umemkosea Mungu na sio kukariri maneno na kuyarudia mara kwa mara.

Hata hivyo wengi bado hatujanufaika na nguvu ya damu ya Yesu kwa vile hatujui kama tumechafuka na wala hatujui kama kuna uwezekano wa kusafika. Lazima uwe na tafsiri sahihi kuhusu uchafu wa mwili, nafsi na roho na namna uchafu huo unavyoweza kuondolewa. 2 Kor 7:1 “Basi, wapenzi wangu, kwa kuwa tuna ahadi hizo, na tujitakase nafsi zetu na uchafu wote wa mwili na roho, huku tukitimiza utakatifu katika kumcha Mungu.”

Ayubu anaomba kwamba Mungu amjulishe dhambi yake:

Ayubu 13:23 “Maovu yangu na dhambi zangu ni ngapi? Nijulishe kosa langu na dhambi yangu.”

Bila kumruhusu Roho Mtakatifu atusaidie hatutaweza kutambua dhambi zetu. Kazi mojawapo ya Roho Mtakatifu ni kutufanya tujisikie hatia tunapokuwa tumetenda dhambi (convict). Yohana 16:8 “Naye akiisha kuja, huyo atauhakikisha ulimwengu kwa habari ya dhambi, na haki.” Bila Roho Mtakatifu tutaendelea kutetea dhambi na mwisho zitatupeleka pabaya.

Lakini pia Neno la Mungu lililo hai linachoma na kumfanya mwenye dhambi ajitambue na kuchukua hatua. Waebrania 4:12 “Maana Neno la Mungu li hai, tena lina nguvu, tena lina ukali kuliko upanga uwao wote ukatao kuwili, tena lachoma hata kuzigawanya nafsi na roho, na viungo na mafuta yaliyomo ndani yake; tena li jepesi kuyatambua mawazo na makusudi ya moyo.”

Neno la Mungu linachoma kuliko sime na kuweka wazi mawazo na makusudi ya moyo. La kusikitisha wengine wanapochomwa na Neno wanatafuta mapungufu ya mhubiri ili waweze kujitetea. Wakati huohuo wengine wakichomwa na Neno wanaanguka mbele za Mungu kwa machozi na kuchukua hatua za mabadiliko.

Sishangai kwa vile hata kipindi cha Biblia watu ‘walipochomwa mioyo’ waliitikia kwa namna mbili tofauti:

1. Kundi la kwanza ni la wale ambao walihitaji msaada zaidi ili wapone

Mdo 2:37 “Walipoyasikia haya wakachomwa mioyo yao, wakamwambia Petro na mitume wengine, Tutendeje, ndugu zetu?”

2. Kundi la pili ni la wale ambao walipinga na kuamua kumuua mhubiri

Mdo 7:54,58 “Basi waliposikia maneno haya, wakachomwa mioyo, wakamsagia meno. wakamtoa nje ya mji, wakampiga kwa mawe. Nao mashahidi wakaweka nguo zao miguuni pa kijana mmoja aliyeitwa Sauli.”

TAHADHARI

1. Usipende kujifariji wakati njia zako hazikubaliki mbele za Mungu. Usisahau kwamba hata wanaokufariji kwamba uko sawa hawajawahi kwenda mbinguni. Usichague maneno ya kusikiliza kwa vile tu unayapenda. Mungu atahukumu kwa kutumia Biblia na sio utashi binafsi wa wahubiri.

Mithali 16:25 “Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu; Lakini mwisho wake ni njia za mauti.”

2. Usipoangalia utakuwa kibao cha kuongoza wengine wakati wewe mwenyewe huendi mbinguni. Hakuna kibao kinakwenda kule kinakoelekeza watu ingawa kimesaidia wengi kufika. 1 Kor 9:27 “bali nautesa mwili wangu na kuutumikisha; isiwe, nikiisha kuwahubiri wengine, mwenyewe niwe mtu wa kukataliwa.”

3. Usidhani kila mahali panafaa kujitakasa. Fanya uchaguzi mzuri wa kanisa la kuabudia. Huwezi kujitakasa wakati uko na watu ambao uchafu ni kawaida ya maisha kwao. Wanatenda dhambi kwa makusudi kabisa.

2 Wakorintho 6:17,18 “Kwa hiyo, Tokeni kati yao, Mkatengwe nao, asema Bwana, Msiguse kitu kilicho kichafu, Nami nitawakaribisha. Nitakuwa Baba kwenu, Nanyi mtakuwa kwangu wanangu wa kiume na wa kike.”

Uwe makini usilishwe matango mwitu badala ya Neno la Mungu. Usiwaze kuwasaidia wengine wakati wewe mwenyewe huko salama. Jali kwanza usalama wa roho yako. 2 Fal 4: 39,40 “Na mmoja wao akaenda nje kondeni ili kuchuma mboga, akaona mtango-mwitu, akayachuma matango-mwitu, hata nguo yake ikawa imejaa, akaja akayapasua-pasua sufuriani; kwa maana hawakuyajua. Basi wakawapakulia hao watu ili wale. Ikawa, walipokuwa katika kula chakula, wakapiga kelele, wakasema, Mauti imo sufuriani, Ee mtu wa Mungu. Wala hawakuweza kula.” 

Linda sana moyo wako kuliko yote ulindayo. Mithali 4:23 “Linda moyo wako kuliko yote uyalindayo; Maana ndiko zitokako chemchemi za uzima.”

Lakini pia uwe na kiasi katika sikukuu hii ukizingatia kwamba katika Agano Jipya hatukuagizwa kuikumbuka siku ya Pasaka bali kumkumbuka Bwana Yesu ambaye ndiye Pasaka wetu. Bwana Yesu mwenyewe ametuagiza kwamba tumkumbuke kwa kushiriki meza ya Bwana. Hivyo Bwana Yesu awe kipaumbele chetu kuliko siku yenyewe ingawa hatukatazwi kusherehekea.

1 Kor 5:7 “Basi, jisafisheni, mkatoe ile chachu ya kale, mpate kuwa donge jipya, kama vile mlivyo hamkutiwa chachu. Kwa maana Pasaka wetu amekwisha kutolewa kuwa sadaka, yaani, Kristo.”

1 Wakorintho 11:23,24 “Kwa maana mimi nalipokea kwa Bwana niliyowapa nanyi, ya kuwa Bwana Yesu usiku ule aliotolewa alitwaa mkate, naye akiisha kushukuru akaumega, akasema, Huu ndio mwili wangu ulio kwa ajili yenu; fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu.”

Maombi:

 1. Ee Mungu naomba unijulishe dhambi yangu ili nisijifariji kumbe nakukosea.

2. Ee Mungu naomba unipe hofu yako ninaposikiliza Neno lako. Nisichague neno ninalotaka kusikia kwa sababu ya kiburi.

3. Ee Mungu naomba unifunulie watu ninaotakiwa kujitenga nao na nisiguse vitu vichafu ili niwe mwanao.

Lawi Mshana