Ticker

6/recent/ticker-posts

MAFANIKIO YA KWELI YANAHITAJI MAGEUZI YAANZIE KWAKO MWENYEWE


 MAFANIKIO YA KWELI YANAHITAJI MAGEUZI YAANZIE KWAKO MWENYEWE

Mara nyingi tunatumia nguvu kubwa kujaribu kubadilisha watu wengine na mazingira yetu na kujisahau sisi wenyewe. HUWEZI KULETA TOFAUTI KAMA KAMA WEWE MWENYEWE HUTAKUWA MTU WA TOFAUTI. WEKEZA KWAKO MWENYEWE! Hatuhitaji tu MABADILIKO bali MAGEUZI katika maisha yetu.

Mifano ya mageuzi katika Biblia

1. Sauli alihitaji kupata mageuzi kabla ya kuwa mfalme wa Israeli

Moja ya matokeo ya upako wa Sauli ilikuwa kugeuzwa awe mtu mwingine. Huwezi kupakwa mafuta kwa kusudi fulani, halafu uendelee kuonekana vilevile.

1 Sam 10:6na roho ya Bwana itakujilia kwa nguvu, nawe utatabiri pamoja nao, nawe utageuzwa kuwa mtu mwingine.

2. Unahitaji mageuzi katika fikra zako na sio kiroho peke yake

Kuna watu wengine wamempokea Bwana Yesu moyoni lakini hawajamruhusu awafanye upya katika fikra zao. Matokeo yake mipango yao haipangiki na haitekelezeki.

Rum 12: 2Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.

3. Unahitaji kujua kwamba kuokoka sio kumaliza safari bali ni mwanzo wa safari ya mageuzi

Kuna baadhi ya watu waliookoka ambao wanadhani kuokoka ni kukiri tu bila kuwa na matokeo dhahiri. Wanatafsiri vibaya maandiko matakatifu. Hawajui kwamba kuokoka ni MWANZO WA SAFARI na sio MWISHO WA SAFARI. Wanasahau kwamba wana wa Israeli waliokoka na mikono ya Farao Misri wakiwa wanaume laki 6 (sawa na milioni 3 tukihesabu pia wanawake na watoto) na wakafika Kanani WAWILI TU miongoni mwao. Wengine wote waliofika walizaliwa wakiwa safarini. Maana ya ‘YAMEKUWA MAPYA’ ni MAISHA MAPYA YAMEANZA yaani kuanza safari mpya ya kiroho hadi ufikie hatima uliyopangiwa na Mungu na sio kuhudhuria tu ibada ukihesabu miaka ya umri wako.

2 Kor 5:17Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya.

4. Ukiwa kiriba cha kale huwezi kubeba divai mpya – utapasuka

Maono mapya yanahitaji kukuta mbeba maono mpya. Kama mbeba maono uko kizamani, maono mapya yatakuletea madhara na yatapotea. Unaweza kuwa na maono mazuri lakini wewe mwenyewe hufai kuyabeba maono hayo. Bwana Yesu anasema maono mapya yatakupasua kama hujaandaliwa kuyabeba.

Lk 5:37,38Wala hakuna mtu atiaye divai mpya katika viriba vikuukuu; na kama akitia, ile divai mpya itavipasua vile viriba, divai yenyewe itamwagika, na viriba vitaharibika. Lakini divai mpya sharti kutiwa katika viriba vipya.

Maombi

1. Ee Mungu naomba unigeuze niwe mtu tofauti anayeweza kuleta tofauti katika jamii inayohitaji msaada wa Mungu.

2. Ee Mungu naomba unigeuze kifikra ili niweze kuhakiki mapenzi yako na mpango wako kuhusu maisha yangu.

3. Ee Mungu nisaidie nisiwe na wokovu wa kuigiza usio na matokeo chanya bali niwe mtu aliyebadilishwa.

4. Ee Mungu naomba unifanye kiriba kipya ili maono mapya unayonipa yasinipe madhara bali yanipe hatua nyingine.

Unaweza kujiunga na makundi yetu ya maombi Facebook ili upate miongozo mbalimbali kuhusu maombi na maombezi.

Dr. Lawi Mshana, +255712924234, Tanzania