Ticker

6/recent/ticker-posts

Unajua sifa na tabia za watumishi ambao Mungu anawatumia kusaidia walioathirika kiuchumi?


 Unajua sifa na tabia za watumishi ambao Mungu anawatumia kusaidia walioathirika kiuchumi?

Usiku wa kuamkia jana niliona watumishi ambao walikuwa wamejishusha na kuishi maisha ya kawaida wakitumiwa na Mungu kusaidia wengi wenye uhitaji kimaisha.

Angalizo:

Tuko katika kipindi ambacho watumishi wengi wa uongo wanacheza na akili za watu na kutumia umasikini wao kujitajirisha. Waumini wengi wako foleni wakisubiri ahadi ambazo hazitimii kwa sababu wamewaendea watumishi ambao wana maagano na shetani. Kwa tafsiri nyingine wamewaendea watu ambao ni ‘kopela’ hivyo wanafilisika zaidi. Hata hivyo tunatakiwa kuwatambua watumishi wenye sifa za kibiblia. Watumishi hawa wako tayari kuishi maisha ya kawaida ili wawaokoe wengine katika moto kwa kutumia kanuni za Biblia Takatifu.

Tabia za watumishi wa kweli wanaoweza kuinua maisha ya watu wanaowahudumia:

1. Hawapendi kutumikiwa bali kutumikia

Hawatafuti kutetemekewa, kusujudiwa, kupigiwa magoti wala kuitwa majina yanayochukua nafasi ya Bwana Yesu. Wana tabia ileile ya Bwana wao wanayemtumikia yaani, YESU KRISTO – ambaye hakupenda kujionyesha kwamba ametoka mbinguni na alipenda kuwatumikia wanadamu. Fil 2:4-7 “Kila mtu asiangalie mambo yake mwenyewe, bali kila mtu aangalie mambo ya wengine. Iweni na nia iyo hiyo ndani yenu ambayo ilikuwamo pia ndani ya Kristo Yesu;  ambaye yeye mwanzo alikuwa yuna namna ya Mungu, naye hakuona kule kuwa sawa na Mungu kuwa ni kitu cha kushikamana nacho; bali alijifanya kuwa hana utukufu, akatwaa namna ya mtumwa, akawa ana mfano wa wanadamu.”

Mathayo 20:28 “kama vile Mwana wa Adamu asivyokuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.”

Badala ya Bwana Yesu kuwaagiza wanafunzi wake wamtawadhe miguu, Yeye ndiye aliwatawadha. Hii ni roho ya kutumikia (servant spirit). Yn 13:4-8 “aliondoka chakulani; akaweka kando mavazi yake, akatwaa kitambaa, akajifunga kiunoni. Kisha akatia maji katika bakuli, akaanza kuwatawadha wanafunzi miguu, na kuifuta kwa kile kitambaa alichojifunga. Hivyo yuaja kwa Simoni Petro. Huyo akamwambia, Bwana! Wewe wanitawadha miguu mimi? Yesu akajibu, akamwambia, Nifanyalo wewe hujui sasa; lakini utalifahamu baadaye. Petro akamwambia, Wewe hutanitawadha miguu kamwe. Yesu akamwambia, Kama nisipokutawadha, huna shirika nami.”

2. Hawachanganyi wito na mali

Kuna Mungu wa mbinguni na mungu-mali (mammon). Mtumishi anaweza kuwa msomi wa Theolojia na kumtaja Mungu kwa maneno lakini moyoni mwake ametanguliza mungu-pesa. Huyu Mungu-pesa katika Biblia anaitwa ‘mammon.’ Huyu mungu-pesa anamfanya mtumishi athamini wale tu wenye pesa, ajilimbikizie mali bila kujali anaowaongoza, apime mafanikio ya huduma yake kwa kumiliki pesa na mali badala ya utendaji wa Roho Mtakatifu (dalili za Roho na nguvu).  Huyu mungu-pesa ndiye anasababisha baadhi ya watumishi kutoza watu walipie huduma ambazo Bwana alizitoa bure.

Luka 16:13 “Hakuna mtumishi awezaye kutumikia mabwana wawili; kwa maana, ama atamchukia huyu na kumpenda huyu, ama atashikamana na huyu na kumdharau huyu. Hamwezi kumtumikia Mungu na mali.”

3. Hawana tabia ya kupenda fedha

Hawatafuti kuitwa matajiri bali kutimiza mahitaji katika kiwango walichopangiwa na Mungu. Wanajua kiwango cha maisha walichokusudiwa na Mungu na hawatafuti njia za mkato katika kufanikiwa.

Waebrania 13:5 “Msiwe na tabia ya kupenda fedha; mwe radhi na vitu mlivyo navyo; kwa kuwa yeye mwenyewe amesema, Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa.”

Ukitafuta kuwa tajiri kwa haraka bila uaminifu utaadhibiwa na Mungu. Mithali 28:20 “Mtu mwaminifu atakuwa na baraka tele; Lakini afanyaye haraka kuwa tajiri hakosi ataadhibiwa.”

4. Hawatumainii utajiri wa dunia bali Mungu

Shauku yake ni kuona Mungu anainuliwa na watu wanakutana na Mungu. Baraka anazopata anazitumia kwa utukufu wa Mungu na sio kwa kujinufaisha mwenyewe. Utajiri wake unatoka kwa Mungu na sio katika maagano ya kishetani yenye masharti yanayowagharimu wafuasi wake. Waumini wanaojiunganisha na watumishi wa kishetani wanatolewa kafara au kuingizwa (kuwa initiated) katika maagano yanayowatesa hata wanapotoka katika imani hizo. Wakifunguka macho na kuamua kuachana na imani hizo potofu wanatakiwa kuombewa na watumishi wa kweli wenye mamlaka katika kuvunja hayo magano ya kishetani. Vinginevyo wataishi maisha magumu sana kwa vile walikula kiapo kwa hiari yao wenyewe.

1 Timotheo 6:17 “Walio matajiri wa ulimwengu wa sasa uwaagize wasijivune, wala wasiutumainie utajiri usio yakini, bali wamtumaini Mungu atupaye vitu vyote kwa wingi ili tuvitumie kwa furaha.”

Shuhuda za watumishi wa kweli zinahusu ukuu wa Mungu na sio mali wanazomiliki hapa duniani. Zaburi 20:7 “Hawa wanataja magari na hawa farasi, Bali sisi tutalitaja jina la Bwana, Mungu wetu.”

5. Shauku yao ni kutajirisha wengi na sio kujitajirisha wao wenyewe

Hawawezi kufurahia kujilimbikizia mali na kujionyesha kwa watu wakati waumini wao wanaomcha Mungu wamechoka kimaisha, ni tegemezi, ombaomba na wanalala njaa. Wanakuwa na juhudi za kuwasaidia waumini na jamii ijue mbinu za kupata upenyo wa kimaisha na sio kuhamasisha utoaji peke yake. 2 Wakorintho 6:10 “kama wenye huzuni, bali siku zote tu wenye furaha; kama maskini, bali tukitajirisha wengi; kama wasio na kitu, bali tu wenye vitu vyote.”

Kuna waumini wamefikia hatua ya kuchenji pesa ili wamudu kutoa sadaka nyingi ambazo zinatolewa kila siku ya ibada na mara nyingi hakuna uwajibikaji wala mrejesho wa wazi wa matumizi yake. Mungu ametuagiza kumtolea lakini hapendi waumini wapangiwe kiasi cha kutoa. 2 Wakorintho 9:7 “Kila mtu na atende kama alivyokusudia moyoni mwake, si kwa huzuni, wala si kwa lazima; maana Mungu humpenda yeye atoaye kwa moyo wa ukunjufu.” Tuwe wabunifu wa njia zingine za kupata kipato kwa vile Neno la Mungu limetuagiza pia kufanya kazi kwa bidii. Asiyefanya kazi hatakiwi kula chakula. Ndiyo maana wengine tunashona hema kama mtume Paulo ili tusiwalemee waumini wetu wala kuweka tozo katika huduma tulizopewa bure. 1 Wathesalonike 2:9 “Maana, ndugu, mnakumbuka taabu yetu na masumbufu yetu; kwa kuwa mchana na usiku tulifanya kazi tusije tukamlemea mtu wa kwenu awaye yote, tukawahubiri hivi Injili ya Mungu.” 2 Wathesalonike 3:10 “Kwa kuwa hata wakati ule tulipokuwapo kwenu tuliwaagiza neno hili, kwamba ikiwa mtu hataki kufanya kazi, basi, asile chakula.”

MAONO YA USIKU WA KUAMKIA LEO

1. Nimeona waumini wanaomba wakiwa katika ukame wa kiroho bila bubujiko na mhubiri ameishiwa maneno kiasi kwamba mahubiri yake hayana mvuto. (Nimemuomba Mungu akuhuishe wewe ambaye umeibiwa bubujiko la Roho ili usitumike kwa kujilazimisha).

2. Nimeona wanafunzi watano wanarubuniwa kufanya mapenzi shuleni. (Hii ni roho inayoharibu watoto wetu mashuleni. Tukemee na kubomoa madhabahu za uasherati mashuleni badala ya kulalamika na kulaumu tu. Wanaofanya vitendo hivi wengine wamepagawa na mapepo hayo na wanajuta kwa kufanya vitendo hivyo lakini wanashindwa kuacha.)

Maombi ya wiki hii:

1. Ee Mungu naomba unipe macho ya kuwatambua watumishi wa kweli ili nisije nikatolewa kafara.

2. Ee Mungu naomba uniwezeshe kukuabudu Wewe peke yako badala ya kukuchanganya na mungu-pesa (mammon).

3. Ee Mungu naomba unipe uwezo wa kuwatajirisha wengi badala ya kutawaliwa na ubinafsi na uchoyo.

4. Ee Mungu naomba unipe bubujiko la Roho wako ili nisijilazimishe kukutumikia bali nitumike kwa shangwe na furaha ya moyo.

5. Tumia mamlaka ya Jina la Yesu kuharibu maagano na madhabahu za shetani zinazotesa wanafunzi. Shetani anajua ni rahisi kuwaharibu wanafunzi kwa vile wametoka mikononi mwa wazazi ambao ndio walimu wakuu wa malezi.

Kumbuka ku-follow kurasa zetu na kujiunga na makundi yetu ili uendelee kupata mafundisho ya kukua katika neema ya Mungu na kushinda changamoto za maisha.

Dr. Lawi Mshana, 0712-924234, Tanzania