Ticker

6/recent/ticker-posts

FANYIA KAZI MAZINGIRA YAKO HATARISHI, USISUBIRI UANGUKE! (ifahamu roho ya 'fantasia')


 FANYIA KAZI MAZINGIRA YAKO HATARISHI, USISUBIRI UANGUKE!

NB: Soma mpaka mwisho uijue roho ya ‘fantasia’ inavyotenda kazi leo.

Juzi Ijumaa: Nimeona mtu yuko katika uhatarishi ambao akiendelea kuupuuza atapata madhara makubwa

Jana Jumamosi: Nimeona watumishi wanaoombea watu na kuwashika shika sehemu za mwili isivyofaa, wakichukuliwa hatua za kiroho na kisheria.

Utangulizi

Bwana Yesu aliwahi kutoa mfano kuhusu mjenzi mwenye busara na mpumbavu na namna ambavyo nyumba ya yule mpumbavu ilianguka vibaya. Sababu kuu ilikuwa ni msingi mbovu ambao haukuweza kustahimili mafuriko na upepo mkali. Mt 7:27 “mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, ikaanguka; nalo anguko lake likawa kubwa.” Usipuuze mazingira ya huduma, kazi, biashara, marafiki, majirani, ndoa nk. Yana mchango mkubwa katika mafanikio yako au anguko lako.

Kwa namna gani uko katika mazingira hatarishi?

1. Una kiburi hivyo hutaki kujifunza kwa wengine

Mithali 16:25 “Iko njia ionekanayo kuwa sawa machoni pa mtu; Lakini mwisho wake ni njia za mauti.”

Kujiamini ni jambo jema sana lakini uwe makini usijiamini kupata kiasi. Wengi waliosema sio rahisi kuanguka walianguka kwa vile walitegemea nguvu zao wenyewe. Usipende kujiona kwamba unajua kila kitu/kuwa mjuaji (know-it-all) – tunategemeana. Biblia inasema hakuna mtu anaanguka bila kutanguliwa na roho ya kiburi. Mithali 16:18 “Kiburi hutangulia uangamivu; Na roho yenye kutakabari hutangulia maanguko.” Ukimuuliza kila mtu aliyeanguka iwe kiroho, kimaisha, kihuduma nk atakuambia kwamba kuna mahali hakutii jambo fulani kv ushauri, sauti ya moyoni nk. Kuna wakati unakatazwa kumkopesha mtu au kufanya kazi na mtu fulani halafu wewe unapuuzia sauti hiyo. Halafu unagundua kosa lako baadaye. 1 Wakorintho 10:12 “Kwa hiyo anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.”

2. Unakaa karibu na dhambi iliyowahi kukutesa sana

Waebrania 12:1 “Basi na sisi pia, kwa kuwa tunazungukwa na wingu kubwa la mashahidi namna hii, na tuweke kando kila mzigo mzito, na dhambi ile ituzingayo kwa upesi; na tupige mbio kwa saburi katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu.”

Fahamu vizuri tabia za aina ya watu unaoshirikiana nao. Kama hufanani nao itakuwa umekubali kuathiriwa na tabia zao. Mara nyingi shetani anapenda kuleta vishawishi vinavyoendana na aina ya dhambi uliyowahi kufanya. Anazo kumbukumbu za maisha yako. Anapojua kwamba kwa umri huo kuanza upya kukushawishi uvute sigara inaweza kuchukua muda, anafuatilia maeneo ambayo una udhaifu na kuelekeza nguvu zake zote hapo. Hivyo epuka maeneo ambayo ni rahisi zaidi kushawishika. Kumbuka miili yetu haiokoki bali inatiishwa na kusulubiwa.  Wagalatia 5:24 “Na hao walio wa Kristo Yesu wameusulibisha mwili pamoja na mawazo yake mabaya na tamaa zake.”

3. Hupigani vita vya kiroho – unakiri ushindi bila kupigana vita

Waefeso 6:13 “Kwa sababu hiyo twaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kushindana siku ya uovu, na mkiisha kuyatimiza yote, kusimama.”

Katika hivi vita vya kiroho lazima tuzingatie mambo kadhaa. La kwanza, lazima tuvae SILAHA ZOTE ZA MUNGU (sio baadhi). La pili, lazima tushindane au tupambane (kumiliki bunduki bila kuitumia au kujua kuitumia ni hatari sana), La tatu, lazima tuwe macho muda wote kwa vile shetani hafi (tusiwe na maombi ya msimu). Moja ya silaha ambayo hatuitumii sana ni KUOMBA KATIKA ROHO MTAKATIFU. Maombi yetu mengi ni ya akili hivyo hatugundui adui ni yupi, yuko upande gani, anatumia silaha gani na sisi wenyewe tuna nguvu kiasi gani. Matokeo yake tunaaibika bila kutegemea. Yuda 1:20 “Bali ninyi, wapenzi, mkijijenga juu ya imani yenu iliyo takatifu sana, na kuomba katika Roho Mtakatifu.”

Hivyo lazima tujue chanzo cha vita kabla ya kuanza kupigana. Yakobo 4:1 “Vita vyatoka wapi, na mapigano yaliyoko kati yenu yatoka wapi? Si humu, katika tamaa zenu zifanyazo vita katika viungo vyenu?”

4. Hutaki kupima roho uliyo nayo

1 Yohana 4:1 “Wapenzi, msiiamini kila roho, bali zijaribuni hizo roho, kwamba zimetokana na Mungu; kwa sababu manabii wa uongo wengi wametokea duniani.”

Unaweza kumpenda Mungu na kupenda kumtumikia na wakati huohuo una roho nyingine inayotenda kazi ndani yako. Utaijua kwa kupima hisia zako, nia yako na kama unakosa amani moyoni. 2 Kor 10:4,5 “(maana silaha za vita vyetu si za mwili, bali zina uwezo katika Mungu hata kuangusha ngome;) tukiangusha mawazo na kila kitu kilichoinuka, kijiinuacho juu ya elimu ya Mungu; na tukiteka nyara kila fikira ipate kumtii Kristo.

Tumepewa silaha zenye uwezo wa kuangusha ngome za shetani ambazo ni “MAWAZO NA FIKRA POTOFU.”

Napenda ujue kidogo shetani anavyotumia ya roho ya fantasia ndani na nje ya kanisa:

1. Kuamsha hisia za mapenzi kwa mtu ambaye sio mwenzi wako. Mf kumpapasa, kumkonyeza nk

2. Kuvaa nguo ambazo unalenga kuwatamanisha watu tofauti na mwenzi wako-unawakosesha na kuzini nao katika ulimwengu wa roho. Unakaribisha kuolewa na majini na kisha kuota ndoto za mahaba.

3. Kufurahia na kutojizuia kuangalia watu ambao wako uchi au nusu uchi kv kuwachungulia wakiwa nyumba za kulala wageni, wakiwa wanaoga, kuwatazama kwenye TV, simu nk

4. Kumfikiria kimapenzi mtu ambaye sio mwenzi wako wa maisha. Hata kama hajui, shetani anajua kwamba unazini naye kwa mawazo na anakusubiria tu ufe ili ukateseke milele.

5. Kutumia vitu vya kusisimua na kuamsha hisia za ngono. Mfano siku hizi kuna ongezeko la midoli ya kike iliyovalishwa nguo za ndani, wengine hawajui shampeni inatoa ujumbe wa matusi inapofunguliwa. Wanachoangalia ni kama ni pombe au la. Shetani amejipanga kufanya kazi kwa hila. Mungu atupe macho ya kiroho. 2 Wakorintho 11:3 “Lakini nachelea; kama yule nyoka alivyomdanganya Hawa kwa hila yake, asije akawaharibu fikira zenu, mkauacha unyofu na usafi kwa Kristo.”

Wiki chache zilizopita niliona perfume kwenye duka moja imeandikwa ‘fantasy’. Juzi tena nikakutana na mtu amevaa fulana ambayo kifuani imeandikwa ‘fantasia’. Fantasia ni kuwaza mambo ambayo hayawezi kutokea na mara nyingi mtu anakuwa mtumwa wa mawazo ya ngono nje ya mwenzi wake wa ndoa. Maneno kama haya yanapokuwa yameandikwa kwenye nguo zako za ndani au perfume, usitegemee kushinda utumwa wa ngono. Hata kama hutaki, utajikuta unafuatiliwa mpaka utakubali vishawishi na kama uko katika ndoa utavutiwa na wengine kuliko mwenzi wako wa maisha. Pengine unaweza kujipa moyo kwamba unamuwaza mwenzi wako tu. Mungu hakukusudia wanandoa waishi kwa kuwaziana kwa tamaa mbaya (lustful desire/fantasize) bali kwa kupendana (love). Fantasia ni dhana isiyo halisi inayoweza kuweka matarajio yasiyofikika na kusababisha majuto na kumlinganisha mwenzi wako na wengine. Lakini upendo ni kitu halisi kinachokuwezesha kumpenda na kumkubali mtu kama alivyoumbwa na Mungu.

Maombi ya wiki hii:

1. Ee Mungu naomba uondoe roho ya kiburi na kunipa roho ya unyenyekevu ili nipokee neema yako na msaada wako.

2. Ee Mungu naomba unipe uwezo wa kutambua na kuepuka mazingira hatarishi na watu hatarishi kwa maisha yangu.

3. Ee Mungu naomba unifundishe jinsi ya kupigana vita vizuri vya kiroho ili nisishindwe na kuaibika.

4. Ee Mungu naomba unipe ushindi dhidi ya roho ya ‘fantasia’ ili nisije nikapoteza roho yangu milele. Marko 9:47 “Na jicho lako likikukosesha, ling'oe, ulitupe; ni afadhali kuingia katika ufalme wa Mungu, una chongo, kuliko kuwa na macho mawili, na kutupwa katika jehanum”

Kumbuka ku-follow kurasa zetu na kujiunga na makundi yetu ili uendelee kupata mafundisho ya kukua katika neema ya Mungu na kushinda changamoto za maisha.

Lawi Mshana, 0712-924234 (ushauri na maombezi kwa simu au whatsap)