UNAJUA MAUMIVU WANAYOPITIA BAADHI YA VIONGOZI WA IMANI? UNAJUA MADHARA YAKE KWAKO? (Sura ya 1)
Mwezi Novemba na Desemba 2024 nitautumia katika kuzungumzia kwa muhtasari ujumbe ambao Mungu alinipa mwaka 2011 na kunielekeza kuandika kitabu wakati huo kinachoitwa KILIO CHA WACHUNGAJI.
Kitabu hicho kina sura zifuatazo:
Sura ya 1: Aina za Maumivu ya Wachungaji
Sura ya 2: Sababu Kuu za Maumivu ya Wachungaji
Sura ya 3: Kuwanusuru Wachungaji kutoka Katika Maumivu
Sura ya 4: Maombi kwa Ajili ya Mchungaji na Familia yake
Sura ya 5: Matendo ya Kumtia Moyo Mchungaji na Familia yake
Sura ya 6: Maswali kwa Ajili ya Mchungaji Kujihoji Kibinafsi
Pengine unajisemea moyoni kwamba ujumbe huu haukuhusu kwa vile wewe sio kiongozi wa imani. Napenda ujue kwamba mtumishi wa Mungu akihuzunika kwa sababu yako unakaribisha laana katika maisha yako. Waebrania 13:17 “Watiini wenye kuwaongoza, na kuwanyenyekea; maana wao wanakesha kwa ajili ya roho zenu, kama watu watakaotoa hesabu, ili kwamba wafanye hivyo kwa furaha wala si kwa kuugua; maana isingewafaa ninyi.”
Ni ukweli usiopingika kwamba wakosoaji wakuu na wanaonyoshea kidole madhaifu ya viongozi wao wa imani HAWAJAWAHI KUWAOMBEA WALA KUTAFUTA NJIA YOYOTE YA KUWASAIDIA. Wakati wote wanawachukulia kwamba wanawakosea kwa makusudi.
Unajua kama mnazungumzia udhaifu wa mchungaji wenu halafu baada ya hapo mkamuombea, mkamshauri au kumtahadharisha, hamjakosea? Mnakosea pale mnapozungumzia udhaifu wake halafu baada ya hapo mnatawanyika bila mkakati wowote wa kumuombea wala kumsaidia. Najua sio viongozi wote wako tayari kushauriwa au kutahadharishwa lakini wewe timiza wajibu wako ila hakikisha unaongea nao kwa hekima. Wakolosai 4:6 “Maneno yenu yawe na neema siku zote, yakikolea munyu, mpate kujua jinsi iwapasavyo kumjibu kila mtu.” Mithali 12:15 “Njia ya mpumbavu imenyoka machoni pake mwenyewe; Bali yeye aliye na hekima husikiliza shauri.”
Nitaeleza sura za kitabu hatua kwa hatua kwa kifupi. Lakini unaweza kusoma kwa kina zaidi kupitia kwenye tovuti yangu (www.lawimshana.com).
Sura ya Kwanza (kwa muhtasari)
Aina za Maumivu ya Wachungaji
Kukosa walezi wa kiroho na kihuduma, kukosa usalama wa maisha ya familia zao, upweke na uchovu, kushindwa kufikia matarajio, na kusalitiwa
1.
Kukosa walezi wa kiroho na kihuduma
·
Wapo
wachungaji wengi ambao wana viongozi wanaowasimamia lakini hawana baba wa
kuwalea na kuwashauri. Mtu anaweza kuwa kiongozi wako na asiwe mlezi wako.
·
Wachungaji
wengi hawana mtu wanayeweza kumwonyesha hisia zao za kuchoka na kukata tamaa.
Hivyo wana maumivu mengi yaliyovia ndani ambayo yanawafanya wawe na uchungu
mioyoni na kukosa maneno yanayobariki. Dalili hizi zinajidhihirisha katika
mahubiri yao yasiyo na shukrani, yaliyojaa lawama na yenye matamshi ya kulaani
hasa pale uwajibikaji wa waumini wao unapopungua.
2.
Kukosa usalama wa maisha ya familia zao.
· Wachungaji
wengi wanamtumikia Mungu lakini hawana uhakika wa maisha ya baadae ya familia
zao hasa wakati wakichoka au wakipumzishwa na Bwana.
· Upo tu
utaratibu mzuri wa kanisa katika kumiliki mali kama vile majengo na viwanja. Ni
vyema pia mchungaji akaandaliwa kumiliki vitu vyake mwenyewe ili akimaliza muda
wake wa utumishi asitelekezwe, asiwe ombaomba wala asililemee kanisa bali aweze
kujitegemea.
· Kama
kweli mchango wa huduma ya mchungaji unathaminiwa, kanisa linapaswa kuwekeza
kwa ajili ya maisha ya baadaye ya mchungaji wao. Kanisa linaweza kumsaidia
katika ujenzi wa nyumba yake binafsi au kumuwekea fedha katika mfuko wa hifadhi
ya jamii wakati bado analitumikia kanisa. Ni aibu kwa kanisa kuwa na wachungaji
waliochoka na ombaomba baada ya kumaliza muda wao wa utumishi wa miaka mingi.
· Wakati
mwingine wahubiri wageni wanaotembelea kufanya semina na mikutano ya injili
ndio wanaonufaika na michango mikubwa kuliko wachungaji wenyeji kwa sababu
washirika hawatambui uzito wa huduma za wachungaji wao.
3.
Upweke na uchovu.
· Wachungaji
wengi wamelemewa na mizigo ya washirika wao inayozidi uwezo wao wa kuibeba.
Wakati huohuo wachungaji hawa, hawana watu waliowazunguka wanaoweza kuwatia
moyo. Ingawa wapo wazee wa Kanisa, baadhi yao hawaoni kwamba kumhudumia
mchungaji na nyumba yake ni kazi ya Mungu pia.
· Wachungaji
wanapokosa watu wa kuwainua katika maombi, wanachoka na kuzimia. Matokeo yake
waumini wa makanisa yao wanashindwa katika majaribu na kuanguka.
· Vilevile,
kuna wachungaji wanadhani kwamba ni dhambi kwa mtumishi wa Mungu kupumzika
akiwa bado duniani. Wanasahau kwamba kupumzika sio uvivu bali ni agizo la
Bwana. Tena sio mwanadamu peke yake anayetakiwa kupumzika bali hata mashamba.
· Unapofanya
huduma bila kujali kupumzika unakosa maono mapya, unamtumikia Mungu kwa mazoea,
unazoeleka mbele za watu kupita kiasi na unapungua katika ufanisi na ubora wa
huduma yako. Hata wanasayansi wamefanya majaribio wakagundua kwamba mnyama
anayetengewa muda wa kupumzika, anafanya kazi kwa ufanisi zaidi kuliko yule
ambaye hapewi muda wa kupumzika.
4.
Kushindwa kufikia matarajio.
· Mchungaji
anaumia moyoni anapoona kwamba pamoja na juhudi anazofanya hafikii matarajio
yake binafsi, ya kanisa analochunga na ya uongozi wa juu wa kanisa lake.
· Anaumia
zaidi anapokuwa ametumia muda mrefu kuandaa ujumbe wa Neno la Mungu halafu
anapofika ibadani anakuta watu wengi hawajafika tena bila taarifa yoyote.
Anajisikia kwamba huduma yake na taabu yake haitambuliwi wala haithaminiwi.
· Wakati
mwingine waumini wanafika ibadani wakiwa wamevaa nguo za thamani kubwa lakini
hawana Biblia, daftari wala kalamu. Wanaitikia mahubiri kwa kutikisa tu vichwa,
lakini hawaandiki chochote.
· Lakini
pia inaumiza mchungaji anapotarajiwa kutoa michango mingi katika ngazi za juu
za dhehebu lake wakati ameshindwa kutimiza mahitaji muhimu ya maisha kama vile
kulipa ada ya mtoto wake. Anavunjika moyo anapoona kwamba hakuna anayejali hata
kumuuliza tu kuhusu maendeleo ya familia yake. Wakati mwingine sio tu wasimamizi
wake wanaomsahau lakini pia hata washirika anaowachunga. Jambo hili linachangia
kuwafanya watoto wa wachungaji kuidharau kazi ya uchungaji.
· Mchungaji
anaposhindwa kutimizia mahitaji ya msingi ya familia yake, anavunjika moyo na
kupoteza heshima kwa familia yake. Mwenzi na watoto wake hawawezi kumuelewa
Mungu kupitia mahubiri ya kanisani ambayo hayaendani na hali halisi ya maisha
ya nyumbani. Tusiwalazimishe watoto kuingia katika wito ambao hawakuitiwa!
5.
Kusalitiwa
· Mchungaji
pia anaumia sana anapowekeza mambo mengi katika mioyo ya kondoo zake halafu
wengine wanamsaliti kwa kuamua kuhamia huduma nyingine bila sababu yoyote ya
msingi na bila kumuaga. Hata hivyo, pamoja na kuwa na sababu yoyote nzuri, mtu
hapaswi kuondoka vibaya kanisani kama anataka kubarikiwa huko aendako.
· Wakati
mwingine Mchungaji anaweza kumuandaa mshirika wake mmojawapo ili amsaidie
huduma halafu baadaye mshirika huyo anatumia ujuzi huohuo kumpindua au kummegea
kanisa. Mara nyingi adui za mtu ni watu wa nyumbani mwake mwenyewe.
· Sio
wakati wote kukimbiwa na washirika kunatokana na tatizo la kiongozi. Wakati
mwingine, washirika wenyewe hawako tayari kujifunza mafundisho yanayohitaji
kujikana nafsi. Tukiogopa kukimbiwa, tutachunga hata wajumbe wa shetani ambao
mwisho wake wataturarua sisi wenyewe.
· Wapo
wachungaji waliowapeleka vijana wao kusoma chuo cha Biblia na waliporudi
wakasahau walikotoka na kuanza kuwakejeli wachungaji wao na kupandikiza mbegu
mbaya kwa waumini wenzao.
· Wapo
pia wachungaji waliowapokea watumishi wageni na kuwapa nafasi kuhubiri katika
makanisa yao halafu baadaye watumishi hao wakamega kundi na kufungua kanisa
jirani nao.
· Hata
hivyo wachungaji tusifanye makosa katika kuchagua watu wa kuwaandaa kwa ajili
ya huduma. Tukumbuke kwamba chuo cha
Biblia hakimpi mtu huduma bali kinaweza kumsaidia mtu ambaye tayari amepewa
huduma na Bwana. Tunapaswa kuona huduma ya mtu kwanza kabla ya kutafuta
kumuendeleza ili tuweze kuchagua vizuri aina ya mafunzo yanayomfaa. Lakini pia
tusiangalie tu karama za roho na kusahau tunda la roho. Tujiulize kama mshirika
tunayetaka kumuendeleza kihuduma ana tabia inayofaa kuigwa.
Kipindi
kijacho utajifunza kuhusu SABABU KUU ZA MAUMIVU YA WACHUNGAJI
Angalia
mahali palipoandikwa Books (Vitabu), kisha bofya ‘Kilio cha Wachungaji,’ utaweza
kusoma utangulizi na sura hii kwa kina.


