Ticker

6/recent/ticker-posts

MASWALI GANI ANAPASWA MCHUNGAJI KUJIHOJI KIBINAFSI? (Sura ya 6)


 MASWALI GANI ANAPASWA MCHUNGAJI KUJIHOJI KIBINAFSI? (Sura ya 6)

Utangulizi

Hii ni sura ya mwisho ya kitabu cha Kilio cha Wachungaji

Unaweza kununua kitabu hiki kwa Tsh 5,000 (elfu tano tu) pamoja na gharama za kutuma. Pia unaweza kukinunua kwa Tsh 3,000 (elfu tatu tu) kikiwa katika mfumo wa Ebook/Epub ili ujisomee kwenye simu ambapo maandishi yake ni makubwa yasiyoumiza macho.

Sura ya Sita (kwa muhtasari)

Maswali kwa ajili ya Mchungaji Kujihoji Kibinafsi

Haya maswali yanamsaidia mchungaji kuwajibika ili kama kuna maeneo anapata mateso ambayo hayakuruhusiwa na Bwana, ayafanyie kazi.

1. Umekuwa ushuhuda kwa ukuu wa Kristo kwa maneno yako na matendo yako? Watu wanapokusikiliza na kutazama mwenendo na mtindo wa maisha yako wamuone Kristo ndani yako. Uwe barua yenye ujumbe wa Yesu hata pale unapokuwa huna Biblia mkononi (2 Kor 3:2,3).

2. Umepungukiwa uadilifu katika masuala ya kifedha au umetamani kitu chochote ambacho si cha kwako? Unatakiwa kuwa mwaminifu katika fedha za kanisa na uridhike na vitu ulivyo navyo. Usijilinganishe na watumishi wa Mungu wengine. Mungu ana mpango maalum kwa ajili ya kila mmoja wetu (1 Tim 6:6-8).

3. Umeheshimu na kuonyesha kujali katika mahusiano yako wiki hii? Usizame katika huduma na kusahau kuwa karibu na familia yako. Unatakiwa kujali familia yako kabla ya kanisa. Usipojali watu wa nyumbani mwako unakuwa mbaya kuliko watu wasioamini. Lakini pia usilione kanisa kama shirika au mradi fulani bali kama watu wanaohitaji uhusiano wa kindugu na kirafiki (1 Tim 5:8).

4. Umetawaliwa na mwenendo usiofaa (addictive behaviour) wiki hii iliyopita? Sio lazima mwenendo usiofaa uwe ulevi wa pombe au sigara tu. Unaposhindwa kufanya huduma kwa sababu ya kuangalia mpira au tamthiliya katika runinga (TV), unakuwa mlevi wa runinga. Uwe na kiasi katika kila jambo. Hata maombi ya muda mrefu ni mazuri kwa ajili ya upako lakini usisahau kupatana na mkeo au mumeo kabla ya kufanya hivyo kwa ajili ya usalama wa familia (1 Kor 7:5).

5. Mtu alikuumiza? Ulimsamehe? Umeendelea kutunza hasira dhidi ya mtu fulani? Pengine unaendelea na huduma wakati kuna mtu husalimiani naye na hakuna juhudi zozote unazochukua. Biblia inasema ukiwa na neno na mtu acha kutoa sadaka ukapatane naye kwanza ndipo uje kuitoa. Jua lisichwe uchungu haujakutoka kama kweli unajua kwamba Bwana anaweza kuja kutuchukua wakati wowote. Efe 4:26,27

6. Umemtakia mabaya mtu yeyote kwa siri? Pengine kuna mtu unatamani ungesikia amekufa au unamuombea afe. Kama unaamini Mungu anaweza kuua, amini pia anaweza kubadilisha na kuhuisha. Watu wengi wanaotukwaza hawafanyi hivyo kwa kukusudia bali wana roho chafu ndani yao. Ungana na Bwana Yesu kwa kusema, ’Baba, wasamehe kwa kuwa hawajui watendalo’.

7. Umeruhusu kutawaliwa na mawazo mabaya kuhusu mtu fulani wiki hii?  Pengine kuna mtu ambaye si mwenzi wako halali lakini anakutesa sana katika moyo wako. Umeshindwa kumng’oa moyoni mwako. Yesu aliyesema, Njoni kwangu ninyi nyote msumbukao na kulemewa na mizigo nami nitawapumzisha, anaweza kutua mzigo wako. Wakati mwingine unawawazia vibaya watu fulani kwamba wametenda dhambi wakati huna ushahidi wowote. Usisahau kwamba ingawa unatumika, hii kazi ina mwenyewe. Mwachie Mungu mwenyewe ahukumu watu wake aliowaumba.

8. Umefanya maombi, umesoma neno na kumsikia Mungu kama inavyotakiwa wiki hii? Mara nyingi unaomba na kusoma Neno wakati tu unapoandaa ujumbe badala ya kujilisha Neno ili liwe sehemu ya maisha yako kwanza kabla ya kulipeleka kwa wengine. Wakati mwingine unajisikia moyoni kwamba ni neema tu ya Mungu inayokuwezesha kusimama madhabahuni kuhubiri kwa vile huna muda kabisa wa kuomba na kusoma Neno. Unahitaji kumsikia Mungu kila wakati ili uwe na ujumbe sahihi wa kuwaambia watu wake.

9. Umekuwa mwaminifu kabisa kwa Mungu? Unajua njia zako kwamba ungekuwa hatarini kiasi gani na kupoteza heshima yako  kama watu wangejua mambo unayoyafanya kwa siri. Unasahau kwamba Mungu anakuona. Na baya zaidi unapenda sana kuwanyoshea kidole wengine na kusahau madhaifu yako lukuki. Epuka kufanya jambo lolote ambalo ungejisikia hatia kama ungeambiwa uombe kwanza kabla ya kulifanya.

Pamoja na haya yote, usijisikie kukata tamaa bali utambue kwamba Mungu anatazama nia yako na anataka kukusaidia ili usije ukahubiri wengine halafu mwishowe wewe mwenyewe ukawa mtu wa kukataliwa (1 Kor 9:27).

Bei ya kitabu katika mfumo wa karatasi ni Tsh 5,000 na mfumo wa mtando (ebook) ni Tsh 3,000.

Soma muhtasari wa sura zote kupitia www.lawimshana.com. Tafuta sehemu iliyoandikwa ’search’ halafu andika WACHUNGAJI na kutafuta. Utaona makala zote.

Dr. Lawi Mshana, Freelance Facilitator & Public Speaker, +255712-924234, Korogwe, Tanga, Tanzania