Ticker

6/recent/ticker-posts

Unahitaji kufichwa chini ya mbawa za Bwana

UNAHITAJI KUFICHWA CHINI YA MBAWA ZA BWANA

Maono: Nimeona watu wanapita katika mazingira hatarishi sana na wanahitaji Mungu awafiche ili wasipate madhara

Kuna wakati unagundua kwamba pamoja na juhudi zako katika mambo mengi umepungukiwa na ulinzi wa Mungu. Tunahitaji ulinzi katika maeneo yote ya maisha yetu – nyumbani, safarini, kazini, miradini, katika huduma nk Zaburi 121:8 “Bwana atakulinda utokapo na uingiapo, Tangu sasa na hata milele.”

SASA TUFANYEJE?

1. Tujifunze kukaa chini ya mbawa za Bwana 

Zaburi 91:1-4 “1 Aketiye mahali pa siri pake Aliye juu Atakaa katika uvuli wake Mwenyezi. 2 Nitasema, Bwana ndiye kimbilio langu na ngome yangu, Mungu wangu nitakayemtumaini. 3 Maana Yeye atakuokoa na mtego wa mwindaji, Na katika tauni iharibuyo. 4 Kwa manyoya yake atakufunika, Chini ya mbawa zake utapata kimbilio; Uaminifu wake ni ngao na kigao.” 

Wakati mwingine ingawa tunalitaja jina la Bwana tukiimba, tukisifu na tukiomba, hatumtumaini kama tunavyowatumainia wanadamu au kazi zetu. Wakati mwingine tunapokuwa na uhitaji tunamuomba Mungu lakini kichwani tunawaza kwenda kumuomba mtu fulani atusaidie. Sio vibaya kuomba msaada wa mtu lakini tunapokuwa magotini katika MAOMBI mbele za Mungu tusahau kuwa OMBAOMBA. Kama Mungu anataka tukapate msaada kwa mtu fulani tusubiri aanzishe yeye lakini tusimuendee wakati tayari tumeshapanga majibu. Tujiandae na kumuacha apange yeye. Tuketi mahali pa siri pake Mwenyezi. Mithali 16:1 “Maandalio ya moyo ni ya mwanadamu; Bali jawabu la ulimi hutoka kwa Bwana.”

Kama vifaranga vinavyotulia chini ya mbawa za tai, Mungu wetu awe KIMBILIO – hakika hatutaaibika. Zaburi 37:19 “Hawataaibika wakati wa ubaya, Na siku za njaa watashiba.”

 2. Tujifunze kumtaja Bwana kuliko shida zetu na nguvu zetu

Zaburi 23:1,4 “Bwana ndiye mchungaji wangu, Sitapungukiwa na kitu. Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti, Sitaogopa mabaya; Kwa maana Wewe upo pamoja nami, Gongo lako na fimbo yako vyanifariji.”

Tunakwama kwa vile tunachanganyikiwa tunapopita katika magumu (bonde la uvuli wa mauti). Tutambue kwamba hakuna wakati Mungu anatuacha. Sisi ndio kuna wakati tunamuacha Mungu. Mruhusu Mungu awe Mchungaji wako (uwe kondoo na Yeye awe Mchungaji) ndipo utaona ukiwa salama kupitia ‘gongo lake na fimbo yake.’

Acha tabia ya kukiri kwa kinywa chako kwamba hutaweza, utafeli, hutafanikiwa nk. Shetani anapokusikia ukikiri kushindwa unampa nafasi ya kufanyia kazi maneno yako ili yawe halisi. Mithali 6:2 “Basi umetegwa kwa maneno ya kinywa chako, Umekamatwa kwa maneno ya kinywa chako.”

Lakini pia acha kutumainia nguvu zako mwenyewe, cheo chako, elimu yako, uzoefu wako au ujanja wako. Badala yake mtegemee Mungu akuwezeshe. Zekaria 4:6 “Akajibu akaniambia, akisema, Hili ndilo neno la Bwana kwa Zerubabeli, kusema, Si kwa uwezo, wala si kwa nguvu, bali ni kwa roho yangu, asema Bwana wa majeshi.” Wafilipi 4:13 “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.”

3. Tambua thamani yako kwa Mungu na hazina alizokuandalia

Zekaria 2:8 “Kwa maana Bwana wa majeshi asema hivi, Ili nitafute utukufu amenituma kwa mataifa wale waliowateka ninyi; maana yeye awagusaye ninyi aigusa mboni ya jicho lake.” Ikiwa mtu anayekugusa wewe anagusa mboni ya jicho la Mungu, Unadhani uko salama kiasi gani mikononi mwa Mungu? Hata kama mtu unamheshimu kiasi gani, unadhani utamfanya nini unapomuona analeta kidole chake kiguse mboni ya jicho lako? Bila shaka utamsukumia mbali bila kujali ana uhusiano gani na wewe! Zaburi 17:8 u7yhj“Unilinde kama mboni ya jicho, Unifiche chini ya uvuli wa mbawa zako.”

Mungu yuko tayari kukumulikia katika giza nene unalopitia. Isaya 9:2 “Watu wale waliokwenda katika giza Wameona nuru kuu; Wale waliokaa katika nchi ya uvuli wa mauti, Nuru imewaangaza.” Lakini pia ziko baraka zako alizoficha kwa ajili yako. Isaya 45:3 “nami nitakupa hazina za gizani, na mali zilizofichwa za mahali pa siri, upate kujua ya kuwa mimi ni Bwana, nikuitaye kwa jina lako, naam, Mungu wa Israeli.” Ili uzijue baraka alizokuandalia SIRINI jifunze kuomba maombi ya kuingia chumba cha ndani na kujifungia – MUNGU AONAYE SIRINI ATAKUPA THAWABU AU MAJIBU YAKO. Mathayo 6:6 “Bali wewe usalipo, ingia katika chumba chako cha ndani, na ukiisha kufunga mlango wako, usali mbele za Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi.”

USHUHUDA WANGU

Jambo la pekee linalonifanya niweke tumaini langu kwa Mungu kuliko mwanadamu yeyote ni mambo haya matatu: 1. MUNGU HAFI 2. MUNGU HABADILI NIA YAKE 3. MUNGU HAFILISIKI. Mojawapo katika haya matatu linaweza kumpata mtu yeyote unayemtegemea na kujikuta pabaya. Kama hatakufa kabla ya kukufanyia alilokuahidi, anaweza kubadilisha nia yake ya kukusaidia kwa sababu ya vipaumbele vyake au changamoto fulani. Asipobadili nia yake, anaweza kutikisika kiuchumi na kujikuta anashindwa kufanya aliyokuahidi.

MAOMBI

1. Ee Mungu naomba unifundishe kukaa chini ya mbawa zako ili nisiogope hata uchumi wa dunia na wa familia unapotikisika.

2. Ee Mungu naomba uniondolee tabia ya kutaja changamoto zangu na nguvu zangu kuliko UWEZO wako. Nitambue kwamba Wewe ndiwe chanzo cha mafanikio na ushindi wangu wakati wote.

3. Ee Mungu naomba uwe JUU YA YOTE KATIKA YOTE NA NDANI YA YOTE (Efe 4:6) maishani mwangu; Wewe uzidi na mimi nipungue kama alivyoomba Yohana Mbatizaji (Yn 3:30).

NAKUOMBEA WIKI HII UFUNIKWE NA MBAWA ZA BWANA KATIKA MAISHA YAKO!

Lawi Mshana, +255712924234, Tanzania