Ticker

6/recent/ticker-posts

Kwanini Wakristo wanaoa ilhali Yesu Kristo hakuoa?


 KWANINI WAKRISTO WANAOA ILHALI YESU KRISTO HAKUOA?

Hivi karibuni mke wangu aliulizwa swali hili wakati akishuhudia kuhusu wokovu ulioletwa na Yesu Kristo. Hivyo akaniomba nimpatie ufafanuzi zaidi. Nimeona umuhimu wa kuandika jibu la swali hili kwa kirefu kwa kutumia Maandiko Matakatifu (Biblia).

Ili kulijibu vizuri swali hili lazima tujue tofauti ya kazi aliyopewa Adamu wa kwanza (Adamu wa Edeni ya duniani) na Adamu wa mwisho (Yesu wa Edeni ya mbinguni au Peponi/Paradiso). Adamu wote wawili wana sura ya Mungu. Mwanzo 1:26a “Mungu akasema, Na tumfanye mtu kwa mfano wetu, kwa sura yetu.” 2 Wakorintho 4:4 “ambao ndani yao mungu wa dunia hii amepofusha fikira zao wasioamini, isiwazukie nuru ya injili ya utukufu wake Kristo aliye sura yake Mungu.”

Kuwa na sura ya Mungu kunamaanisha kwamba mtu amepewa ‘utashi’. Uwezo huu wa kuhisi, kufikiri na kuamua tumepewa sisi wanadamu lakini malaika hawakupewa. Wana nguvu kuliko sisi lakini wanasubiri tu maelekezo na maagizo. Ndiyo maana mwanadamu anabuni na kugundua vitu vingi na anaweza kuchagua kumkataa na kumtukana Yesu leo na asifanywe chochote mpaka siku ya hukumu ndipo atashughulikiwa. Tumepewa uhuru wa kuchagua aina ya maisha tunayotaka na kuwa tayari kwa matokeo yake (consequence). Kum 30:19 “Nazishuhudiza mbingu na nchi juu yenu hivi leo, kuwa nimekuwekea mbele yako uzima na mauti, baraka na laana; basi chagua uzima, ili uwe hai, wewe na uzao wako.”

Tofauti ya Adamu wa kwanza na Adamu wa mwisho

1. 1 Wakorintho 15:45 “Ndivyo ilivyoandikwa, Mtu wa kwanza, Adamu, akawa nafsi iliyo hai; Adamu wa mwisho ni roho yenye kuhuisha.”

Andiko hili lina maana kwamba Adamu wa kwanza alikuja kama NAFSI ILIYO HAI (living being) yaani ‘kiumbe mwenye uhai’ wakati Adamu wa mwisho, yaani Yesu Kristo alikuja kama ROHO YENYE KUHUISHA (a life-giving spirit) yaani ‘roho anayetupatia uhai.’ Kwa lugha rahisi, Adamu wa kwanza ni MWILI WENYE ROHO wakati Adamu wa mwisho ni ROHO YENYE MWILI. Adamu wa kwanza ni mwili uliopuliziwa pumzi ya Mungu (Mwa 2:7) wakati Adamu wa mwisho ni Mungu aliyefanyika mwili (Yn 1:14).

2. Adamu wa kwanza aliumbwa aishi duniani maisha yake yote wakati Adamu wa mwisho alikuja duniani kwa muda maalum na kwa misheni maalumu. Maisha Yake ya milele yako mbinguni. Yesu hakuja duniani kuleta amani bali kumpokonya shetani watu anaowatesa na kuwapeleka mbinguni. Luka 12:51 “Je! Mwadhani ya kwamba nimekuja kuleta amani duniani? Nawaambia, La, sivyo, bali mafarakano.”  1 Yohana 3:8 “atendaye dhambi ni wa Ibilisi; kwa kuwa Ibilisi hutenda dhambi tangu mwanzo. Kwa kusudi hili Mwana wa Mungu alidhihirishwa, ili azivunje kazi za Ibilisi.” Kwa mujibu wa Biblia, sifa ya kwanza ya mpinga-Kristo ni mtu anayekataa kwamba Kristo ni Mungu aliyekuja duniani katika mwili (incarnation). 1 Yohana 4:2.3 “Katika hili mwamjua Roho wa Mungu; kila roho ikiriyo kwamba Yesu Kristo amekuja katika mwili yatokana na Mungu. Na kila roho isiyomkiri Yesu haitokani na Mungu. Na hii ndiyo roho ya mpinga Kristo ambayo mmesikia kwamba yaja; na sasa imekwisha kuwako duniani.”

3. Adamu wa kwanza alipewa kazi ya KUZAA NA KUONGEZEKA wakati Adamu wa mwisho alikuja KUMNUNULIA MUNGU WATU waliokuwa wameuzwa kwa shetani.

Mwanzo 1:28a “Mungu akawabarikia, Mungu akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha.” Ufu 5:9 “Nao waimba wimbo mpya wakisema, Wastahili wewe kukitwaa hicho kitabu na kuzifungua muhuri zake; kwa kuwa ulichinjwa, ukamnunulia Mungu kwa damu yako watu wa kila kabila na lugha na jamaa na taifa.” Usisahau pia kwamba Mungu aliagiza watu waongezeke kabla ya anguko la dhambi ya Adamu na Hawa na baada ya kuangamiza wenye dhambi kwa gharika kipindi cha Nuhu (Mwa 9:1). Moyo wa Mungu ni kutaka waongezeke wenye haki na sio wenye dhambi.

Kwa hiyo Bwana Yesu hakuja kuonyesha namna ya kuoa na kuzaa. Hiyo kazi ilikuwa ya Adamu wa kwanza na alishaifanya na bado inaendelea. Kazi iliyomleta Yesu duniani ni kumsaidia mwanadamu awe na sifa za kuingia mbinguni. Tambua kwamba mwanadamu hakuumbwa kwa ajili ya kwenda mbinguni wala kwenda Jehanum. Alikusudiwa kukaa duniani milele. Ndiyo maana ilibidi mambo kadhaa yafanyike baada ya anguko la dhambi:

1. Mwanadamu asamehewe dhambi na kuandaliwa kuwa na maisha matakatifu ya viwango vya mbinguni (yenye utukufu wa Mungu).

Warumi 3:23 “kwa sababu wote wamefanya dhambi, na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” Waefeso 5:27 “apate kujiletea Kanisa tukufu, lisilo na ila wala kunyanzi wala lo lote kama hayo; bali liwe takatifu lisilo na mawaa.” Hakuna kinyonge kitakachoingia mbinguni. Ufu 21:27 “Na ndani yake hakitaingia kamwe cho chote kilicho kinyonge, wala yeye afanyaye machukizo na uongo, bali wale walioandikwa katika kitabu cha uzima cha Mwana-Kondoo.”

Wengi watataka kuingia katika Ufalme wa Mungu lakini hawataweza kwa vile wanategemea matendo yao mazuri badala ya kuipokea neema ya Mungu kupitia Yesu Kristo. Luka 13:24 “Jitahidini kuingia katika mlango ulio mwembamba, kwa maana nawaambia ya kwamba wengi watataka kuingia, wasiweze.” Efe 2:8,9 “Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu.”

2. Makao yaandaliwe mbinguni kwa ajili ya wale walioamua kumuishia Mungu.

Yohana 14:2,3 “Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; kama sivyo, ningaliwaambia; maana naenda kuwaandalia mahali. Basi mimi nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi, nanyi mwepo.” Watakaoenda mbinguni hawatafanana. Itategemea uaminifu na utumishi wao ulivyokuwa wakiwa duniani. Watatofautiana kiwango cha utukufu. 1 Wakorintho 15:40, 41 “Tena kuna miili ya mbinguni, na miili ya duniani; lakini fahari yake ile ya mbinguni ni mbali, na fahari yake ile ya duniani ni mbali.  Kuna fahari moja ya jua, na fahari nyingine ya mwezi, na fahari nyingine ya nyota; maana iko tofauti ya fahari hata kati ya nyota na nyota.” Wengine watakuwa hawana fahari yoyote ingawa wako mbinguni kwa vile hawakumtumikia Mungu ingawa walimwamini Yesu na kumkataa shetani. 1 Wakorintho 3:15 “Kazi ya mtu ikiteketea, atapata hasara; ila yeye mwenyewe ataokolewa; lakini ni kama kwa moto.”

Mbinguni tutaishi kama malaika. Hakuna kuoa wala kuolewa. Bwana Yesu ametufundisha kwa MANENO na VITENDO kuhusu namna tutakavyoishi baada ya kuondoka katika dunia hii. Marko 12:25 “Kwa maana watakapofufuka katika wafu, hawaoi wala hawaolewi, bali huwa kama malaika walioko mbinguni.”

3. Mwanadamu aliyeamua kumfuata shetani atatupwa motoni pamoja naye (hata hivyo Jehanum haikutengenezwa kwa ajili ya mwanadamu).

Mathayo 25:41 “Kisha atawaambia na wale walioko mkono wake wa kushoto, Ondokeni kwangu, mliolaaniwa, mwende katika moto wa milele, aliowekewa tayari Ibilisi na malaika zake.”

Mungu ana sifa kuu mbili ambazo zinachanganya wengine – NI MWENYE UPENDO na MWENYE HAKI. Amempenda mwanadamu kiasi cha kumtoa mwanawe pekee Yesu Kristo ili kila amwaminiye asipotee. Lakini pia ni mwenye haki hivyo atamlipa kila mtu sawasawa na matendo yake. Hivyo kama unasema Mungu mwenye upendo hawezi kuwatupa wanadamu motoni, endelea kuchezea kipindi hiki cha upendo wake kwako. Kuna siku hutaipata nafasi hii tena. Yohana 3:16 “Kwa maana jinsi hii Mungu aliupenda ulimwengu, hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” Zaburi 9:8 “Naye atauhukumu ulimwengu kwa haki; Atawaamua watu kwa adili.” Swali jingine linaweza kujitokeza kwamba Mungu alimuoa nani mpaka akamzaa Mwanae. Mtu anaweza kuuliza swali hili kama tu amempa Mungu mipaka kwamba lazima mwanaume na mwanamke wajamiiane ndipo azae mtoto. Anasahau kwamba kuna wakati anasema maembe yamezaliwa wakati hawezi kutuonyesha mume wa muembe huo ni nani. Lakini pia anasahau kwamba Adamu na Hawa hawakuzaliwa bali waliumbwa na Mungu. Hivyo Mungu hangeshindwa kumzaa Mwanae bila mwanaume kuhusika.

UPENDO WA MUNGU unadhihirika kipindi hiki cha neema. Itakapofika siku ya hukumu hatakuwa tena MWOKOZI bali atakuwa HAKIMU. Hapo ndipo tutajua maana ya HAKI YA MUNGU.

MWISHO

Kama mtu anajua kuhusu hii fursa ya kwenda mbinguni, hawezi kuishi kama watu wa dunia hii. Ni kweli kwamba Mungu ameahidi kutubariki pia hapa duniani lakini maisha yetu ni mafupi sana hapa. Hivyo hatupaswi kutumia muda wetu wote na kujilimbikizia mali kiasi cha kusahau kuwekeza kwa ajili ya umilele wetu. Kila atakayeingia mbinguni, atakaa mahali panapoendana na uwekezaji wake kwa Mungu alioufanya akiwa duniani. Ingawa katika Agano la Kale Adamu wa kwanza aliagizwa kuoa, katika Agano Jipya tunaona Bwana Yesu akiitwa Bwana arusi na kanisa likiitwa bibi arusi. Ufu 19:7,8 “Na tufurahi, tukashangilie, tukampe utukufu wake; kwa kuwa arusi ya Mwana-Kondoo imekuja, na mkewe amejiweka tayari. Naye amepewa kuvikwa kitani nzuri, ing'arayo, safi; kwa maana kitani nzuri hiyo ni matendo ya haki ya watakatifu.” Pia tunaona mtume Paulo akisema amepewa KARAMA YA KUTOKUOA. Ndoa ina faida zake tukiwa hapa duniani lakini sio tiketi ya kwendea mbinguni. 1 Wakorintho 7:7,8 “Ila nipendalo ni kwamba watu wote wawe kama mimi nilivyo; walakini kila mtu ana karama yake mwenyewe itokayo kwa Mungu, huyu hivi, na huyu hivi. Lakini nawaambia wale wasiooa bado, na wajane, Ni heri wakae kama mimi nilivyo.”

Kazi ya kuleta ukombozi ilikuwa ya muhimu kwa Bwana Yesu na kwetu kiasi kwamba kipaumbele cha siku yake ya kuzaliwa hakikuwepo tangu katika kanisa la kwanza. Adamu wa kwanza na wa mwisho, wote walizaliwa. Lakini Adamu wa kwanza alianguka akatuuza kwa shetani na kuleta kifo. Adamu wa mwisho alishinda kifo akawahamisha watakatifu waliokuwa kuzimu (kuzimu ilikuwa na upande wa makao ya wenye dhambi na upande wa makao ya watakatifu) na kuwapeleka Paradiso, yaani Edeni ya mbinguni. Kumbuka Adamu wa kwanza alipotenda dhambi alifukuzwa asile matunda ya mti wa uzima katika Edeni ya duniani. Mwanzo 3:24 “Basi akamfukuza huyo mtu, akaweka Makerubi, upande wa mashariki wa bustani ya Edeni, na upanga wa moto uliogeuka huko na huko, kuilinda njia ya mti wa uzima.” Kupitia Yesu tunarejezwa tena Edeni. Ufu 2:7b “Yeye ashindaye, nitampa kula matunda ya mti wa uzima, ulio katika bustani ya Mungu.” 

Naamini kwa sehemu maelezo haya yamekupa mwanga kuhusu sababu za Bwana Yesu kutokuoa alipokuja duniani.

Sala ya toba

Omba sala hii kwa kumaanisha kama umetambua kwamba unamuhitaji Yesu awe Bwana na Mwokozi wako.

“Ee Mungu, naomba unisamehe dhambi zangu. Ulimtuma Mwanao mpendwa Yesu Kristo afe kwa ajili yangu msalabani. Nakubali kumpokea moyoni mwangu ili anipe maisha mapya. Naomba uandike Jina langu katika kitabu cha uzima na kunipa Roho wako Mtakatifu aniongoze na kunifundisha. Nashukuru kwa kuniokoa katika Jina la Yesu Kristo. Amina.”

Kama umeomba sala hii kwa imani, jitambulishe kwa wapendwa wanaokiri wokovu ili ujengwe kiroho na kusimama imara katika imani uliyoipokea.

Unaweza kuwasiliana nami kama una swali lolote kuhusu safari yako mpya ya imani.

Lawi Mshana, 0712-924234