Ticker

6/recent/ticker-posts

Unajua kwa nini watoto wanalawitiwa na kufundishwa tabia hizo?


 Unajua kwa nini watoto wanalawitiwa na kufundishwa tabia hizo?

Nawashukuru wazazi na walezi ambao waliwaruhusu watoto na vijana wao wenye miaka kati ya 10 na 24 kuja kwenye mafunzo ya kushinda vishawishi na uhatarishi. Tulifunza aina za stadi za maisha, sababu za vijana kujihusisha na ngono mapema, sababu za baadhi ya vijana kutojihusisha na ngono, ushoga na madhara yake, mbinu za kushinda changamoto za ngono, maneno yanayotumika kuwahadaa au kuwalaghai vijana wajihusishe na ngono na utunzaji wa sehemu za siri. Pia tuliangalia video kuhusu kushinda ukatili wa kijinsia na kufahamu afya ya hedhi.

Ziko sababu nyingi za watoto kunajisiwa na kulawitiwa. Napenda kukupa sababu chache kati ya hizo ili tusaidiane kuchukua tahadhari. Lakini pia tutambue kwamba tunapaswa kuripoti bila kujali aliyefanyiwa unyanyasaji ni mtoto wa kumzaa au la. Namba mojawapo ya bure ya kuripoti kuhusu masuala ya ukatili wa kijinsia ni namba 116.

Baadhi ya sababu za watoto kulawitiwa na kufundishwa tabia hizo ni:

1. Wazazi kuruhusu watoto wa kiume walale na wageni wasiowajua wakijifariji kwamba ni wanaume wenzao. Baadhi ya wageni hao ni ndugu wa karibu kama vile wajomba nk. Wageni hao wanajenga ukaribu na watoto hao na kuwatoa (kwenda nao ‘out’) na kuwapa zawadi. Wanawapa huduma ambazo ni nadra sana kwa wazazi/walezi kuwapatia watoto wao. Hali hii inawafanya watoto wawaamini na kuwapenda zaidi hao wageni na mwishowe wanatumbukia katika majanga.

2. Wazazi/walezi kutofuatilia kwamba watoto wakitembelea ndugu zao wakati wa likizo wanalala katika mazingira gani. Wanachojali tu ni kwamba mtoto amefika salama na kupokelewa. Kuna msichana alienda kufanya kazi za ndani mji fulani akashanga wanalala kitanda kimoja na (sio tu chumba kimoja) watoto wa kiume na wa kike kutokana na ufinyu wa vyumba vya kulala. Tujiulize nyumba ina vyumba vingapi na familia ina watu wangapi kabla ya kuwaruhusu watoto kwenda matembezi ya likizo kwa ndugu au marafiki wa familia.

3. Wazazi/walezi kuwa wakali sana kiasi kwamba mtoto hawezi kutoa maoni au kupinga wazo lolote. Mtoto anaweza kukataa akitumwa dukani usiku lakini mzazi hataki kumdodosa. Kumbe kuna watu wabaya anaokutana nao na kumnajisi na kisha wanamuonya asimwambie mtu. Mtoto anaposhindwa kupatiwa taulo za kike na wazazi wake, jamii itamsaidia lakini itadai sadaka ya shukrani kutoka kwake.

4. Watoto wa kiume mara nyingi ni wakimya kuliko wa kike. Hivyo wanapofanyiwa ukatili wanaweza kunyamaza bila kumwambia mtu yeyote. Wanaona aibu kusema na baada ya muda wakizoea mchezo huo wanajikuta wameupenda. Watoto hawa wameanza mtindo mashuleni wa kuomba wakajisaidie kumbe wanaenda kulawitiana vyooni. Na wakati huohuo mikakati mingi iliyopo ni ya kumlinda mtoto wa kike zaidi. Watoto wa jinsi zote sasa wako hatarini na inawezekana watoto wa kiume ndio wako hatarini zaidi.

5. Hata watoto wa kike wanalawitiwa kwa vile mhalifu anataka aepuke kumpa mimba. Anadhani kwa kufanya hivyo uhalifu wake hautagundulika. Kibaya zaidi wazazi wengi tunajali zaidi kulinda mtoto asipate mimba na kusahau kwamba wahalifu wamebadilisha mbinu. Kama msichana atazoea mtindo huu hata akiolewa anaweza kumshinikiza mumewe. Tumekutana na ndoa kama hizi ambazo mmojawapo analalamika kwamba analazimishwa kujamiiana kinyume na maumbile na anaambiwa kama anakataa atatoka nje kutafuta ambao wako tayari.

6. Watoto wa kike wanaotoka familia ambazo zinakagua zaidi kama ameanza kutembea na wanaume au la bila kutoa elimu ya maadili, haziwasaidii sana. Watoto wanahitaji elimu na ushauri nasaha zaidi kuliko MAKATAZO YASIYO NA SABABU ZILIZOJITOSHELEZA. Niliwahi kupata kisa fulani kwamba msichana alitoka eneo ambapo mwanamke hawezi kuolewa bila kukaguliwa kwanza. Msichana huyu alipofikia kuolewa akakaguliwa na kugundulika kwamba ana sifa kwa vile hajawahi kukutana na mwanaume. Walipopima VVU akagundulika ameambukizwa. Walipofuatilia wakagundua amefanya sana ngono kwa njia ya haja kubwa. Alipoulizwa mazingira gani hatarishi amepitia akasema, “Nilipoenda nje ya nchi kusoma, niliwaomba wapenzi walinde sana ubikira wangu ili nisije nikashindwa kuolewa nikirudi nyumbani. Hivyo wamefanya sana ngono na mimi kwa njia ya haja kubwa.” Kumbuka njia ya haja kubwa ni rahisi zaidi kupata maambukizi ya VVU kwa vile ni rahisi kuchanika na kuruhusu VVU kuingia katika mkondo wa damu kwa kupitia michubuko. (Hata hivyo mtu anaweza kutofanya ngono na bado akawa sio bikira kwa sababu aliwahi kufanyiwa matibabu, kushiriki michezo mbalimbali nk Lakini wakati huohuo hapo kuna ubaguzi wa kijinsia kwa vile kijana wa kiume yeye hakaguliwi).

7. Wazazi wanaolala chumba kimoja na watoto wakubwa na ambao hawajali faragha wanachangia pia kuwaharibu watoto. Siku moja walionekana watoto wakifanya igizo la kujamiiana. Walipoulizwa wakasema waliona wazazi wao wakifanya hivyo usiku. Pamoja na kwamba watoto hawa waliwaona wazazi ambao ni baba na mama, wanaweza kufanya igizo wakiwa wote ni watoto wa jinsi moja au jinsi tofauti.

8. Wazazi/walezi kukosa muda wa kufuatilia mahusiano ya wadada wa kazi na watoto wao. Hata wanapokuwa nyumbani siku za wikiendi wako busy na shughuli zingine. Mama mmoja alishangaa mtoto wake mdogo sana akimpapasa usiku ili amsugue sehemu za siri. Akagundua kwamba dada wa kazi amekuwa akimtumia mtoto huyo kumfanyia kitendo hicho mara kwa mara. Huyo mama akaweka mtego na kugundua kwamba kweli msichana huyo anamtumia mtoto wake kufanya kitendo hicho kwa vidole vyake.

9. Walimu katika shule fulani walishangaa mbona mwanafunzi fulani ana maisha magumu sana lakini anafanana na mama fulani tajiri katika mji huo. Walipomuita mama yake mzazi akawapa kisa hiki: “Nilikuwa msichana wa kazi kwenye familia ya huyo mama tajiri. Nikawa namchezea mtoto niliyekuwa namlea tangu akiwa mdogo mpaka alipobalehe. Nikashangaa nimepata mimba. Hivyo nikatoroka.” Kijana huyo akiwa mkubwa akashangaa kwamba ana mtoto bila kujua na wala kudhamiria.

10. Kukataza watoto wasiguse simu badala ya kuwapa mafunzo ya matumizi sahihi ya simu. Hata kama utamnyima mtoto simu yako anaweza kutumia simu ya rafiki yake. Hivyo njia bora zaidi ni kumfundisha mtoto matumizi sahihi ya simu yako kama vile tovuti za masomo ya kujisomea nk na wakati huohuo ukifuatilia kujua kama aliangalia vitu vingine visivyofaa kwa vile simu inaacha kumbukumbu. Ukigundua hali isiyo ya kawaida utaweza kumsaidia mapema ili akawasaidie na wenzake wanaotaka kumpotosha. Kipindi hiki cha teknolojia ya kidijitali kinahitaji STADI ZA MAISHA kuliko MAKATAZO.

Haya ni machache kati ya mengi ambayo unaweza kuyapata kupitia mafunzo na ushauri tunaotoa kwenye jamii. Tunafanya warsha na kambi zinazolenga wanandoa, vijana, wanafunzi, wanawake, wababa, viongozi wa dini, na viongozi wa jamii bila mipaka yoyote ya kidini.

Katika mpango huu wa vijana unaoitwa NITATOBOA tunalenga kuwasaidia vijana balehe na vijana wadogo katika masuala ya afya ya uzazi, teknolojia na uchumi.

Download & Install app | Lawi Mshana (https://www.appcreator24.com/app2584201-q514wi) ili iwe rahisi kupata mafunzo mengi kwa maandishi, audio na video. Ukiwa na hii APP utaweza kupata huduma zote bure kupitia sehemu moja kama vile Blog yangu, TLMC, BFW, Youtube, TikTok, SoundCloud na Watch & Downlod (utaweza kudownload ninapoweka video hapo).  

Dr Lawi Mshana, 0712-924234