Pengine umekata tamaa kwamba Mungu
hajibu hata unapomtumikia kwa kufunga na kuomba. Napenda kukupa somo muhimu la
kukusaidia. Nimemuona Mungu akijibu baada ya kufanyia kazi vizuizi mbalimbali.
1.
Usijihesabie haki na kuwahukumu wengine
Lk 18:11-14 “Yule Farisayo akasimama akiomba hivi moyoni
mwake; Ee Mungu, nakushukuru kwa kuwa mimi si kama watu wengine, wanyang'anyi,
wadhalimu, wazinzi, wala kama huyu mtoza ushuru. Mimi nafunga mara mbili kwa
juma; hutoa zaka katika mapato yangu yote. Lakini yule mtoza ushuru alisimama
mbali, wala hakuthubutu hata kuinua macho yake mbinguni, bali alijipiga-piga
kifua akisema, Ee Mungu, uniwie radhi mimi mwenye dhambi. Nawaambia, huyu
alishuka kwenda nyumbani kwake amehesabiwa haki kuliko yule; kwa maana kila
ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa.”
Mungu anataka tufunge na kuomba lakini
si kwa dharau na kujihesabia haki. Tabia yako ya kujiona uko viwango vya juu
kuliko waumini wa madhehebu mengine ndiyo inakuponza. Acha kuwanyoshea kidole
watu ambao hujui kwanini Mungu aliwaumba na kwanini pamoja na makosa yao
makubwa Mungu hawaangamizi. Waombee bila kusahau kutengeneza maisha yako binafsi.
Usipokuwa makini utashangaa usiowatarajia
wakijibiwa kabla yako kwa vile wao wamepondeka mioyo na hawatafuti
dhambi za watu wengine.
2.
Kuna dhambi unaijua lakini hutaki
kuiungama na kuiacha
Zab 66:18-20 ‘Kama ningaliwaza maovu moyoni
mwangu, Bwana asingesikia. Hakika Mungu amesikia; Ameisikiliza sauti ya
maombi yangu. Na ahimidiwe Mungu asiyeyakataa maombi yangu, Wala kuniondolea
fadhili zake’. Usidhani kosa linaitwa dhambi unapofumaniwa. Mungu anaiona
dhambi kuanzia moyoni. Unapokusudia mabaya, hata kama hutayafanya kimwili,
tayari umeshaanguka. Ili mradi unahukumiwa moyoni kwamba umemkosea Mungu,
kubali na kutubu hata kama wanaokuzunguka hawajui. 1 Sam 3:13 ‘Kwa maana nimemwambia ya kwamba
nitaihukumu nyumba yake milele, kwa ajili ya ule uovu alioujua; kwa kuwa wanawe walijiletea laana, wala yeye
hakuwazuia.’
Hutapata mafanikio unayoyangojea kama
unajaribu kuficha dhambi zako. Acha kuilea dhambi. Huwezi kumficha Yesu wala
shetani hata kama unatuficha sisi. Mithali 28:13 “Afichaye dhambi zake hatafanikiwa; Bali yeye
aziungamaye na kuziacha atapata rehema.”
3.
Unaabudu sanamu katika moyo wako
Eze 14:3 ‘Mwanadamu, watu hawa wametwaa vinyago vyao na kuvitia mioyoni mwao,
nao wameweka kwazo la uovu wao mbele ya nyuso zao. Je! Ni laiki yangu niulizwe
na wao katika neno lo lote?’ Usikubali kitu chochote kichukue nafasi ya
Mungu katika moyo wako. Mungu hawezi kumvumilia mtu ambaye hajampa nafasi ya
kwanza. Je nafasi yako ya kwanza ni Mungu au ni mke/mume, mpira, mpenzi, kazi,
huduma, askofu, dhehebu, dini, pesa! Anza kujichekecha maana vitu hivyo vikiwa
kipaumbe chako kuliko Mungu vinakuwa kizuizi. Kumbuka baraka za mtu wa Mungu
SIO KUMILIKI PEKE YAKE BALI NI KUFURAHIA ANACHOKIMILIKI. Baraka za Mungu
hazichanganyiki na huzuni. Mithali 10:22 “Baraka
ya Bwana hutajirisha, Wala hachanganyi huzuni nayo.” Unapokuwa na mali
halafu zinakupa tu umaarufu lakini huzifurahii, bado katika uchumi wa Mungu
hujabarikiwa bali umelaaniwa. Ngoja nikupe andiko linaloonyesha kwamba unaweza
kumiliki vitu vizuri na bado uwe umelaaniwa kwa vile umezuiwa kuvifurahia. Sio
lazima laana ikuzuie kupata. Unaweza kupata na usifurahie unachokimiliki. Kum 28:30
“Utaposa mke na mume mwingine atalala
naye; utajenga nyumba usiikae; utapanda mizabibu usitumie matunda yake.”
4.
Wewe ni bahili na mchoyo
Mit 21:13 ‘Azibaye masikio yake asisikie kilio cha maskini, Yeye naye atalia,
lakini hatasikiwa’. Unapuuza mahitaji ya wengine ambayo unaweza kuyatimiza.
Hakuna mtu ambaye hawezi kumbariki mwingine kwa kitu fulani. Ukikosa kitu cha
kutoa, tumia nguvu zako kumsaidia mwingine kazi lakini usione kwamba ni wewe tu
mwenye haki ya kusaidiwa. Tafuta unachoweza kumsaidia mwingine kwa kiwango
chako hata kama ni kumnunulia chungwa au kumsaidia kazi za nyumbani. Mdo 20:35 “Katika mambo yote nimewaonyesha ya kuwa
kwa kushika kazi hivi imewapasa kuwasaidia wanyonge, na kuyakumbuka maneno ya
Bwana Yesu, jinsi alivyosema mwenyewe, Ni heri kutoa kuliko kupokea.”
5.
Kuna mtu umekataa kumsamehe na una
uchungu moyoni
Mt 6:14-15 ‘Kwa maana mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa mbinguni
atawasamehe ninyi. Bali msipowasamehe
watu makosa yao, wala Baba yenu hatawasamehe ninyi makosa yenu.’
Unapofungua mlango ili kumsamehe mtu
fulani, tayari umefungua mlango ili Mungu aingie nyumbani kwako. Usijidanganye
kwamba uko salama kwa kumtumikia Mungu wakati kuna mtu husalimiani naye. Unashauriwa
uache kwanza utumishi wako, ukatengeneze na yeye.
Mt 5:23-26 “Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu
yako ana neno juu yako, iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako,
upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako. Patana na mshitaki
wako upesi, wakati uwapo pamoja naye njiani; yule mshitaki asije akakupeleka
kwa kadhi, na kadhi akakupeleka kwa askari, ukatupwa gerezani. Amin, nakuambia,
Hutoki humo kamwe hata uishe kulipa senti ya mwisho.”
6.
Huombi katika mapenzi ya Mungu
Yakobo 4:3 “Hata mwaomba, wala hampati kwa sababu mwaomba vibaya, ili mvitumie kwa
tamaa zenu.”
Mungu anataka uombe vitu ambavyo ni
mahitaji yako halisi. Usiombe kwa tamaa kwa vile tu umeona mtu fulani anacho au
unataka kushindana naye. Ridhika na aina ya maisha aliyokupangia Mungu. Mungu
atakuinua kwa wakati wake.
1 Yn 5:14 -15 ‘Na huu ndio ujasiri tulio nao kwake, ya kuwa, tukiomba kitu sawasawa na
mapenzi yake, atusikia. Na kama tukijua kwamba atusikia, tuombacho chote,
twajua kwamba tunazo zile haja tulizomwomba.”
Maombi
ya leo
1. Ee Mungu naomba uondoe tabia ya
kifarisayo ndani yangu ya kujiona ni wa maana kuliko wengine.
2. Ee Mungu naomba uondoe tabia ya kujidanganya
kwamba nimekuficha dhambi zangu kwa vile kwa kufanya hivyo ninalaani mafanikio
yangu.
3. Ee Mungu naomba uondoe ibada ya
sanamu ndani ya moyo wangu ili niweze kukuabudu Wewe peke Yako.
4. Ee Mungu naomba uondoe ubahili na
uchoyo ndani yangu ili ninapolia unisikie.
5. Ee Mungu naomba uniwezeshe
kuwasamehe wote walionikosea na nisiwe na uchungu na mtu yeyote moyoni mwangu
6. Ee Mungu naomba uniwezeshe kuomba
maombi yenye kibali mbele zako ili nisipoteze muda wangu.
Naomba Mungu akusaidie kupitia ujumbe
huu uijue dhambi yako na kuishinda ili ufikie kusudi la Mungu kwa ajili ya
maisha yako.
Lawi Mshana, +255712-924234, Tanzania