Ticker

6/recent/ticker-posts

TUSITAFUTE KUFANANA BALI KUKAMILISHANA


 TUSITAFUTE KUFANANA BALI KUKAMILISHANA

Saa 8 usiku wa kuamkia Jumapili juzi nilipata ujumbe kwa ajili ya wachungaji nikaweza kuushirikisha katika ibada ya pamoja ya madhehebu mbalimbali Jumapili hiyohiyo jioni. Nimeona ni ujumbe unaoweza kukufaa pia wewe kama kiungo katika mwili wa Kristo: Niliona niko na wachungaji nikasema maneno haya: “Kila mtu kati yetu ana kitu ambacho mwenzake hana. Tofauti zetu zinakamilishana. Tusitafute kulingana wala kufanana bali kukamilishana. Nikawa naongoza wachungaji kunyoosha na kukunja kiganja. Tukajifunza kwamba kiganja kikikunjuliwa, vidole vinapishana sana urefu lakini tukikunja vidole vinaendana kiasi kwamba tofauti hazionekani sana.” Huu ulikuwa ufunuo mpya kwangu.

Maana yake ni kwamba: 1. Tofauti zinajitokeza zaidi au zinakuwa kubwa zaidi ukiwa peke yako kuliko ukiwa na wenzako 2. Ingawa ukinyosha mkono dole gumba limezidiwa urefu na vidole vyote, ndilo linategemewa kuongeza nguvu wakati wa kushika au kukunja ngumi. 3. Vidole vidogo havipati sapoti ya dole gumba kama ilivyo kwa vidole virefu pale unapokunja ngumi. Mungu alipanga vidole virefu visaidiwe zaidi kuliko vidole vifupi. Vidole vifupi amevipa nguvu ya kutosha kujisimamia. Hata mguuni kidole kidogo ndicho kinachokusaidia usianguke ovyo (kinakupa ‘balance’), ingawa pengine hujawahi kukishukuru wala kujua kama ni cha muhimu kiasi hicho.

Kwa kifupi tunajifunza kwamba TUNAHITAJIANA. Hivyo kila mmoja ajue ana nini na hana nini na nani ana hicho asichokuwa nacho ili waweze kukamilishana. Hii ina maana kwamba uhusiano wa mtumishi na mtumishi usiwe wa kukariri wala wa maeneo yote bali yale ambayo wanaona kwamba wanakamilishana yaani kila mmoja anapata kitu kwa mwenzake. Ukisoma 1 Kor 12 utaona jinsi mtume Paulo alivyotumia mfano wa kulinganisha (analogy) kati ya watumishi na viungo vya mwili. Kila mmoja wetu ni wa muhimu sana katika kuukamilisha mwili wa Kristo. Mdomo wako unauheshimu sana maana unakuwezesha kula vitu vitamu. Na unaweza kuamua uunyamazishe usile chochote kwa kipindi kirefu. Hata hivyo kuna kiungo ambacho hatuwezi kukitaja mbele za watu na wala hatukiheshimu sana lakini kama kikiamua kugoma kufanya kazi yake kwa muda mfupi tu unaweza kulia kama mtoto mdogo. Mungu atusaidie tuheshimu viungo vyote katika mwili wa Kristo bila kujali vina heshima au havina. Barikiwa na Bwana.

1 Kor 12:21-23 “Na jicho haliwezi kuuambia mkono, Sina haja na wewe; wala tena kichwa hakiwezi kuiambia miguu, Sina haja na ninyi. Bali zaidi sana vile viungo vya mwili vidhaniwavyo kuwa vinyonge zaidi vyahitajiwa zaidi. Na vile viungo vya mwili vidhaniwavyo kuwa havina heshima, viungo vile twavipa heshima zaidi; na viungo vyetu visivyo na uzuri vina uzuri zaidi sana.

Lawi Mshana