Ticker

6/recent/ticker-posts

USING’ANG’ANE KUPATA VITU AMBAVYO SIO VYA KWAKO

USING’ANG’ANE KUPATA VITU AMBAVYO SIO VYA KWAKO

Leo saa 10 usiku nikiwa jijini Dodoma nimepata ujumbe huu: Nimeona nikifundisha semina kanisani nikawa naonya kwa sauti kubwa nikisema, “Using’ang’ane kupata vitu ambavyo sio vya kwako. Mtu mmoja akataka nipunguze sauti ili watumishi wanaosoma chuo pembeni wasisikie bali waendelee na darasa lao. Nikasema moyoni kwamba nashukuru wamesikia nilichosema.”

MAANA YAKE

1. Mungu anasema kuna watu wa Mungu wanalazimisha kupata vitu ambavyo Mungu hajawapangia. Biblia imetuagiza kwamba TUHAKIKI NI NINI IMPENDEZAYO BWANA. Waefeso 5:10 “mkihakiki ni nini impendezayo Bwana.” Rum 12:2 “Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.” Kabla ya kufanya maombi ya kung’ang’ana hakikisha kitu hicho ni mpango wa Mungu kwako. Mungu anafanya kazi pamoja na watu wake kwa kuzingatia kusudi lake. Lazima ujue kusudi la Mungu kwako kabla ya kutaka kufanya kazi PAMOJA na Mungu. Warumi 8:28 “Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake.”

Usimtumikie Mungu kwa mazoea. Mfalme Daudi hakutumia kanuni hiyohiyo kwa nyakati tofauti. Alitafuta mwongozo kwa kila aina ya vita na kupewa maelekezo tofauti. Siku moja alipouliza kwamba aende kupigana Wafilisti na kama Mungu atawatia maadui zake chini yake, alikubaliwa kupanda. 2 Sam 5:19 “Basi Daudi akauliza kwa Bwana, akisema, Je! Nipande juu ya Wafilisti? Utawatia mkononi mwangu? Naye Bwana akamwambia Daudi, Panda; kwa kuwa hakika nitawatia Wafilisti mikononi mwako.” Kipindi kingine akapewa mkakati tofauti kwamba asipande bali azunguke nyuma yao ingawa maadui ni haohao. 2 Samweli 5:23 “Naye Daudi alipouliza kwa Bwana, alisema, Usipande; zunguka nyuma yao, ukawajie huko mbele ya miforsadi.” Acha kumzoea Mungu katika utumishi wako kama unataka mafanikio.

2. Kuna watumishi ambao wamenga’ng’ana na elimu kiasi kwamba hawampi Mungu nafasi ya kuzungumza nao. Mungu anapewa nafasi kubwa kwenye SEMINA lakini anakosa nafasi kwenye baadhi ya VYUO. Tusisahau kwamba kanisa la Laodikia lilijisahau kiasi kwamba lilibaki kujiona lina utajiri wakati Bwana Yesu yuko nje ya kanisa. Ilibidi aliambie kanisa hilo kwamba wamfungulie aingie maana hayuko ndani yao ingawa ibada zilikuwa zinaendelea. (Ufu 3:14-22) “Kwa kuwa wasema, Mimi ni tajiri, nimejitajirisha, wala sina haja ya kitu; nawe hujui ya kuwa wewe u mnyonge, na mwenye mashaka, na maskini, na kipofu, na uchi….Tazama, nasimama mlangoni, nabisha; mtu akiisikia sauti yangu, na kuufungua mlango, nitaingia kwake, nami nitakula pamoja naye, na yeye pamoja nami.” Usitegemee elimu hata kama ni ya Theolojia kuliko Mungu mwenyewe. Kuna watumishi katika mji huu ambao wamemkataa Mungu katika fahamu zao. Warumi 1:28 “Na kama walivyokataa kuwa na Mungu katika fahamu zao, Mungu aliwaacha wafuate akili zao zisizofaa, wayafanye yasiyowapasa.”

Elimu ni ya muhimu sana maana hata mimi nimesoma shahada ya udaktari wa masuala ya theolojia kwa miaka mingi (2002-2012) na hata kuja kwangu hapa Dom kipindi hiki nimekuja kufanya maandalizi ya tathmini ya mahitaji ya jamii (needs assessment) kwa ajili ya NGO yetu. Elimu ni ya muhimu sana. Hata Hivyo tuwe waangalifu elimu yetu isitupe kiburi bali itupe unyenyekevu zaidi. 1 Kor 8:1 “…Twajua ya kuwa sisi sote tuna ujuzi. Ujuzi huleta majivuno, bali upendo hujenga.”

Tuna tabia ya kunukuu na kutafsiri vibaya (misquote and misinterpret) maandiko ili kuhalalisha au kutetea mambo tunayotaka kufanya (eisegesis) badala ya kuliacha Neno lijisemee lenyewe na sisi kulifuata kama lilivyo (exegesis). Mfano, kwa kila aina ya elimu tunapenda kusema, Biblia ilisema usimuache elimu aende zake. Na kwa kila maarifa hata yasiyo na maana kwa Mungu, tunasema, Watu wanaangamia kwa kukosa maarifa. Lakini swali la kujiuliza, Je ni kweli hiyo elimu na hayo maarifa tunayotaka kuyasapoti kwa nukuu za maandiko yanakubaliana na Biblia Takatifu au ni kinyume kabisa (out of context)?

Namaliza kwa kusema, TUNAOMBA NA HATUJIBIWI KWA VILE TUNAOMBA KWA NIA MBAYA (WRONG MOTIVE). WAKATI MWINGINE HUNA HITAJI HILO LAKINI UNATAKA KULAZIMISHA ILI TU UFANANE NA JIRANI YAKO. LAKINI PIA HATUJIULIZI KAMA MUNGU ATAPATA UTUKUFU WOWOTE NDANI YAKE. Yakobo 4:3 “Hata mwaomba, wala hampati kwa sababu mwaomba vibaya, ili mvitumie kwa tamaa zenu.”

Mungu akusaidie na kukurudisha kwenye mstari wewe ambaye leo Mungu amenipa ujumbe huu kwa ajili yako.

Lawi Mshana, 0712924234; Tanzania