Ticker

6/recent/ticker-posts

MUNGU ANARUHUSU UPITIE MAGUMU ILI UJUE UMUHIMU WAKE NA NGUVU ZAKE


 MUNGU ANARUHUSU UPITIE MAGUMU ILI UJUE UMUHIMU WAKE NA NGUVU ZAKE

Watu wengi wanajiuliza kwamba inakuwaje Mungu wa upendo na mwenye nguvu zote anaruhusu tupitie magumu ya aina mbalimbali. Nitakupa mifano hai ambayo inathibitisha kwamba Mungu anaruhusu mambo fulani yatokee kwa vile ana kusudi jema mbele yako.

1. Mungu hataki kumuua shetani ili ajue tunampenda kiasi gani na tuzidi kumtegemea

Mungu ametupa ‘utashi’ au ‘uwezo wa kuchagua maisha tunayotaka’ ili mradi tuwe tayari kwa matokeo yake badaye. Kama shetani hangekuwepo ingekuwa vigumu Mungu kujua tunampenda kiasi gani. Unaposhawishiwa na shetani halafu ukaamua kumtii Mungu, unakaribisha baraka kwako na kwenye uzao wako. Maisha yako leo ni matokeo ya uchaguzi ulioufanya au walioufanya watangulizi wako. 

Kum 30:19 “Nazishuhudiza mbingu na nchi juu yenu hivi leo, kuwa nimekuwekea mbele yako uzima na mauti, baraka na laana; basi chagua uzima, ili uwe hai, wewe na uzao wako.”

2. Mungu amempa mkuu wako au mumeo moyo mgumu ili aonyeshe nguvu zake

Hakuna Mwisraeli alifurahia kuteswa na Farao. Lakini kwa upande mwingine Mungu aliruhusu hilo litokee ili atambulishe nguvu Zake katika dunia yote. Israeli walijua umuhimu wa Mungu pale waliposhindwa kwa nguvu zao wenyewe kujinasua katika makucha ya Farao. Kinachokuumiza zaidi sio KILE UNACHOTENDEWA NA ADUI YAKO bali JINSI UNAVYOITIKIA BAADA YA KUTENDWA MABAYA. Kinachokuumiza sio wewe kuitwa mbwa bali ni namna unavyoitikia. Ukikubali kwamba unaweza kuwa mbwa utaumia sana. Lakini ukitambua kwamba huwezi kamwe kuwa mbwa, utapuuzia na kuwa salama. Puuzia majina mabaya unayopewa na watu na badala yake simamia jina jipya ulilopewa na Mungu wako.

Warumi 9:17,18 “Kwa maana maandiko yasema juu ya Farao, ya kwamba, Nilikusimamisha kwa kusudi hili, ili nionyeshe nguvu zangu kwako, jina langu likatangazwe katika nchi yote. Basi, kama ni hivyo, atakaye kumrehemu humrehemu, na atakaye kumfanya mgumu humfanya mgumu.”

3. Mungu ameruhusu upite kwenye bonde la uvuli wa mauti ili uhitaji msaada Wake (gongo lake na fimbo yake vikufariji)

Unaweza kujua maana ya faraja pale unapolia machozi. Faraja haina maana sana kwa mtu anayecheka. Kwa hiyo kuna wakati Mungu anaruhusu upite kwenye hali ngumu ili akikuvusha ujue Mteteaji wako yu hai. Ayubu 19:25 “Lakini mimi najua ya kuwa Mteteaji wangu yu hai, Na ya kuwa hatimaye atasimama juu ya nchi.” Usikubali uongo wa shetani kwamba Mungu amekuacha hata kama unapitia ugumu wowote. Mungu hajawahi kukuacha ila wewe ndiye mara nyingi unamuacha. Waebrania 13:5 “….kwa kuwa yeye mwenyewe amesema, Sitakupungukia kabisa, wala sitakuacha kabisa.”

Zaburi 23:4 “Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti, Sitaogopa mabaya; Kwa maana Wewe upo pamoja nami, Gongo lako na fimbo yako vyanifariji.”

4. Mungu anaweza kuruhusu adui wapigane na wewe lakini kamwe hataruhusu wakushinde

Hata kama kuna watu wanapigana na wewe, HAWATAKUSHINDA kwa vile huko peke yako. Mwanzoni watajifariji kwamba wanakutesa lakini mwisho wao utakuwa mbaya.

Yeremia 15:20 “Nami nitakufanya kuwa kama ukuta wa boma la shaba juu ya watu hawa; nao watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe, ili nikuokoe, na kukuponya, asema Bwana.”

Mungu ameruhusu maji yafike shingoni lakini HAYATAWEZA KUKUGHARIKISHA. Isaya 43:2 “Upitapo katika maji mengi nitakuwa pamoja nawe; na katika mito, haitakugharikisha; uendapo katika moto, hutateketea; wala mwali wa moto hautakuunguza.”

5. Pamoja na mafanikio yaliyoko mbele yako, wengi hawafurahii

Katika mafanikio yako sio wote wanafurahia. Kuna watu watahakikisha wanapinga juhudi zako kwa nguvu zote. Hivyo shetani aliyeshindwa kuzuia mafanikio yako, sasa anatafuta watu wa kupinga mafanikio yako. 1 Wakorintho 16:9 “kwa maana nimefunguliwa mlango mkubwa wa kufaa sana, na wako wengi wanipingao.” Kwa hiyo usichoke kuomba ulinzi wake hata kama umefanikiwa. Zidi kuonyesha uaminifu wako kwa Mungu ili baraka zako ziwe za kudumu na sio za msimu.

Wakati una hali ngumu kimaisha unapewa majina ya kimaskini. Unapofanikiwa usishangae ukiitwa Freemason hata kama hujui maana yake. Na usishangae wanaokuzushia hivyo wakiwa ni marafiki zako wa karibu uliowaamini sana, uliowasaidia sana na ambao hata hawajui Freemasonry ina maana gani. Zab 55:12-14 “Kwa maana aliyetukana si adui; Kama ndivyo, ningevumilia. Aliyejitukuza juu yangu siye anichukiaye; Kama ndivyo, ningejificha asinione. Bali ni wewe, mtu mwenzangu, Rafiki yangu, niliyejuana nawe sana. Tulipeana shauri tamu; na kutembea Nyumbani mwa Mungu pamoja na mkutano.”

Maombi ya wiki hii

1. Ee Mungu naomba unifundishe kuishi maisha ya aina yoyote bila kukuacha kama mtume Paulo alivyosema, “Najua kudhiliwa, tena najua kufanikiwa; katika hali yo yote, na katika mambo yo yote, nimefundishwa kushiba na kuona njaa, kuwa na vingi na kupungukiwa.” (Fil 4:12).

2. Ee Mungu naomba unisaidie nijue sababu ya watu kunipinga wakati sijawakosea ili nisipambane nao bali nikutazame Wewe.

3. Ee Mungu naomba ushughulike na watu wanaopigana nami. “Ee Bwana, utete nao wanaoteta nami, Upigane nao wanaopigana nami.” (Zab 35:1)

Nakuombea upokee baraka zifuatazo:

1. Mungu akufanye ukuta wa boma la shaba juu ya watu wanaopigana nawe ili waumie wenyewe na kuachana nawe ili umtukuze Mungu wako.

2. Mungu akushike usianguke pale maadui zako wanapokusukuma. Zab 118:13 “Ulinisukuma sana ili nianguke; Lakini Bwana akanisaidia.”

Lawi Mshana, 0712-924234; Tanzania