Ticker

6/recent/ticker-posts

Mtetezi wako yu hai, hutaonewa tena!


 Mtetezi wako yu hai, hutaonewa tena!

Mwisho wa kuonewa kwako umefika. Mungu amekuona. Kama ulikuwa unasikia tu watu wakisimulia kwamba Mungu anaweza, SASA jicho lako mwenyewe litaona Mungu akikupigania. Ayubu 42:5 “Nilikuwa nimesikia habari zako, kwa kusikia kwa masikio; Bali sasa jicho langu linakuona.”

Mungu anasema nawe mambo yafuatayo:

1. Kilio chako kimefika kwa Mungu

Mungu amesikia kuugua kwako na amekumbuka agano lake alilokuwa amefanya kuhusu uzima wako. Sasa sio tu kwamba anakuona, bali ANAKUANGALIA.

Kut 2:23-25 “Hata baada ya siku zile nyingi mfalme wa Misri akafa; wana wa Israeli wakaugua kwa sababu ya ule utumwa, wakalia; kilio chao kikafika juu kwa Mungu kwa sababu ya ule utumwa. Mungu akasikia kuugua kwao, Mungu akakumbuka agano lake alilolifanya na Ibrahimu na Isaka na Yakobo. Mungu akawaona wana wa Israeli, na Mungu akawaangalia.”

2. Mungu anataka kuwa mtetezi wako

Umekuwa kama mtu asiye na mtetezi? Mungu anataka kukufuta machozi. Atashuka Mwenyewe hadi hapo kwenye vita zako.

Zab 74:21,22 “Aliyeonewa asirejee ametiwa haya, Mnyonge na mhitaji na walisifu jina lako. Ee Mungu, usimame, ujitetee mwenyewe, Ukumbuke unavyotukanwa na mpumbavu mchana kutwa.” Mungu anataka kutoka kwenye kiti chake mbinguni na kushuka hadi hapo ulipo ili akutetee. Ayubu 19:25 “Lakini mimi najua ya kuwa Mteteaji wangu yu hai, Na ya kuwa hatimaye atasimama juu ya nchi.”

3. Utakuwa mbali na kuonewa

Hakuna kitu kitakachoweza kukutia hofu tena. Waliochezea maisha yako kwa muda mrefu hutawaona tena. SASA utapata amani tele! Isaya 54:14 “Utathibitika katika haki; utakuwa mbali na kuonewa, kwa maana hutaogopa; na mbali na hofu, kwa maana haitakukaribia.” Kutoka 14:13,14 “Musa akawaambia watu, Msiogope, simameni tu, mkauone wokovu wa Bwana atakaowafanyia leo; kwa maana hao Wamisri mliowaona leo hamtawaona tena milele. Bwana atawapigania ninyi, nanyi mtanyamaza kimya.”

4. Yesu alikuja duniani kwa ajili ya watu wanaoonewa

Sasa utajua kwamba Yesu hakuja duniani ili tu umuabudu bali alikuja pia kwa ajili ya kukutoa katika uonevu wa shetani. Mdo 10:38 “habari za Yesu wa Nazareti, jinsi Mungu alivyomtia mafuta kwa Roho Mtakatifu na nguvu naye akazunguka huko na huko, akitenda kazi njema na kuponya wote walioonewa na Ibilisi; kwa maana Mungu alikuwa pamoja naye.”

5. Mungu anataka kuwa ngome na kimbilio lako.

Kuanzia sasa hutawakimbilia wanadamu bali Mungu aliyekuleta duniani. Waliokuwa wamekushika na kukufanya kama msukule, hawataweza kukushika tena. Bwana wa majeshi ni Mkombozi wako. Zaburi 9:9 “Bwana atakuwa ngome kwake aliyeonewa, Naam, ngome kwa nyakati za shida.” Yer 50:33-34 “Bwana wa majeshi asema hivi, Wana wa Israeli, na wana wa Yuda, wameonewa pamoja; na wote waliowachukua mateka wanawashika sana; wanakataa kuwaacha. Mkombozi wao ni hodari; Bwana wa majeshi ndilo jina lake; yeye atawatetea kwa bidii, apate kuistarehesha nchi, na kuwasumbua wakaao katika Babeli.”

Wiki hii mshukuru Mungu hivi:

1. Ee Mungu nakushukuru kwamba sasa sio tu kwamba unaiona bali umeniangalia kwa karibu kama mtoto wako unayempenda.

2.  Ee Mungu nakushukuru kwamba umeamua ushuke mwenyewe na kunitetea katika mappito yangu.

3. Ee Mungu nakushukuru kwamba umewatowesha wote waliokuwa wanatishia maisha yangu Hivyo amani yako itathibitika kwangu.

4. Ee Mungu nakushukuru kwamba sitaendelea kuwa muumini aliyezoea kuonewa na ibilisi bali sasa niko huru kabisa.

5. Ee Mungu nakushukuru kwamba sasa WEWE ndiye kimbilio langu kwa hiyo sitaishi tena kama mateka au msukule. Nitaona nikinufaika na kazi zangu ninazozitaabikia.

Mungu aione shukrani yako kwake wiki hii na kukupa thawabu ya majibu dhahiri katika Jina la uweza la Yesu Kristo!

Lawi Mshana, 0712-924234