Ticker

6/recent/ticker-posts

Mungu anataka kukurejeza katika ubora uliokuwa nao


 Mungu anataka kukurejeza katika ubora uliokuwa nao

Usiku wa kuamkia jana niliona maneno haya:”RESTORATION, RESTORATION, RESTORATION.” Maana ya RESTORATION ni UREJESHO. Kurejeshwa katika ubora uliokuwa nao awali.

Maana yake: Ujumbe huu ni wa kwako wewe ambaye umepoteza hali yako ya kwanza. Shauku yako imepotea, pesa zimepotea, amani imepotea, umepoteza furaha ya wokovu wako, umepoteza upendo wako wa kwanza nk. Ufu 2:4 “Lakini nina neno juu yako, ya kwamba umeuacha upendo wako wa kwanza.”

Mungu anakwenda kukurudishia furaha ya wokovu wako leo ili na wewe ucheke kuanzia moyoni. Zaburi 51:12 “Unirudishie furaha ya wokovu wako; Unitegemeze kwa roho ya wepesi.” Lakini pia Mungu anataka kukurudishia miaka yako iliyopotea. Kuna matatizo mengi yamekula miaka yako lakini Mungu ni mwaminifu. Yoeli 2:25 “Nami nitawarudishia hiyo miaka iliyoliwa na nzige, na parare, na madumadu, na tunutu, jeshi langu kubwa nililotuma kati yenu.”

Hatua za kuchukua ili urejezwe na Bwana:

1. Funga saumu inayokubalika kwa Mungu

Usifunge ili kutimiza wajibu tu. Maombi ya kufunga yana kanuni zake. Usilemee watu kazi kisa umefunga. Saumu yako ikiwa sahihi, utakuwa baraka kwa wengi na utakarabati maeneo mengi yaliyochoka badala ya kuyanyoshea kidole.

Isaya 58:6,12 “Je! Saumu niliyoichagua, siyo ya namna hii? Kufungua vifungo vya uovu, kuzilegeza kamba za nira, kuwaacha huru walioonewa, na kwamba mvunje kila nira? Na watu wako watapajenga mahali palipokuwa ukiwa; utaiinua misingi ya vizazi vingi; nawe utaitwa, Mwenye kutengeneza mahali palipobomoka; na, Mwenye kurejeza njia za kukalia.”

2. Rudi kwa Bwana Mungu wako

Mungu anatafuta UKARIBU NA WEWE (INTIMACY) kuliko utumishi wako kwake. Tafuta ushirika na Yeye kuliko kumtumikia. Ukiwa karibu na Yeye utagundua anataka nini kwako. Kwa hiyo hutafanya huduma ambazo hazina mguso kwake.

Yeremia 15:19 “Kwa sababu hiyo Bwana asema hivi, Ukirudi, ndipo mimi nitakapokurejeza, upate kusimama mbele zangu; nawe ukitoa kilicho cha thamani katika kilicho kibovu, utakuwa kama kinywa changu; nao watakurudia wewe, bali hutawarudia wao.”

Dada yetu Martha alidhani anajua sana mahitaji ya Bwana Yesu. Hivyo Bwana alipofika numbani kwao hakumuuliza chochote zaidi ya kukimbilia jikoni. Haikutosha kufanya hivyo bali alimlaumu hata Bwana Yesu kwamba kwanini hamfukuzi Mariamu ili wasaidiane kuandaa chakula. Luka 10:40-42 “Lakini Martha alikuwa akihangaika kwa utumishi mwingi; akamwendea, akasema, Bwana, huoni vibaya hivyo ndugu yangu alivyoniacha nitumike peke yangu? Basi mwambie anisaidie. Bwana akajibu akamwambia, Martha, Martha, unasumbuka na kufadhaika kwa ajili ya vitu vingi;lakini kinatakiwa kitu kimoja tu; na Mariamu amelichagua fungu lililo jema, ambalo hataondolewa.”

3. Usipende kufanana na dunia hii

Chagua kuwa mwana wa mfalme badala kuwa mtu wa dunia hii. Mathayo 13:38 “lile konde ni ulimwengu; zile mbegu njema ni wana wa ufalme; na yale magugu ni wana wa yule mwovu.” Kumbuka hii dunia inapita na tamaa zake. 1 Yohana 2:17 “Na dunia inapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele.”

Huhitaji kuokoka roho peke yake. Unahitaji pia mageuzi kwenye mtazamo wako (mindset). Mageuzi haya ni ya KUFANYWA UPYA. Warumi 12:2 “Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.” Mruhusu Roho Mtakatifu akufanye upya katika utu wa ndani ndipo hutalegea katika maisha yako. 2 Wakorintho 4:16 “Kwa hiyo hatulegei; bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa, lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku.” Tito 3:5 “si kwa sababu ya matendo ya haki tuliyoyatenda sisi; bali kwa rehema yake, kwa kuoshwa kwa kuzaliwa kwa pili na kufanywa upya na Roho Mtakatifu.”

TAHADHARI

Hata hivyo ukitenda dhambi kwa makusudi unaweza kufikia hatua hutengenezeki tena. Unafikia hatua ambayo mahubiri hayakuchomi tena katika moyo wako. Badala yake yanateleza tu juu ya moyo wako kama kama maji yanavyoteleza kwenye mawe ya mtoni. Haya mawe ya mtoni hayana maji ndani ila yamechongwa kwa nje kiasi kwamba yanafaa tu kusugulia miguu. Usijifariji kwamba utatubu wakati unakaribia kufa. Hakuna uhakika kama toba za aina hii zote zinakubaliwa. Hebu soma maandiko haya:

Waebrania 6:6 “wakaanguka baada ya hayo, haiwezekani kuwafanya upya tena hata wakatubu; kwa kuwa wamsulibisha Mwana wa Mungu mara ya pili kwa nafsi zao, na kumfedhehi kwa dhahiri.”

Waebrania 10:26,27 “Maana, kama tukifanya dhambi kusudi baada ya kuupokea ujuzi wa ile kweli, haibaki tena dhabihu kwa ajili ya dhambi; bali kuna kuitazamia hukumu yenye kutisha, na ukali wa moto ulio tayari kuwala wao wapingao.”

Maombi ya wiki hii:

1. Ee Mungu naomba uondoe maombi ya kufunga ya mazoea ili nipate majibu yanayotia moyo.

2. Ee Mungu naomba uniwezeshe kutambua thamani ya kuwa karibu na wewe ilivyo kubwa kuliko kupata vitu kutoka kwako.

3. Ee Mungu naomba unitengeneze niwe mwana wa ufalme wako ili nisikimbizane tena na dunia hii inayopita na tamaa zake.

Lawi Mshana, 0712-924234