Ticker

6/recent/ticker-posts

MATENDO MAKUU YA MUNGU KATIKA UZINDUZI RASMI WA MAOMBEZI YA NYUMBA KWA NYUMBA




MATENDO MAKUU YA MUNGU KATIKA UZINDUZI RASMI WA MAOMBEZI YA NYUMBA KWA NYUMBA

Leo nimeanza rasmi kufanya huduma za maombezi katika nyumba ninazoalikwa. Nimeona uhitaji mkubwa pale watu watano walipolipuka mapepo. Majirani walishiriki kwa ajili ya maombezi ya afya na upenyo wa kiuchumi. Kesho saa 10.30 jioni tumetenga muda maalum kwa ajili yao ili kubomoa madhabahu zilizokuwa zimewashikilia hao ambao mapepo yalijidhihirisha pamoja na wahitaji wengine.

Matatizo mengi hayaishi kwa vile hatuchukui muda wa kutosha kutambua yalivyoanza na mabadiliko yanayotokea. Tusiwalazimishe watu kukiri ushindi hasa pale ambapo hakuna dalili zozote za uponyaji.

Ingawa Yesu aliponya kimuujiza, kuna siku alimfungua mtu kwa mchakato na sio papo kwa papo.

Mk 8:22-26 “22 Wakafika Bethsaida, wakamletea kipofu, wakamsihi amguse. 23 Akamshika mkono yule kipofu, akamchukua nje ya kijiji, akamtemea mate ya macho, akamwekea mikono yake, akamwuliza, Waona kitu? 24 Akatazama juu, akasema, Naona watu kama miti, inakwenda. 25 Ndipo akaweka tena mikono yake juu ya macho yake, naye akatazama sana; akawa mzima, akaona vyote waziwazi. 26 Akampeleka nyumbani kwake, akisema, Hata kijijini usiingie.”

Mchakato ulikuwa hivi:
1. Alimtoa nje ya chanzo cha matatizo yake – kuna watu wanahitaji kuombewa mbali na nyumba zao kutokana na maagano yaliyopo hapo. Vinginevyo, tatizo litarudi haraka.

2. Alipomwekea mikono alimuuliza kama anaona kitu – alitaka kujua kama kuna mabadiliko yameanza. Mtu anapowekewa mikono anapaswa kusema anavyojisikia ili mwombaji ajue anatakiwa kuombaje zaidi.

3. Alisema uhalisia kwamba anaona nusunusu (maruerue) – hakuna haja ya kukiri umepona wakati maumivu yanaendelea. Sema ili uombewe zaidi. Hata hivyo mwambie shetani kwa kupigwa kwake Yesu wewe umepona. Ila waombaji waeleze uhalisia.

4. Yesu aliweka tena mikono yake – kutokana na maelezo yake kwamba hajafunguliwa vizuri, Yesu aliweka mikono yake TENA.

5. Akatazama sana (akakaza macho) – mtu anapoombewa aonyeshe bidii ya kufanya alichokuwa hawezi. Kwa kufanya hivyo, atasababisha muujiza utokee na kutambua kama ameshapona.

6. Yesu akampeleka nyumbani kwake na kumzuia kurudi kijijini kwake – agano la shetani katika kijiji chake lingeweza kumsumbua kama hajaimarika zaidi. Kama hospitalini wanavyomlaza mtu, hata katika huduma kuna watu wanatakiwa kuzuiwa kurudi nyumbani hadi wakati fulani.

Tuombee ili huduma hii iwaguse wengi bila kujali wanaabudu au la kwa vile Mungu ana mpango na kila mtu aliyemuumba. Ni gharama kuwafikia lakini kwa maombi yako tutaweza kuwafikia bila kuwachangisha pesa.

Lawi Mshana, 0712-924234