Ticker

6/recent/ticker-posts

TUSIWE WATUMWA WA MADENI SABABU YA SHEREHE (Video na Maandishi)

 TUSIWE WATUMWA WA MADENI SABABU YA SHEREHE (Bofya hapa uangalie video)

TUSIWE WATUMWA WA MADENI SABABU YA SHEREHE

Ndoto: Hivi karibuni nimeona waumini wakionywa kwamba waepuke kuwa watumwa wa madeni kwa sababu ya sherehe.

Tumefika wakati ambapo sherehe zimeanza kupoteza lengo lake. Zimeanza kuwa mzigo badala ya kuwa baraka. Watu wanakopa kwa ajili ya kufurahisha watu na kisha wanajikuta ni watumwa wa madeni. Wengine wanauza zawadi walizopewa kwenye harusi.

Mambo ya msingi kuzingatiwa na wacha Mungu katika sherehe kwa mujibu wa Neno la Mungu:

1 Pet 4:2-5 “2 Tangu sasa msiendelee kuishi katika tamaa za wanadamu, bali katika mapenzi ya Mungu, wakati wenu uliobaki wa kukaa hapa duniani. 3 Maana wakati wa maisha yetu uliopita watosha kwa kutenda mapenzi ya Mataifa; kuenenda katika ufisadi, na tamaa, na ulevi, na karamu za ulafi, na vileo, na ibada ya sanamu isiyo halali; 4 mambo ambayo wao huona kuwa ni ajabu ya ninyi kutokwenda mbio pamoja nao katika ufisadi ule ule usio na kiasi, wakiwatukana. 5 Nao watatoa hesabu kwake yeye aliye tayari kuwahukumu walio hai na waliokufa.”

Ufafanuzi kuhusu huu ujumbe wa mtume Petro:

1. Kuacha mapokeo ambayo yanapingana na Neno la Mungu – kwa vile mmeanza safari ya kiroho msiishi kama zamani kabla hamjaamini – zamani mlienenda katika ufisadi (lewdness) – matendo ya zinaa/kingono kv kuangalia watu ambao wako nusu uchi, kuvaa nusu uchi nk;

tamaa (lusts) – tamaa mbaya za mwili (kuwashana tamaa),

ulevi – watu wanajumuika wakiwa wamelewa

karamu za ulafi – kufanya mambo ambayo si ya msingi. Mtu anakodi gauni laki 2-5 lakini hana chakula cha wiki moja.  

vileo (drinking parties) na

ibada ya sanamu isiyo halali (abominable idolatries) – kumtukuza mwanadamu badala ya Mungu. Mungu hapewi nafasi sherehe nzima.

Je hatujiulizi kwamba katika kumbi za sherehe nyingi tunalazimishwa kucheza dansi (miziki ya dunia yenye matusi), tunachangia pombe hata kama hatunywi, zinavaliwa nguo za makahaba (mtu huyohuyo aliyevaa vizuri kanisani, ukumbini anakuwa nusu uchi). Unadhani hatunajisiki katika mazingira hayo? Au ni mpaka mahali paitwe baa tu? 

2. Kuwa tayari kutukanwa tunapoepuka ufisadi huo – mst 4 “mambo ambayo wao huona kuwa ni ajabu ya ninyi kutokwenda mbio pamoja nao katika ufisadi ule ule usio na kiasi, wakiwatukana.”

Wasiomjua Mungu watakushangaa na kukutukana – Neno limesema wazi. Kwamba hutapongezwa bali utatengwa.

3. Wanaopinga msimamo wako watahukumiwa siku ya mwisho – mst 5 “Nao watatoa hesabu kwake yeye aliye tayari kuwahukumu walio hai na waliokufa.”

Kitendo cha kukupinga hakitawaacha salama siku ya hukumu.

Sasa ufanyeje kama mtu wa Mungu:

1. Changia na kushiriki sherehe ambayo utapata shangwe ya moyo na sio maumivu na kulemewa.

Esta 8:17 “Na katika kila jimbo, na kila mji, po pote palipowasili amri ya mfalme na mbiu yake, Wayahudi wakapata furaha na shangwe, karamu na sikukuu.”

2. Usiishi kwa kuwaogopa wanadamu. Mwogope Mungu na kuisimamia imani yako.

Mithali 29:25 “Kuwaogopa wanadamu huleta mtego; Bali amtumainiye Bwana atakuwa salama.”

3. Fanya sherehe za kiwango chako na maadili yako na kuwajulisha watu mapema.

Warumi 12:16 “Mpatane nia zenu ninyi kwa ninyi. Msinie yaliyo makuu, lakini mkubali kushughulishwa na mambo manyonge. Msiwe watu wa kujivunia akili.”

Ukichangisha kila mtu itabidi naye akuchangishe hata kama ya kwake haina maadili kama ya kwako. Huna sababu za kukopa kwa ajili ya sherehe.

4. Usifanye sherehe ambazo unawaalika waliokuchangia tu – kama unataka thawabu

Luka 14:12-14 “Akamwambia na yule aliyemwalika, Ufanyapo chakula cha mchana au cha jioni, usiwaite rafiki zako, wala ndugu zako, wala jamaa zako, wala jirani zako wenye mali; wao wasije wakakualika wewe ukapata malipo.Bali ufanyapo karamu waite maskini, vilema, viwete, vipofu, nawe utakuwa heri, kwa kuwa hao hawana cha kukulipa; kwa maana utalipwa katika ufufuo wa wenye haki.”

Kuna watu wengi wametoa mchango katika maisha yako kiasi kwamba huwezi kuwaacha kwa sababu tu hawakuchangia fedha. Chakula kizuri ni kile ambacho umemuandalia mgeni bila yeye kuchangia.

5. Epuka wanakamati na viongozi ambao hawatambui wala kuheshimu imani na maadili yako. Amosi 3:3 “Je! Watu wawili waweza kutembea pamoja, wasipokuwa wamepatana?”

6. Epuka sherehe zinazoweza kukutoa kafara

Kutoka 34:15 “Usije ukafanya agano na wenyeji wa nchi, watu wakaenda kufanya uzinzi na miungu yao, na kuitolea sadaka miungu yao; mtu mmoja akakuita, ukaila sadaka yake.”

Maombi ya wiki hii:

1. Ee Mungu naomba unipe ujasiri wa kukataa mapokeo yanayopingana na Neno lako hata kama nitatengwa na dunia.

2. Ee Mungu naomba uniwezeshe kutambua kiwango cha maisha ulichonipangia ili nisishindane na watu waovu.

UNAWEZA KUWASILIANA NAMI KWA MAOMBI NA USHAURI KWA SIMU NAMBA 0712-924234