Ticker

6/recent/ticker-posts

TUMEKUWA WAPOKEAJI KWA MUDA MREFU, SASA NA SISI TUBARIKI WENGINE


 TUMEKUWA WAPOKEAJI KWA MUDA MREFU, SASA NA SISI TUBARIKI WENGINE

Tunashukuru kwa mara nyingine tumepokea nguo (suruali na mashati) kutoka kwa mpendwa kutoka Singida. Nikuhakikishie kwamba umepanda kwenye udongo wenye rutuba. Nguo hizi zitavaliwa na watu ambao huwajui kwa hiyo thawabu yako itakuwa kubwa zaidi mbinguni. Wengi wetu tunasaidia zaidi watu tunaowajua na wanaotupa asante, kwa hiyo thawabu yetu tunaipata hapahapa duniani. Hakuna mtu atapata thawabu mbinguni kwa kitu ambacho dunia ilishamlipa. Mathayo 6:1 “Angalieni msifanye wema wenu machoni pa watu, kusudi mtazamwe na wao; kwa maana mkifanya kama hayo, hampati thawabu kwa Baba yenu aliye mbinguni.”

Mpendwa uliyeguswa kutoa msaada huu, Mungu atimize mahitaji yote uliyoorodhesha kwamba unahitaji Mungu akutendee kwa sababu Neno limesema anabarikiwa (ni heri) anayetoa kuliko anayepokea.” Mdo 20:35 “Katika mambo yote nimewaonyesha ya kuwa kwa kushika kazi hivi imewapasa kuwasaidia wanyonge, na kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, jinsi alivyosema mwenyewe, Ni heri kutoa kuliko kupokea.”

Nilipoenda nchi fulani kufundisha viongozi wa dini takriban 40 hivi na kuwahudumia chakula cha mchana. Mchungaji Mtanzania anayeishi nchi hiyo aliniambia jambo hilo limewagusa sana kwa vile linafanywa na wahubiri wazungu tu. Nimejifunza kwamba hatushindwi kuhudumia watu kama tungepiga mahesabu ya sherehe tunazochangia kwa mwaka. Wazungu wanafanya mengi kwa vile wengi wao sherehe sio za lazima. Wanapoona tunafanya sherehe za kifahari wanadhani zimeandaliwa na matajiri wakubwa sana. Kumbe nyingi ni za watu maskini ambao sherehe ni kipaumbele kikubwa kwetu kuliko hata kusomesha watoto.

Lakini pia wengine wanapoona naenda kuhubiri nchi zingine wanadhani ni kama kwenda kutalii. Hawajui ugumu wa huduma za kimisheni. Nilienda nchi fulani nikafika katika kijiji ambacho nililala mazingira ya shida ambayo sijawahi kulala katika mazingira kama hayo kwa hapa kwetu na mboga niliyoandaliwa ilikuwa ni panya na sijawahi kumla. Unapochangia huduma hii unawezesha usafiri pamoja na kuwalisha chakula washiriki ili walengwa wa hali zote wafikiwe.

Tangazo

Napenda kuwakumbusha vijana wenye umri wa miaka 18-35 wenye ujuzi, uzoefu na ndoto fulani wajitambulishe ili kupitia ofisi yetu ya kujenga uwezo (empowerment office) chini ya Beyond Four Walls, tuwaunganishwe na fursa zinapojitokeza. Hakuna mtu ataota kwamba kijana fulani ana elimu fulani, utayari fulani, maono fulani na anapatikana katika mji au kijiji fulani. Nakumbuka tulipata tabu kupata vijana wa kujitolea wenye ujuzi fulani tulipokuwa tunafanya tathmini ya awali kwa vile hakuna mahali maalum pa kuwapata. Hapa tunajali ujuzi rasmi na usio rasmi. Kuna vijana wanaweza kufanya mambo mengi ingawa hawana vyeti vya mambo hayo. Kwa hiyo sisi tunahitaji kutambua wasifu wa kijana kwa ujuzi wake rasmi na usio rasmi kuanzia waliomaliza darasa la saba hadi chuo kikuu.

Lakini pia tunahitaji kufahamu taasisi zinazohitaji kutambulisha fursa walizo nazo na masharti yao kwa ajili ya vijana ili mradi taasisi hizo ziwe zinafanya kazi za halali, zinatambuliwa na serikali yetu na zinafanya kazi kwa mujibu wa sheria. 

Dr Lawi Mshana, 0712-924234 (Simu na Whatsapp)