Ticker

6/recent/ticker-posts

MAFUNZO MAALUM KWA AJILI YA WAZAZI NA WALEZI




 MAFUNZO MAALUM KWA AJILI YA WAZAZI NA WALEZI

Ni ukweli usiopingika kwamba wazazi ndio walezi wakuu (primary caregivers) wa watoto. Na wajibu huu wamepewa na Mungu mwenyewe. Kinyume chake tumeanza kuhamishia wajibu huu kwa watu wengine ambao walitakiwa tu kuunga mkono juhudi zetu. Kwa bahati mbaya wapo wazazi wanaodhani kuwa wajibu wa kulea watoto wao ni wa mabinti wa kazi (house girls), walimu wa watoto katika nyumba za ibada, walimu wa shule au hata shangazi na bibi. Wengine wameenda mbali zaidi wanadhani ni kazi ya serikali kuwalea watoto wao waliowazaa wenyewe na wengine wameamua wamuachie Mungu kana kwamba watoto wao walianguka kutoka mbinguni.

Tunataka kuwarudisha wazazi kwenye misingi. Tumeanza na mada ya kujadili namna tulivyolelewa na jinsi hali hiyo inavyoathiri namna tunavyowalea watoto wetu leo. Tulijifunza aina za uleaji (parenting styles) tukagundua kwamba tuna mapungufu makubwa. Kuna vitu vingi watoto wanavikosa kwetu na ndiyo maana wanageukia mitandao ya jamii na watu mbadala ili wawasaidie. Matokeo yake wakiharibika tunalaumu utandawazi wakati hatujawahi kuwapa malezi yoyote. Tunadhani tukiwapa chakula na kulipa ada za shule kwa uaminifu tumeshawalea tayari.

Hata maandiko yanasema kwamba maisha ya mtu kuanzia utoto hadi uzee wake yanategemea alilelewaje na sio tu alivyoombewa au kusomeshwa shule. Mithali 22:6 “Mlee mtoto katika njia impasayo, Naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.”

Watoto wa wanyama wakishazaliwa tu wanaanza kujitegemea kwa vile Mungu hakuwapa wanyama akili ya kulea kama sisi. Watoto wetu wanachukua muda mrefu sana kwa vile tuna wajibu wa kuwasaidia wawe watu wenye tabia fulani. Huwezi kuwafanya watoto wawe tofauti na wewe (labda Mungu mwenyewe aingilie kati). Tenda yale unayotaka watoto wako wayaige. Usijidanganye kwa kuwaambia, “fanyeni yale ninayosema, msiangalie matendo yangu.” Kanuni ya kupanda na kuvuna inasema kila mti utazaa matunda yanayofanana na mti wenyewe. Mwanzo 1:12 “Nchi ikatoa majani, mche utoao mbegu kwa jinsi yake, na mti uzaao matunda, ambao mbegu zake zimo ndani yake, kwa jinsi yake; Mungu akaona ya kuwa ni vyema.”

Mpango huu utawafikia pia walimu, wahudumu wa afya na viongozi wa dini kadiri tutakavyopata raslimali za kuwafikia.

Mlango uko wazi wa kushirikiana na wadau mbalimbali wenye shauku ya kuona familia zikiwa imara kwa ajili ya taifa zima.

Dr Lawi Mshana, Beyond Four Walls, +255 712924234