Ticker

6/recent/ticker-posts

LEO VIONGOZI WA MADHEHEBU TOFAUTI WAMESHIRIKI MAFUNZO HAPA BURUNDI



 LEO VIONGOZI WA MADHEHEBU TOFAUTI WAMESHIRIKI MAFUNZO HAPA BURUNDI

Pamoja na mvua nyingi na majukumu mengi ya viongozi wa makanisa hasa siku za Jumamosi, bado wamejitahidi kushiriki. Wametamani kipindi kingine tuwape fursa wengi zaidi kushiriki mafunzo kama haya.

Tumejifunza JINSI YA KUTUMIKA KATIKA WITO AMBAO MTU AMEPEWA NA MUNGU. Tumeongozwa na andiko la 2 Petro 1:10 “Kwa hiyo ndugu, jitahidini zaidi kufanya imara kuitwa kwenu na uteule wenu; maana mkitenda hayo hamtajikwaa kamwe.” Mtumishi wa Mungu asipojitahidi kuimarisha wito na uteule wake lazima atajikwaa. Bwana Yesu aliwahi kuwauliza wanafunzi wake kama walipungukiwa na kitu alipowatuma. Wakasema, La. Sisi leo tunapungukiwa kwa vile tunafanya huduma ambazo ziko nje ya wito wetu. Baraka za mtumishi wa Mungu ziko katika kusimamia wito wake. Hata katika kazi za ajira, mfanyakazi analipwa kwa ile kazi ambayo ana mkataba wake tu. Akifanya zingine asitegemee kulipwa hata kama amefanya vizuri na kuchoka.

Lakini pia tumekumbushana jinsi ya kuwekeza katika ndoa na familia zetu. Kuna watumishi wamezama katika huduma za kiroho mpaka wamesahau ndoa na familia zao. Wamesahau kwamba Mungu alianzisha ndoa na familia kabla ya Kanisa. Kanisa liliasisiwa kama njia ya kumrudisha mwanadamu katika mstari lakini kamwe sio mbadala wa familia.

Maombi yako ni muhimu sana ili watumishi wengi zaidi wajengewe uwezo kwa vile wanalisha waumini kiroho wakati wao wenyewe wamepungukiwa. Mama anayenyonyesha anahitaji sana matunzo ili atoe maziwa mengi na bora kwa mtoto wake.

Karibu sana uwe sehemu ya kuwatia moyo watumishi wa Mungu bila mipaka ya kimadhehebu.

Dr. Lawi Mshana