Ticker

6/recent/ticker-posts

Tumeanza semina yetu hapa Burundi


Tumeanza semina yetu hapa Burundi

Semina hii imebebwa na kichwa kinachosema POKEA MWELEKEO MPYA WA MAISHA ambapo andiko la msingi ni Kum 2:3 “Mlivyouzunguka mlima huu vyatosha; geukeni upande wa kaskazini.” Pengine hata wewe umezunguka milima kwa muda mrefu. Sasa Mungu anataka upige hatua kuelekea mbele kwenye hatima yako.

Maisha ya watu wa Mungu wengi yamekuwa duni kwa vile wanajali roho zao tu na kusahau nafsi zao. Matokeo yake tunakuwa na watu waliojitakasa vizuri rohoni lakini maisha yao kiuchumi hayana mwelekeo. Katika ‘nafsi’ ndipo kuna KUHISI, KUFIKIRI NA KUAMUA. Hivyo mtu anaweza kuwa mzuri katika huduma za kiroho (rohoni) lakini anafanya maamuzi mabaya katika maisha yake na kujikuta akiwabebesha wengine lawama kwa matatizo aliyoyasababisha mwenyewe. Hata kama uko vizuri kiroho, lazima UGEUZWE NA KUFANYWA UPYA NIA (MINDSET) YAKO ndipo utajua vizuri mapenzi ya Mungu kuhusu maisha yako. Rum 12:2 “Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.”

Lakini pia wengi wanaotaka baraka za Mungu hawamtumikii Mungu kwa lolote. Hivyo mafanikio yao yanategemea juhudi zao tu bila mkono wa Mungu (God’s favour). Mafanikio kutoka kwa Mungu yanahitaji mtu awe ANAMSIKIA NA KUMTUMIKIA MUNGU. Yaani, asikie Mungu anamtaka afanye nini leo na awe na huduma fulani anayofanya kwa ajili ya Mungu. Ayubu 36:11 anasema hivi “Kama wakisikia na kumtumikia, Watapisha siku zao katika kufanikiwa, Na miaka yao katika furaha.”

Hata hivyo mtu anatakiwa ajiridhishe kama kweli anamtumikia Mungu na sio dini peke yake. Unaweza kuhatarisha maisha yako katika dini au dhehebu wakati hatari hizo hazina uhusiano wowote na wito wako wala Ufalme wa Mungu. Kuna tofauti ya kufia dini au dhehebu na kufa kwa ajili ya Kristo (kuwa shahidi Wake). Mdo 1:8 “Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.”

Barikiwa na Bwana

Dr. Lawi Mshana, +255712924234, Tanzania