Ticker

6/recent/ticker-posts

TUNAWEZAJE KUWANUSURU WACHUNGAJI WASIPATE MAUMIVU KATIKA MAISHA YAO? (Sura ya 3)

TUNAWEZAJE KUWANUSURU WACHUNGAJI WASIPATE MAUMIVU KATIKA MAISHA YAO? (Sura ya 3)

Naendelea na muhtasari wa sura ya tatu ya kitabu cha Kilio cha Wachungaji

Sura ya Tatu (kwa muhtasari)

Kuwanusuru Wachungaji kutoka katika Maumivu

1. Mateso yanaporuhusiwa na Bwana, yanaweza kumuimarisha mchungaji. 1 Pet 5:10 ‘Na Mungu wa neema yote, aliyewaita kuingia katika utukufu wake wa milele katika Kristo, mkiisha kuteswa kwa muda kidogo, yeye mwenyewe atawatengeneza, na kuwathibitisha, na kuwatia nguvu’.  Mchungaji anatakiwa kuyapokea mateso ya kimungu kwa mtazamo mzuri ndipo yatatumiwa kama mawe ya kumsaidia kuvuka ng’ambo ya pili (stepping stone). Mungu haruhusu mateso kwa ajili ya kumvunja moyo mtumishi wake. Kinachoweza kumuumiza mchungaji, ni namna yeye mwenyewe anavyoyatafsiri au kuyapokea mateso anayoyapata. Akiwa tayari kujifunza kusudi la Mungu ndani ya mateso hayo, yatakuwa baraka kwake. Lakini akilalamika na kuhamishia lawama kwa watu wengine, mateso hayo yatamfanya awe mchungu. Ukiitikia vyema (respond) mateso, yanaweza kukufanya uwe mzuri (better) lakini ukiitikia vibaya (react), yanaweza kukufanya uwe mchungu (bitter). Kuna mfano mzuri wa watu wawili waliowahi kutukanwa kwamba ni mbwa. Mmoja akasema najua hata siku moja siwezi kubweka hivyo akapuuzia lakini mwenzake akawaza sana mbwa alivyo na mdomo mrefu na jinsi alivyofananishwa naye, akaamua kupambana. Kinachotuathiri na kutuumiza mara nyingi sio maneno yanayosemwa juu yetu bali ni namna tunavyoyatafsiri maneno hayo.

2. Mchungaji anahitaji kupata malezi kutoka kwa watu anaowatumikia. Ili mchungaji aifurahie kazi yake, anahitaji kanisa analolisimamia liweze kutosheleza mahitaji ya msingi ya familia yake. Mchungaji anajisikia vizuri sana anapoona kwamba anamudu kujikimu kwa sababu ya utoaji wa kanisa lake kuliko kwa kufanya kazi zake binafsi. Hapa sina maana kwamba ni vibaya mchungaji kuwa na shughuli binafsi inayomuongezea kipato. Mchungaji anaweza kuwa na shughuli ya kuongeza kipato kama mtume Paulo alivyoshona mahema (Mdo 18:2,3) ili mradi shughuli hiyo isimchukulie muda wa kumtumikia Mungu katika wito wake. Mchungaji ambaye anaishi kwa kutegemea zaidi kazi zake binafsi anaweza kukosa mzigo na muda wa kulea kanisa analochunga. Hata hivyo, mchungaji asijisahau pale kanisa linapojitahidi kumtunza. Aonyeshe shukurani hata kama kanisa halijafikia matarajio yake bila kusahau kwamba hakuajiriwa na kanisa (washirika) bali ameajiriwa na Mungu ambaye ana njia nyingi za kumbariki. Hata Bwana Yesu, si kila aliyemhudumia kiroho alihusika katika kutimiza mahitaji yake ya kimwili. Maandiko yanataja watu wachache tu ambao walimhudumia Bwana Yesu kwa mali zao (Lk 8:3).

3. Mchungaji anahitaji kutambuliwa kibinadamu (human understanding) kama walivyo waumini. Mchungaji anaweza kuwa mpweke katika kundi lake mwenyewe kama hakuna mtu anayetambua hisia zake. Mtu mwenye ufahamu wa rohoni akimwona mchungaji wake anakuwa mkali kupita kiasi, hatalaumu na kutafuta kuhama kanisa bali atatafuta kujua nini kinaendelea katika maisha ya mchungaji wake. Kama mchungaji ameshindwa kulipa ada ya mtoto wake au amelala njaa, hawezi kuwa na mahubiri yenye baraka. Kanisa lina wajibu wa kujua changamoto anazopitia mchungaji wake na kuzitafutia ufumbuzi hata kwa maneno tu ya kutia moyo. Maneno yanayotia moyo wachungaji ni maneno kama vile kazi yako ni njema, uwe na moyo mkuu na maneno mengine kama hayo. Tusiwe na macho yanayoona madhaifu ya wachungaji peke yake bali pia tuone uwezo wao au mazuri yao. Na hata kama wamekosea leo, tusisahau walivyowahi kutusaidia kabla hawajakosea. Hata kama baba yako mzazi atakosea leo, bado utaendelea kumuita baba. Mbona baba zetu wa kiroho tunawasahau mapema sana? Paulo alipokataliwa kama mtume alisema wengine wanaweza kunikataa lakini sio ninyi. 1 Kor 9:2 ‘Kwa maana ikiwa mimi si mtume kwa wengine, lakini ni mtume kwenu ninyi’. Usipende kufuata mkumbo katika kumkataa mtumishi wa Mungu ambaye amewahi kuwa hazina kwako.

4. Mchungaji anahitaji washirika wampende, wajitiishe katika uongozi wake na wamuombee. 1 The 5:12,13 ‘Lakini, ndugu, tunataka mwatambue wale wanaojitaabisha kwa ajili yenu, na kuwasimamia ninyi katika Bwana, na kuwaonyeni; mkawastahi sana katika upendo, kwa ajili ya kazi zao’. Mchungaji  akifanyiwa matendo ya upendo naye ataitikia kwa huduma yenye upendo. Ingawa mchungaji amepewa huduma hii na Bwana, bado anahitaji mwitikio mzuri wa watu anaowaongoza. Tusione ni wajibu wake kututumikia hata kama hatuonyeshi matendo ya huruma na upendo kwake. Kama anaagiza jambo na wewe ukashindwa kulitekeleza, jifunze kumjulisha mapema au kumuomba samahani ili asikudhanie kwamba umemdharau.  Hata kama umemzidi umri, elimu au kipato; jifunze kujitiisha kwake kwa vile hutapoteza chochote kwa kufanya hivyo. Kama unashindwa kumheshimu kwa sababu zingine, mheshimu tu kwa ajili ya kazi yake aliyopewa. Kumbuka mchungaji akitumika kwa huzuni, kanisa linakosa baraka. Ebr 13:17 ‘Watiini wenye kuwaongoza na kuwanyenyekea …ili kwamba wafanye hivyo kwa furaha wala si kwa kuugua; maana isingewafaa ninyi’. Ingawa mchungaji amepewa mamlaka na wajibu wa kuwaombea wengine, anahitaji pia kuinuliwa kwa maombi kutoka kwa watu anaowahudumia.

Kipindi kijacho utajifunza kuhusu MAOMBI KWA AJILI YA MCHUNGAJI NA FAMILIA YAKE

Mwaliko

Tunajiandaa kumaliza mwaka na kuanza mwaka mwingine. Huduma tunayofanya inagusa na kujengea uwezo jamii bila kubagua dini wala dhehebu. Tunakualika uungane nasi kama rafiki-mwenza au mdau (partner) kwa mwaka 2025. Sio mpango wa Mungu umtumikie kiroho peke yake. Wewe una ujuzi, uwezo na uzoefu mkubwa ambao huutumii kwa ajili ya ufalme wa Mungu bali unautumia tu kazini kwako na katika maisha yako binafsi. Zipo huduma unazoweza kuzifanya hata kama uko mbali nasi. Shiriki katika maono haya yanayogusa ulimwengu mzima. Yapo mataifa ambayo haingekuwa rahisi kuyafikia lakini kupitia maono haya tumeweza kuyafikia.

Njia rahisi kuwasiliana nasi kwa ajili ya ufafanuzi zaidi kupitia hapa chini kwenye tovuti (angalia sehemu yenye kichwa cha WASILIANA NASI) au baruapepe (info@lawimshana.com) au kupitia Whatsapp (0712-924234).

Wewe ni mtu muhimu sana kwetu na mbele za Mungu.

Dr. Lawi Mshana, +255712-924234, Korogwe, Tanga, Tanzania