UNAJUA KWANINI BAADHI YA VIONGOZI WA IMANI WANA MAUMIVU KATIKA MAISHA YAO? (Kilio cha Wachungaji, Sura ya 2)
Utangulizi
Pengine unajisemea moyoni kwamba ujumbe huu haukuhusu kwa vile wewe sio mchungaji. Napenda ujue kwamba mtumishi wa Mungu akihuzunika kwa sababu yako unakaribisha laana katika maisha yako. Waebrania 13:17 “Watiini wenye kuwaongoza, na kuwanyenyekea; maana wao wanakesha kwa ajili ya roho zenu, kama watu watakaotoa hesabu, ili kwamba wafanye hivyo kwa furaha wala si kwa kuugua; maana isingewafaa ninyi.”
Ni ukweli usiopingika kwamba wakosoaji wakuu na wanaonyoshea kidole madhaifu ya viongozi wao wa imani HAWAJAWAHI KUWAOMBEA WALA KUTAFUTA NJIA YOYOTE YA KUWASAIDIA. Wanawachukulia wakati wote kwamba wanawakosea kwa makusudi.
Nitaeleza sura za kitabu hatua kwa hatua kwa kifupi. Lakini unaweza kusoma kwa kina zaidi kwa kununua kitabu cha karatasi za kawaida (hardcopy) au kitabupepe (ebook).
Sura ya Pili (kwa muhtasari)
Sababu Kuu za Maumivu ya Wachungaji
Kuingia
katika utumishi bila wito maalum, mifumo
mibovu na kandamizi ya madhehebu na makanisa wanayoyachunga, kuandaa kanisa
kiroho na kusahau kuliandaa kijamii na kiuchumi, kutosheka na maisha ya chini
ya kiwango, waumini kutotambua maumivu ya familia za wachungaji wao na kupata
upinzani usiokoma katika huduma.
Yapo mambo mengi yanayosababisha maumivu kwa wachungaji.
Nitazungumzia sababu kadhaa nilizogundua kwamba zinachangia zaidi maumivu hayo:
1.
Kuingia katika utumishi bila wito maalum:.
Katika utumishi kuna makundi makuu matatu.
· Kundi
la kwanza ni la watumishi ambao wametumwa na watu. Watumishi hawa wameingia
katika utumishi kwa msukumo wa watu wengine bila wao wenyewe kupata uthibitisho
wowote mioyoni mwao. Wanatumika kwa hofu ya kibinadamu bila hofu yoyote ya
Mungu. Hivyo wanachotafuta ni kulipendeza dhehebu hata kama jambo wanalolifanya
liko kinyume na maagizo ya Mungu.
· Kundi
la pili ni la watumishi waliojituma wenyewe. Watumishi hawa wameingia katika
huduma kwa kujitolea wenyewe kwa kuona hitaji bila kusikia msukumo wowote wa
Kimungu mioyoni mwao. Watumishi hawa wameamua kuingia katika huduma kwa vile
wanawahurumia watu au kwa vile wana muda wa kufanya huduma hiyo. Ni rahisi sana
watumishi wa aina hii kuchoka mapema kwa vile wanachunga kanisa kwa kutumia
karama ya masaidiano badala ya huduma ya kichungaji.
· Kundi
la tatu ni la watumishi waliotumwa na Mungu. Watumishi hawa wamesikia wito
mioyoni mwao wenyewe na kupata uthibitisho kwa njia kadhaa kama vile kupitia
katika Neno la Mungu, watu wengine, maono na unabii.
Kama mtumishi wa Mungu atagundua ametumwa wapi, wakati gani
na kwa kundi gani lazima huduma hiyo itafanikiwa. Hata hivyo, mafanikio ya
huduma hayapimwi kwa vipimo vya kibinadamu bali kwa viwango Mungu alivyomuwekea
mtumishi wake. Ndiyo maana Mtume Paulo alisema mwendo nimeumaliza wakati katika
kipindi chake hakufika Tanzania. Alijua kipimo alichopimiwa na Mungu.
Huduma sio cheo au wadhifa bali ni moyo wa Mungu kwa ajili
ya kuhudumia watu wake. Mtu anapopewa huduma ya kitume anapewa moyo wa tofauti
na mtu mwenye huduma ya kichungaji. Kama mtu hajui wito wake maalum anaweza
kutumika katika wito ambao Mungu hakumpa na hivyo kukosa baraka zilizokuwa
zimeandaliwa na Mungu kwa ajili yake. Hata hivyo, wapo watumishi wengine ambao
Mungu amewapa huduma zaidi ya moja. Ni
wajibu wa mtumishi wa aina hiyo kutambua huduma iliyo kubwa zaidi ndani yake
ili atumike zaidi katika huduma hiyo ndipo atapata upenyo mkubwa zaidi.
2. Mifumo mibovu na kandamizi ya madhehebu na
makanisa wanayoyachunga.
Yapo madhehebu ambayo hayana mfumo mzuri wa kujali maisha ya
watumishi wake. Viongozi wake wakuu wanajali tu makanisa yakue kiidadi ili
mapato ya dhehebu yaongezeke bila kupitia upya kiwango cha maisha na posho za
watumishi wake. Hata huo ukuaji wenyewe haufanyiwi tathmini. Ukifuatilia sana
sio ‘ukuaji wa kanisa’ bali ni ‘ukuaji wa dhehebu’ kwa vile wengi wanaojiunga
walishaokoka huko walikotoka. Na kibaya zaidi hawakuletwa na Bwana ili wapate
malezi bali ni ushawishi wa makusudi uliowafanya wahamie kanisa hilo jipya. Na
wengi wao tangu wahamie hadi leo hawajapokea yale waliyoahidiwa kwamba
watayapata. Tunapolazimika kuhamia kanisa jingine tuwe na sababu za msingi
mioyoni mwetu. Vinginevyo, tushirikiane tu na huduma zingine na kurudi kwetu
kwa vile kila kanisa la mahali (local church) ni kiungo tu katika mwili wa
Kristo (universal church) hivyo haliwezi kumtosheleza mtu kwa kila kitu.
Makanisa pia yana mikakati ya mamilioni ya kuendeleza
majengo na kununua vyombo vya muziki wakati mahitaji ya familia za wachungaji
hayashughulikiwi. Baadhi ya viongozi wakuu wanaona kama mchungaji kulala njaa
ndio wito wake. Hivyo, fedha nyingi zinapelekwa ngazi za juu za dhehebu na
kumuacha mchungaji bila kitu. Nimeshuhudia washirika kadhaa katika semina
ninazofundisha wakisema wameamua kukiuka utaratibu kandamizi wa madhehebu yao.
Hutashangaa pia kuona mkutano wa injili ukiandaliwa kwa
mamilioni ya fedha ambapo wahubiri na waimbaji wakija wanalala vyumba vya
watoto wa mchungaji vyenye vyandarua.
Watoto hao wanalazimika kuwapisha wageni na kulala sebuleni ambapo
wanaumwa na mbu au kulala kwa shida usiku kucha.
Ni makanisa machache yanayojali kuwawekea akiba ya uzeeni
wachungaji wake. Makanisa mengine yanakata posho za wachungaji wake lakini
fedha hizo hazipelekwi katika mfuko wa hifadhi ya jamii bali zinaliwa na
wajanja.
3.
Kuandaa kanisa kiroho na kusahau kuliandaa kijamii na kiuchumi.
Yapo makanisa ambayo yana mikakati mizuri sana ya maisha ya
kiroho ya washirika wake. Hata hivyo, mikakati yao haina matokeo mazuri kwa
vile haiwaandai waumini katika maeneo mengine ya maisha. Huduma ya Yesu
akitembea duniani iligusa maeneo yote ya maisha ya mwanadamu (holistic
ministry). Hatuna budi na sisi pia kujitahidi kugusa maeneo yote ya maisha ya mwanadamu,
yaani, mwili, nafsi na roho.
Hatukutumwa kuhubiri mikutano ya Injili peke yake bali pia
kukemea ubadhirifu wa fedha za makanisa na za wananchi zinazotolewa na
wahisani, mashirika, serikali na jamii. Lazima tuwe na mikakati ya kufikia
makundi yanayoishi katika mazingira magumu kama vile watu wanaoishi na virusi
vya UKIMWI, watoto, vijana, wazee na walemavu kwa kuwapa mafunzo, kutetea haki
zao na kuwapa misaada mbalimbali. Kutojali mahitaji ya kimwili na kihisia
kunaweza kutufanya tuikose mbingu hata kama tunatoa vizuri huduma za kiroho.
Wapo wanaodai kwamba mafundisho kuhusu mafanikio wameyapa
kipaumbele kikubwa. Lakini ukifuatilia sana mkazo wa mafundisho yao, ni kuhusu
‘utoaji’ peke yake. Kumbuka somo la utoaji linalenga kuwasaidia watu wawe waaminifu
katika kumtolea Mungu katika kile walicho nacho, wakati somo la uchumi
linawasaidia watu wawe na kipato kizuri na matumizi mazuri ili wamzalie Mungu
matunda na kuishi maisha bora.
Kama hatuko tayari kushirikiana na watu wengine,
tunajifungia nje ya baraka za Mungu na matokeo yake ni kuwabebesha mzigo
waumini tunaowachunga zaidi ya uwezo wao. Kimsingi, ugumu unaowapata wachungaji
wengi, unatokana na ubaguzi wa kimadhehebu unaowafanya wawe wenyeji wa makundi
yao wanayoyachunga peke yake.
4.
Kutosheka na maisha ya chini ya kiwango.
Wapo wachungaji ambao wanadhani utumishi ni kuteseka wakati
wote. Kwa hiyo, kwa upande wao maisha ya raha ni anasa na ni dhambi. Wapo
tayari kujitesa hata pale ambapo Mungu anataka kuwatia moyo na kuwaburudisha.
Biblia inatuagiza turidhike na vitu tulivyo navyo (1 Tim 6:6) lakini hii
haimaanishi tutosheke na vitu tulivyo navyo.
Ni vizuri zaidi kwa mchungaji na mwenzi wake (mkewe au
mumewe) kutambua kiasi cha fedha kinachohitajika kwa mwezi kwa ajili ya familia
na kisha kumwambia Mungu aliyewaita badala ya kusubiri kumshukuru Mungu kwa
chochote watakachokipata. Katika hili hatuhitaji kuangalia uwezo wa kiuchumi wa
waumini tunaowachunga bali ukubwa wa mahitaji yetu na uwezo wa Mungu. Lazima
pia tutambue kwamba Biblia haisemi fedha yenyewe ni mbaya bali inasema kibaya
ni ‘kupenda fedha’.
5.
Waumini kutotambua maumivu ya familia za wachungaji wao
Waumini wengi hawatambui
maumivu na mateso ya wachungaji wao. Wanafunzi wa Yesu hawakutambua kwa nini
Yesu amechagua kwenda nao katika maombi. Hawakujua kinachoendelea moyoni mwake.
Wachungaji wakipata matatizo ni watu wachache sana makanisani wanaoonyesha
kujali na kama watajali ni kwa mchungaji peke yake na si kwa mkewe na watoto
wake. Mzigo wa huduma waliokuwa nao awali kwa ajili ya wachungaji wao umepungua
kama sio kutoweka kabisa.
Zipo sababu mbalimbali
zinazowafanya waumini wapoteze shauku. Mojawapo ni kwamba kadiri kanisa
linavyokua, ndivyo majukumu ya mchungaji yanavyoongezeka na kumfanya mchungaji
ashindwe kuwatembelea washirika mara kwa mara kama walivyokuwa wamezoea. Pia
hali ya mchungaji kimaisha inapoanza kuwa nzuri au Mungu anapomuinulia watu
wanaomjali, wapo waumini wanaoanza kumuonea wivu badala ya kufurahia mafanikio
yake. Mt 26:8,9 ’Wanafunzi wake
walipoona, wakachukiwa, wakasema, Ni wa nini upotevu huu? Maana marhamu hii
ingaliweza kuuzwa kwa fedha nyingi wakapewa maskini’. Kuna watu wakiona
mchungaji amefanikiwa, wanaamua kuacha kutoa zaka (sehemu ya kumi ya mapato
yao) katika kanisa analochunga ingawa bado wanahitaji mafundisho yake, maombi
yake na ushauri wake. Kufanya hivi ni kutafuta laana na kusahau kwamba si kazi
ya muumini kupanga matumizi ya zaka bali jukumu lake ni kumtolea Mungu kama
Neno lilivyoagiza. Kama mtu ameona hakubaliani na utaratibu wa utoaji uliowekwa
na kanisa husika, asiyaasi maono wakati bado anaendelea kupokea msaada wa
kiroho kupitia huduma hiyo. Labda tu kama amepata maelekezo maalum kutoka kwa
Mungu kutokana na ubadhirifu wa fedha uliopo au kutokana na sababu za Mungu
mwenyewe ambazo zinampa amani moyoni na ambazo hazipingani na Neno la Mungu.
Mchungaji anaweza kusafiri
kwa muda mrefu na washirika wasikumbuke kuiangalia familia yake aliyoiacha
nyumbani. Wanashindwa hata kutembelea tu familia ya mchungaji wao ili kuijulia
hali. Wanasubiri wasikie mchungaji amerudi ndipo wafike kumuona, tena kwa ajili
ya kumshirikisha matatizo yao tu. Wakati mwingine waumini wajifunze pia
kushirikisha baraka wanazopata ili wasiwachoshe watumishi wa Mungu. Gal 6:6 ’Mwanafunzi na amshirikishe mkufunzi wake
katika mema yote’. Mchungaji pia kama mtu mwingine yeyote anahitaji kuwa
karibu na familia yake mara tu anaporudi safari. Hata kama yeye mwenyewe haoni
hilo, mkewe na watoto wanamuhitaji. La kushangaza unaweza kukuta washirika
wanapomtembelea mchungaji wanaongea naye hadi usiku wa manane na kusahau kwamba
wanainyang’anya familia yake faragha. Lazima busara itumike katika mahusiano
yetu na familia za wachungaji ili tuwe baraka badala ya kuwa kero. Wajibu wa
kwanza wa mchungaji, ni kwa Bwana; wa pili, ni kwa familia yake na wa tatu, ni
kwa kanisa. Mungu alianzisha familia kabla ya kuanzisha kanisa hivyo tuheshimu
mpangilio wake. Hivyo, tunapomkuta mchungaji anaongea na mkewe au watoto wake
tutambue kwamba yuko pia katika kazi ya Mungu.
Ni wachache wanaotambua
kwamba mchungaji anachoka baada ya huduma hivyo anahitaji kupumzika. Unagundua
udhaifu huu kwa kuona jinsi watu wanavyokuwa wengi wakimsubiri mchungaji baada
ya ibada kwa matatizo ya kawaida badala ya kuomba wapangiwe siku ya kumuona
katikati ya wiki. Washirika wengine wanaona kwamba katikati ya wiki hawataweza
kuvunja shughuli zao kuja kumuona mchungaji. Hivyo wanataka wamalizane naye
siku hiyohiyo ya ibada kuu.
Ni lazima tuwe na huruma na
tutambue muda unaofaa kumshirikisha mchungaji masuala nyeti. Si wakati wote
unafaa kumshirikisha mchungaji kila jambo. Mhu 3:1 ’Kwa kila jambo kuna majira yake, na wakati kwa kila kusudi chini ya
mbingu’. Tuombe hekima ya Mungu kama malkia Esta ili tujue wakati muafaka wa kushirikisha masuala nyeti. Sio
busara kumshirikisha mchungaji suala nyeti la kiroho wakati umemkuta anasikiliza
taarifa ya habari au anakula chakula. Soma mazingira na nyakati kabla ya
kushirikisha mahitaji yako yanayohitaji majibu makini.
6.
Kupata upinzani usiokoma katika huduma.
Wapo waachungaji ambao wamepata upinzani katika huduma kwa
miaka mingi kiasi kwamba wamepoteza imani na viongozi wakuu wa madhehebu yao.
Wengine wametengenezewa kesi ili tu wafukuzwe halafu wengine wachukue nafasi
zao. Tena wamefukuzwa kwa kazi ambazo waliwekeza nguvu zao na mali zao kwa
miaka mingi na kusahau hata kujenga nyumba zao binafsi. Kilio hiki kiko kwa
wengi na kimechangia sana kuwa na utitiri wa madhehebu ambayo ukifuatilia sana
yana imani moja na mfumo mmoja. Kwa vile madhehebu mengi hayakuandaliwa kupokea
maono mapya, hayana fursa ya kuingiza maono mapya kutoka kwa Bwana.
Kwa wengine, vita inaanzia ndani ya kanisa hasahasa kwa wale
ambao wanafurahia kupokea vikundi vinavyojimega kutoka kanisa jingine. Mara
nyingi kikundi kilichojimega kutoka kanisa jingine, kinakuja na mchungaji wake
wa siri. Siku huyo mchungaji wa siri akiasi maono aliyoyakuta, kikundi hicho
kinaweza kutoka naye na kubeba wengine kadhaa ambao kiliwakuta.
Wakati mwingine vita ya ndani inaanzishwa na mchungaji
mwenyewe kwa kuweka matajiri katika uongozi hata kama ni wachanga kiroho au
wamehamia tu siku za karibuni kutoka mahali pengine na hawajayaelewa vizuri
maono ya kanisa hilo. 1 Tim 3:6 ‘Wala
asiwe mtu aliyeongoka karibu, asije akajivuna akaanguka katika hukumu ya
Ibilisi’. Mchungaji anaweza kudanganyika kwamba kwa kuwapa majukumu wageni
hao matajiri, atawafanya wadumu katika kanisa lake bila kuhamia kanisa
jingine. Anasahau kwamba kanisa
linakuzwa na Bwana na sio kwa ujanja. Pia anasahau kwamba mtu ambaye hujawahi
kumuona akiwa amekasirika, hujamfahamu bado. Ni vigumu kujua mgeni ataitikaje
siku atakapokemewa kwa kosa alilolifanya. Tunahitaji muda wa kutosha katika
kufahamu vizuri uwezo na udhaifu wa mgeni kabla ya kumuingiza katika maeneo
nyeti ya huduma.
Vita nyingine inaweza kuanzia ndani ya familia ya mchungaji.
Kama huduma ya mchungaji haikamilishani na ya mkewe bali zinashindana, ni
rahisi kushindwa kuinuana katika utumishi. Ikiwa mchungaji na mwenzi wake wote
ni wahubiri, kila mmoja anaweza kuangalia makosa ya mwenzake na kujisemea
moyoni, ‘Kama angenipisha nihubiri mimi, ningetumiwa na Mungu zaidi kuliko
yeye’. Hivyo anakosekana wa kumuombea mwenzake. Badala yake, kama huduma
zinakamilishana (complementary), mmoja anajisikia fahari anapomuona mwenzake
akitumika hivyo anamtia moyo zaidi na kumuombea. Mchungaji anahitaji kutiwa
moyo na watu wa nyumbani mwake. Mchungaji anapotiwa moyo na watu wengine kuliko
mwenzi wake wa maisha, upendo wake unaweza kuhamia kwa watu wengine na kufungua
mlango wa dhambi. Wanandoa wanapaswa kulindana kwa kuonyeshana upendo kwa
vitendo badala ya kutumia maandiko ya Biblia peke yake katika kudai upendo. Mtu
yeyote anayetaka kupendwa, anatakiwa kupendeza na kujali mahitaji ya mwenzake
na sio kudai peke yake wala kulaumu.
Kipindi
kijacho utajifunza kuhusu KUWANUSURU WACHUNGAJI KUTOKA KATIKA MAUMIVU
Soma kwa
kina utangulizi hadi sura hii kupitia kiungo hiki https://www.lawimshana.com/p/books-vitabu.html
Nakukaribisha
kutoa sadaka yako ya upendo kwa ajili ya kuwezesha huduma hii tunayoitoa bure ingawa
inalipiwa mtandaoni
TigoPesa:
+255 712 924234
Mpesa:
+255 754 653217
CRDB
Bank: 0152219784300
Dkt. Lawi Mshana


