Ticker

6/recent/ticker-posts

(Maswali na Majibu) Na 2. Kwanini Wakristo hatuzai watoto wengi na tunaoa mke mmoja


 Na 2: Kwanini Wakristo hatuzai watoto wengi na tunaoa mke mmoja?

Mwanzo 1:28 “Mungu akawabarikia, Mungu akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho juu ya nchi.”

Hili ni moja ya maandiko yanayotumiwa na wengi katika kuzungumzia mpango wa Mungu kuhusu uzazi. Hata hivyo kuna mambo kadhaa ambayo mimi binafsi ninajifunza kupitia andiko hilo.

1. Mungu alisema ZAENI MKAONGEZEKE kwa mume na mke mmoja tu (Adamu na Hawa) wakati hakuna wenye dhambi duniani.

Ndiyo maana alitangulia kuwabariki kwanza kabla ya kuwaagiza kuongezeka. Mungu alitoa agizo la kuzaa na kuongezeka kwa Adamu na Hawa kabla ya anguko la dhambi halafu akarudia wakati wa Nuhu baada ya kuwaangamiza wenye dhambi katika uso wa nchi kwa gharika. Mwa 9:1 “Mungu akambariki Nuhu na wanawe, akawaambia, Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi.” Kwa hiyo shauku kubwa ya Mungu ni kuona wenye haki wanaongezeka na sio wenye dhambi. Kwa tafsiri ya leo tunaweza kusema kwamba jambo la muhimu zaidi kwa Mungu ni kuona wengi wanazaliwa mara ya pili (wanaokoka) na kuingizwa katika Ufalme Wake ili waweze kulibeba Jina lake na kutangaza haki yake.

2. Mungu hakuishia katika kusema watu wazae na kuongezeka bali alisema MKAIJAZE NCHI.

Mungu hakukusudia watu waongezeke kwa hasara. Alitaka wanapoongezeka watumie vizuri raslimali zilizopo. Kuijaza nchi sio kujaa kama mihogo iliyopangwa kwenye kikapu bali ni kuhakikisha hakuna maeneo ambayo yamekaa tu bila kutumika kwa faida. Mungu hakukusudia nchi ijazwe na watu wavivu ambao wamezungukwa na vichaka ambavyo wameshindwa kuviendeleza. Wapo watu wamezungukwa na vichaka lakini wameshindwa kupanda hata miti ya matunda huku wakitegemea kuomba ruhusa ya kuchuma matunda kwenye miti ya majirani zao kila siku.

3. Mungu alitaka baada ya watu wake kuijaza nchi WAITIISHE.

Lazima tujiulize kiasi gani tumeitiisha au kuitawala dunia yetu. Kwa lugha nyingine kiasi gani dunia inatutumikia sisi. Kinyume chake watu wengi wanaitumikia dunia badala ya dunia kuwatumikia. Mungu alitaka tuwe na mamlaka juu ya dunia tunayoishi. Tunufaike na mali tulizo nazo na kuweza kuzitiisha roho zozote zinazoinuka kinyume na mpango wa Mungu kwetu. Mathayo 17:20 “Yesu akawaambia, Kwa sababu ya upungufu wa imani yenu. Kwa maana, amin, nawaambia, Mkiwa na imani kiasi cha punje ya haradali mtauambia mlima huu, Ondoka hapa uende kule; nao utaondoka; wala halitakuwako neno lisilowezekana kwenu.” Mungu ametupa uwezo wa kusema na milima iliyosimama mbele ya ndoto zetu na iweze kutusikia na kuhamia kule tunakotaka iende.

4. Baada ya kuitiisha dunia, Mungu alisema MKATAWALE viumbe vya baharini, vya nchi kavu na vya angani.

La kusikitisha ni kwamba kazi ya kutunza mazingira tuliyopewa na Mungu tumeiachia serikali. Tumeshindwa kufanya hata vile ambavyo tunaweza kufanya. Tunafanya usafi wa mazingira yetu kwa kuogopa kuadhibiwa na serikali. Tunatakiwa kujua kwamba anayefuga kuku na kunufaika nazo kwa sehemu amewatawala ndege. Mtu mwenye imani kwa Mungu (Elohim) hawezi kutawala kwa kuongea tu bila vitendo. Yakobo 2:26 “Maana kama vile mwili pasipo roho umekufa, vivyo hivyo na imani pasipo matendo imekufa.” Hatuwezi kuendelea kuhubiri tu kwamba Mungu anaweza mambo yote wakati sisi wenyewe tumeshindwa maisha. Tukiwa hivyo tutakuwa tuna shida mahali fulani.

5. Lakini pia tujue kwamba Adamu na Hawa ni wawakilishi wa vizazi vyote vya wanadamu.

Hivyo Mungu alipowaambia zaeni mkaongezeke hakumaanisha kwamba hiyo kazi ya kuongezeka na kuijaza nchi wataifanya peke yao kama wanandoa katika kipindi cha uhai wao. Ukifuatilia sana katika Biblia hakuna familia moja ilizaa watoto wengi kwa kisingizio cha kuongezeka na kuijaza nchi. Hata Yakobo alipata watoto 12 kupitia wanawake wanne tofauti ambao ni Raheli, Lea, Bilha na Zilpa (Mwa 29,30). Kwa hiyo ukizaa mtoto mmoja au watoto kumi umechangia katika kuijaza nchi kwa vile hakuna idadi maalum iliyotolewa. Ukweli ni kwamba HATA KAMA TAFSIRI YA KUIJAZA NCHI NI YA KUZAA WATOTO WENGI, SI MPANGO WA MUNGU KWAMBA UIJAZE NCHI WEWE PEKE YAKO. Lazima tusaidiane kupitia familia zetu mbalimbali.

Kwanini Wakristo tunaoa mke mmoja

1. Tunafuata maelekezo ya Bwana Yesu aliyosema tangu mwanzo Mungu aliumba mtu mume na mtu mke na kwamba talaka haikuanzishwa na Mungu

Mathayo 19:4 “Akajibu, akawaambia, Hamkusoma ya kwamba yeye aliyewaumba mwanzo, aliwaumba mtu mume na mtu mke.”

Alijibu Mafarisayo Mk 10:2-9 “2 Basi Mafarisayo wakamwendea, wakamwuliza, Je! Ni halali mtu kumwacha mkewe? Huku wakimjaribu. 3 Naye akajibu, akawaambia, Musa aliwaamuru nini? 4 Wakasema, Musa alitoa ruhusa kuandika hati ya talaka na kumwacha. 5 Yesu akawaambia, Kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu aliwaandikia amri hii. 6 Lakini tangu mwanzo wa kuumbwa ulimwengu, aliwafanya mume na mke. 7 Kwa sababu hiyo mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; 8 na hao wawili watakuwa mwili mmoja; hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja. 9 Basi alichokiunganisha Mungu, mwanadamu asikitenganishe.”

Alijibu wanafunzi wake. Mk 10:11,12 “Akawaambia, Kila mtu atakayemwacha mkewe na kuoa mwingine azini juu yake; na mke, akimwacha mumewe na kuolewa na mtu mwingine, azini.na mke, akimwacha mumewe na kuolewa na mtu mwingine, azini.

Mt 19:8,9 “Akawaambia, Musa, kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu, aliwapa ruhusa kuwaacha wake zenu; lakini tangu mwanzo haikuwa hivi. Nami nawaambia ninyi, Kila mtu atakayemwacha mkewe, isipokuwa ni kwa sababu ya uasherati, akaoa mwingine, azini; naye amwoaye yule aliyeachwa azini.”

2. Baada ya Yesu kuja, kufa na kufufuka hatuishi tena katika nyakati za ujinga

Matendo ya Mitume 17:30,31 “Basi, zamani zile za ujinga Mungu alijifanya kama hazioni; bali sasa anawaagiza watu wote wa kila mahali watubu. Kwa maana ameweka siku atakayowahukumu walimwengu kwa haki, kwa mtu yule aliyemchagua; naye amewapa watu wote uthabiti wa mambo haya kwa kumfufua katika wafu.”

Kina Ibrahimu na Yakobo waliishi kipindi cha ujinga kabla Bwana Yesu aliye hekima yake Mungu kuja duniani. 1 Kor 1:24 “bali kwao waitwao, Wayahudi kwa Wayunani, ni Kristo, nguvu ya Mungu, na hekima ya Mungu.”

3. Hata hivyo mtu akimwamini Yesu haruhusiwi kumuacha mkewe au mumewe na akiwa ana mke zaidi ya mmoja atatakiwa kubaki na mmoja lakini hatakiwi kutelekeza familia yake kwa mahitaji ya maisha.

1 Kor 7:9-16 “9 Lakini ikiwa hawawezi kujizuia, na waoe; maana ni afadhali kuoa kuliko kuwaka tamaa. 10 Lakini wale waliokwisha kuoana nawaagiza; wala hapo si mimi, ila Bwana; mke asiachane na mumewe; 11 lakini, ikiwa ameachana naye, na akae asiolewe, au apatane na mumewe; tena mume asimwache mkewe. 12 Lakini watu wengine nawaambia mimi, wala si Bwana, ya kwamba iwapo ndugu mmoja ana mke asiyeamini, na mke huyo anakubali kukaa naye asimwache. 13 Na mwanamke, ambaye ana mume asiyeamini, na mume huyo anakubali kukaa naye, asimwache mumewe. 14 Kwa maana yule mume asiyeamini hutakaswa katika mkewe; na yule mke asiyeamini hutakaswa katika mumewe; kama isingekuwa hivyo, watoto wenu wangekuwa si safi; bali sasa ni watakatifu. 15 Lakini yule asiyeamini akiondoka, na aondoke. Hapo huyo ndugu mume au ndugu mke hafungiki. Lakini Mungu ametuita katika amani. 16 Kwa maana wajuaje, wewe mwanamke, kama utamwokoa mumeo? Au wajuaje, wewe mwanamume, kama utamwokoa mkeo?”

Maana ya neno ‘hafungiki’. Je ina maana anaruhusiwa kuoa au kuolewa tena? Tutambue kwamba ndoa sio kifungo (bondage/dedoulotai). Kwa hiyo alimaanisha hana sababu ya kumng’ang’ania (aheshimu uamuzi wake) bali ajali amani (asitengeneze mazingira mabaya). Haina maana kwamba anaruhusiwa kuoa au kuolewa. Kama itakuwa anaruhusiwa kuoa au kuolewa Paulo atakuwa anajipinga mwenyewe na atakuwa anapingana na Bwana Yesu jambo ambalo sio kweli. Lk 16:18 “Kila amwachaye mkewe na kumwoa mke mwingine azini; naye amwoaye yeye aliyeachwa na mumewe azini.”

Dr. Lawi Mshana, Tanzania